Book of Common Prayer
Upendo wa Paulo kwa Waamini wa Korintho
11 Nimekuwa nikizungumza kama mjinga, lakini ninyi ndiyo mliosababisha nikafanya hivyo. Ninyi ndiyo mnaopaswa kuzungumza mema juu yangu. Mimi si kitu, lakini mimi si myonge kwa njia yeyote ile kwa hao “mitume wakuu”. 12 Nilipokuwa pamoja nanyi, nilifanya kwa uvumilivu wote vitu vilivyo nilidhihirisha kuwa mimi ni mtume kwa ishara, maajabu na miujiza. 13 Kwa hiyo mlipokea kila kitu ambacho makanisa yote yalipata. Kitu kimoja tu ndicho kilikuwa cha tofauti na cha kipekee: Sikuwa mzigo au msumbufu kwenu. Mnisamehe kwa hilo.
14 Niko tayari sasa kuwatembelea kwa mara ya tatu, na sitakuwa mzigo kwenu. Mimi sitafuti kitu chochote kilicho chenu. Ninawataka ninyi tu. Watoto wasiweke akiba vitu vya kuwapa wazazi wao. Wazazi wanapaswa kuweka akiba vitu vya kuwapa watoto wao. 15 Kwa hiyo ninayo furaha kutumia kile nilichonacho kwa ajili yenu. Na mimi mwenyewe nitajitoa kikamilifu kwa ajili yenu. Je, kama upendo wangu kwenu utakuwa mkubwa, upendo wenu kwangu utapungua?
16 Ni wazi kuwa sikuwa mzigo kwenu, lakini baadhi yenu wanadhani kuwa nilikuwa mjanja, na kutumia hila kuwaweka mtegoni. 17 Je, niliwadanganya kwa kuwatumia mtu yeyote kati ya wale niliyowatuma kwenu? Mnafahamu kuwa sikufanya hivyo. 18 Nilimwomba Tito aje kwenu, na nilimtuma kaka yetu afuatane naye. Tito hakuwadanganya, je alifanya hivyo? Hapana! Na kwa hiyo mjue kuwa matendo yangu na tabia yangu ilikuwa ya dhati kama ilivyokuwa kwake.
19 Je! Mnadhani tumekuwa tukijitetea? Hapana, tunasema haya katika Kristo na mbele za Mungu. Ninyi ni rafiki zetu wapendwa, na kila tunