M’Cheyne Bible Reading Plan
Yohana Atayarisha Njia kwa Ajili ya Yesu
(Mt 3:1-12; Lk 3:1-9,15-17; Yh 1:19-28)
1 Mwanzo wa Habari Njema za Yesu Masihi,[a] Mwana wa Mungu,[b] 2 zilianza kama vile Nabii Isaya alivyosema zitaanza, aliandika,
“Sikiliza! Nitamtuma mjumbe mbele yako.
Yeye ataandaa njia kwa ajili yako.”(A)
3 “Kuna mtu anayeipaza sauti yake toka nyikani:
‘Tayarisheni njia kwa ajili ya Bwana;
nyoosheni njia kwa ajili yake.’”(B)
4 Naye Yohana akaja, akiwabatiza watu huko nyikani huku akiwahubiri watu ujumbe kutoka kwa Mungu. Aliwaambia wabatizwe kuonesha kuwa wamekubali kubadili maisha yao ndipo dhambi zao zitasamehewa. 5 Watu kutoka Yerusalemu na maeneo yote ya Uyahudi walikwenda kwa Yohana Mbatizaji; huko waliungama matendo yao mabaya kwake naye akawabatiza katika Mto Yordani.
6 Huyo Yohana alivaa mavazi yaliyofumwa kutokana na manyoya ya ngamia. Naye alijifunga mkanda wa ngozi kuzunguka kiuno chake, na alikula nzige na asali mbichi.
7 Yeye alitangaza yafuatayo: “Yupo mwingine ajaye baada yangu, mwenye nguvu zaidi kuliko mimi. Nami niliye mtumwa wa chini kabisa sistahili hata kuinama na kufungua kamba za viatu vyake.[c] 8 Mimi nawabatiza katika maji, lakini yeye huyo atawabatiza katika Roho Mtakatifu.”
Yohana Ambatiza Yesu
(Mt 3:13-17; Lk 3:21-22)
9 Ikatokea katika siku hizo Yesu alikuja toka Nazareti uliokuwa mji wa Galilaya akabatizwa na Yohana katika mto Yordani. 10 Mara tu aliposimama kutoka ndani ya maji, Yesu aliona mpasuko ukitokea angani, akamwona Roho akishuka chini kuja kwake kama njiwa. 11 Sauti ikasikika toka mbinguni, “Wewe ni mwanangu, ninayekupenda, napendezwa nawe sana.”
Yesu Ajaribiwa na Shetani
(Mt 4:1-11; Lk 4:1-13)
12 Kisha baada ya kutokea mambo haya Roho Mtakatifu alimchukua Yesu na kumpeleka nyikani,[d] 13 naye akawa huko kwa siku arobaini, ambapo alijaribiwa na Shetani. Yesu alikuwa nyikani pamoja na wanyama wa porini, na malaika walimhudumia.
Yesu Aanza Kazi yake Galilaya
(Mt 4:12-17; Lk 4:14-15)
14 Baada ya Yohana kuwekwa gerezani, Yesu akaja katika wilaya karibu na Ziwa Galilaya, huko aliwatangazia watu Habari Njema kutoka kwa Mungu. 15 Akasema, “Wakati umefika. Ufalme wa Mungu umewafikia.[e] Mbadili mioyo yenu na maisha yenu, na kuiamini habari njema!”
Yesu Achagua Baadhi ya Wafuasi
(Mt 4:18-22; Lk 5:1-11)
16 Alipokuwa akitembea kando kando ya Ziwa Galilaya, Yesu alimwona Simoni[f] na Andrea ndugu yake. Hao walikuwa wavuvi na walikuwa wakizitupa nyavu zao ziwani kukamata samaki. 17 Yesu akawaambia, “njooni mnifuate, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa aina nyingine, nitawafundisha jinsi ya kukusanya watu badala ya samaki.” 18 Mara moja, Simoni na Andrea wakaziacha nyavu zao na kumfuata.
19 Kisha Yesu akaendelea mbele kidogo na akawaona ndugu wawili, Yakobo mwana wa Zebedayo na kaka yake Yohana. Yesu aliwaona wakiwa kwenye mashua wakiandaa nyavu zao za kuvulia samaki. 20 Naye akawaita mara moja. Hivyo wakamwacha baba yao Zebedayo katika mashua na watu waliowaajiri na kumfuata Yesu.
Yesu Amweka Huru Mtu Kutoka Pepo Mchafu
(Lk 4:31-37)
21 Kisha Yesu na wafuasi wake waliingia Kapernaumu. Siku ya Sabato Yesu aliingia katika sinagogi na akaanza kuwafundisha watu. 22 Walishangaa sana namna alivyokuwa akifundisha. Hakufundisha kama walimu wao wa sheria; alifundisha kwa mamlaka.[g] 23 Ndani ya sinagogi alikuwemo mtu aliyepagawa na pepo mchafu. Naye mara alipiga kelele na kusema, 24 “Unataka nini kwetu, Yesu wa Nazareti? Je, umekuja kutuangamiza? Ninajua wewe ni nani. Wewe ni Mtakatifu wa Mungu.”
25 Lakini Yesu akamkemea na kumwambia, “Nyamaza kimya, na kisha umtoke ndani yake.” 26 Ndipo roho yule mchafu akamfanya mtu yule atetemeke. Kisha akatoa sauti kubwa na kisha akamtoka.
27 Kila mmoja akashangazwa sana kiasi cha kuwafanya waulizane, “Hii ni nini? Ni mafundisho ya aina mpya, na mtu yule anafundisha kwa mamlaka! Yeye huwapa amri pepo wachafu nao wanamtii!” 28 Hivyo habari kuhusu Yesu zikaenea haraka katika eneo lote la Galilaya.
Yesu Awaponya Watu Wengi
(Mt 8:14-17; Lk 4:38-41)
29 Wakaondoka kutoka katika sinagogi na mara hiyo hiyo wakaenda pamoja na Yakobo na Yohana hadi nyumbani kwa Simoni na Andrea. 30 Mara Yesu alipoingia ndani ya nyumba watu wakamweleza kuwa mama mkwe wake Simoni alikuwa mgonjwa sana na alikuwa amepumzika kitandani kwa sababu alikuwa na homa. 31 Yesu akasogea karibu na kitanda, akamshika mkono na kumsaidia kusimama juu. Ile homa ikamwacha, na yeye akaanza kuwahudumia.
32 Ilipofika jioni, baada ya jua kuzama waliwaleta kwake watu wote waliokuwa wagonjwa na waliokaliwa na mashetani. 33 Mji mzima ulikusanyika mlangoni pale. 34 Naye akawaponya watu waliokuwa na magonjwa ya kila aina, na kufukuza mashetani wengi. Lakini yeye hakuyaruhusu mashetani kusema, kwa sababu yalimjua.[h]
Yesu Aenda Katika Miji Mingine
(Lk 4:42-44)
35 Asubuhi na mapema, ilipokuwa giza na bado hakujapambazuka, Yesu aliamka na kutoka kwenye nyumba ile na kwenda mahali ili awe peke yake na kuomba. 36 Lakini Simoni na wale wote waliokuwa pamoja naye waliondoka kwenda kumtafuta Yesu 37 na walipompata, wakamwambia, “kila mmoja anakutafuta.”
38 Lakini Yesu akawaambia, “Lazima twende kwenye miji mingine iliyo karibu na hapa, ili niweze kuhubiri huko pia, kwa sababu hilo ndilo nililokuja kulifanya.” 39 Hivyo Yesu alienda katika wilaya yote iliyoko mashariki mwa ziwa la Galilaya akihubiri Habari Njema katika masinagogi na kuwafungua watu kutoka katika nguvu za mashetani.
Yesu Amponya Mgonjwa
(Mt 8:1-4; Lk 5:12-16)
40 Ikatokea mtu mmoja mwenye ugonjwa mbaya sana wa ngozi akamwendea Yesu na kupiga magoti hadi chini akimwomba msaada. Mtu huyo mwenye ugonjwa mbaya sana wa ngozi akamwambia Yesu, “Kama utataka, wewe una uwezo wa kuniponya nikawa safi.”
41 Aliposikia maneno hayo Yesu akakasirika.[i] Lakini akamhurumia. Akautoa mkono wake na kumgusa mtu yule mwenye ugonjwa mbaya sana wa ngozi, na kumwambia, “Ninataka kukuponya. Upone!” 42 Mara moja ugonjwa ule mbaya sana wa ngozi ulimwacha, naye akawa safi.
43 Baada ya hayo Yesu akampa maonyo yenye nguvu na kumruhusu aende zake mara moja. 44 Akamwambia, “Usimwambie mtu yeyote kilichotokea. Lakini nenda kwa kuhani akakuchunguze,[j] Na umtolee Mungu sadaka ambazo Musa aliamuru[k] watu wanaoponywa watoe, ili iwe ushahidi kwa watu kwamba umepona kwa kuwa safi tena. Ukayafanye haya ili yawe uthibitisho kwa kila mmoja ya kwamba umeponywa.” 45 Lakini mtu yule aliondoka hapo na kwenda zake, na huko alianza kuzungumza kwa uhuru kamili na kusambaza habari hizo. Matokeo yake ni kwamba Yesu asingeweza tena kuingia katika mji kwa wazi wazi. Ikamlazimu kukaa mahali ambapo hakuna watu. Hata hivyo watu walikuja toka miji yote na kumwendea huko.
1 Salamu kutoka kwa Paulo, mtumishi wa Kristo Yesu.[a]
Mungu alinichagua niwe mtume na akanipa kazi ya kuhubiri Habari Njema yake. 2 Tangu zamani, kwa vinywa vya manabii katika Maandiko Matakatifu, Mungu aliahidi kwamba angewaletea Habari Njema watu wake. 3 Habari Njema hii inahusu Mwana wa Mungu, ambaye kama mwanadamu, alizaliwa katika ukoo wa Mfalme Daudi. 4 Na alipofufuliwa na Roho Matakatifu[b] kutoka kwa wafu, alipewa mamlaka kamili ya kutawala kama Mwana wa Mungu. Ni Yesu Kristo, Bwana wetu.
5 Kupitia kwa Yesu, Mungu amenionyesha wema wake. Na amenipa mamlaka ya kuwaendea watu wa mataifa yote na kuwaongoza kumwamini na kumtii yeye. Kazi yote hii ni kwa ajili yake. 6 Nanyi pia ni miongoni mwa waliochaguliwa na Mungu ili mmilikiwe na Yesu Kristo.
7 Waraka huu ni kwa ajili yenu ninyi nyote mlio huko Rumi. Kwani Mungu anawapenda na amewachagua kuwa watu wake watakatifu.
Ninamwomba Mungu Baba yetu na Bwana wetu Yesu Kristo, wawape ninyi neema na amani.
Maombi ya Shukrani
8 Kwanza, ninamshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kwa ajili yenu ninyi nyote. Ninamshukuru yeye kwa sababu kila mahali ulimwenguni watu wanazungumza kuhusu imani yenu kuu. 9-10 Kila wakati ninapoomba, ninawakumbuka ninyi daima. Mungu anajua kuwa hii ni kweli. Yeye ndiye ninayemtumikia kwa moyo wangu wote nikiwaambia watu Habari Njema kuhusu Mwanaye. Hivyo ninaendelea kuomba kwamba mwishowe Mungu atanifungulia njia ili niweze kuja kwenu. 11 Ninataka sana niwaone na niwape zawadi ya kiroho ili kuimarisha imani yenu. 12 Ninamaanisha kuwa ninataka tusaidiane sisi kwa sisi katika imani tuliyo nayo. Imani yenu itanisaidia mimi, na imani yangu itawasaidia ninyi.
13 Kaka zangu na dada zangu, ninataka mjue kwamba nimepanga mara nyingi kuja kwenu, lakini jambo fulani hutokea na kubadili mipango yangu kila ninapopanga kuja. Juu ya kazi yangu miongoni mwenu, ningependa kuona matokeo yale yale mazuri yakitokea ya kazi yangu miongoni mwa watu wengine wasio Wayahudi.
14 Imenilazimu kuwatumikia watu wote; waliostaarabika na wasiostaarabika,[c] walioelimika na wasio na elimu. 15 Ndiyo sababu ninataka sana kuzihubiri Habari Njema kwenu ninyi pia mlio huko Rumi.
16 Kwa mimi hakuna haya[d] katika kuhubiri Habari Njema. Ninayo furaha kwa sababu Habari Njema ni nguvu ya Mungu inayomwokoa kila anayeamini, yaani inawaokoa Wayahudi kwanza, na sasa inawaokoa Mataifa.[e] 17 Ndiyo, wema wa uaminifu wa Mungu umedhihirishwa katika Habari Njema kwa uaminifu wa mmoja, ambao huongoza imani ya wengi. Kama Maandiko yanavyosema, “Aliye na haki mbele za Mungu[f] ataishi kwa imani.”[g]
Mungu ni Mwaminifu Na Atauadhibu Uovu
18 Mungu huonesha hasira yake kutokea mbinguni dhidi ya mambo mabaya ambayo waovu hutenda. Hawamheshimu na wanatendeana mabaya. Maisha yao maovu yanasababisha ukweli kuhusu Mungu usijulikane. 19 Hili humkasirisha Mungu kwa sababu wamekwisha oneshwa Mungu alivyo. Ndiyo, Mungu ameliweka wazi kwao.
20 Yapo mambo yanayoonekana kuhusu Mungu, kama vile nguvu zake za milele na yale yote yanayomfanya awe Mungu. Lakini tangu kuumbwa kwa ulimwengu, mambo haya yamekuwa rahisi kwa watu kuyaona. Maana yake ni kuwa, watu wanaweza kumwelewa Mungu kwa kuangalia yale aliyoumba. Hivyo watu hawana udhuru kwa uovu wanaotenda.
21 Watu walimjua Mungu, lakini hawakumheshimu kama Mungu. Na hawakumpa shukrani. Badala yake waliyageukia mambo ya hovyo yasiyo na manufaa. Akili zao zilichochanganyikiwa zilijaa giza. 22 Walisema kuwa wana hekima, lakini wakawa wajinga. 23 Hawakuuheshimu ukuu wa Mungu, anayeishi milele. Wakaacha kumwabudu Mungu wakaanza kuabudu sanamu, vitu vilivyotengenezwa vikaonekana kama wanadamu, ambao wote mwisho hufa, au kwa mfano wa ndege na wanyama wanaotembea na wanaotambaa.
24 Hivyo Mungu akawaacha wazifuate tamaa zao chafu. Wakawa najisi na wakaivunjia heshima miili yao kwa njia za uovu walizotumia. 25 Waliibadili kweli kuhusu Mungu kwa uongo. Wakasujudu na kuabudu vitu alivyoviumba Mungu badala ya kumwabudu Mungu aliyeviumba vitu hivyo. Yeye ndiye anayepaswa kusifiwa milele yote. Amina.
26 Hivyo, kwa kuwa watu hawakumheshimu Mungu, Mungu akawaacha wafuate tamaa zao za aibu. Wanawake wao wakabadili namna ya kujamiiana na wakawatamani wanawake wenzao na wakajamiiana wao kwa wao. 27 Wanaume wakafanya vivyo hivyo. Wakaacha kujamiiana na wanawake kwa mfumo wa asili, wakaanza kuwawakia tamaa wanaume wenzao. Wakafanya mambo ya aibu na wanaume na wavulana. Wakajiletea aibu hii juu yao wenyewe, wakapata yale waliyostahili kwa kutelekeza kweli.
28 Watu hawa waliona kuwa haikuwa muhimu kwao kumkubali Mungu katika fikra zao. Hivyo Mungu akawaacha wayafuate mawazo yao mabaya. Hivyo hufanya mambo ambayo mtu yeyote hapaswi kufanya. 29 Maisha yao yamejaa kila aina ya matendo mabaya, uovu, tamaa na chuki. Wamejaa wivu, uuaji, ugomvi, uongo na hamu ya kuwadhuru wengine. Wanasengenya 30 na kusemana maovu wao wenyewe. Wanamchukia Mungu. Ni wakorofi, wana kiburi na hujivuna. Hubuni njia za kufanya maovu. Hawawatii wazazi wao. 31 Ni wapumbavu, hawatimizi ahadi zao. Hawawaoneshi wema wala huruma wengine. 32 Wanajua amri ya Mungu kuwa yeyote anayeishi kwa namna hiyo lazima afe. Lakini si tu kwamba wanaendelea kufanya mambo haya wenyewe, bali wanakubaliana na wengine wanaofanya mambo hayo.
© 2017 Bible League International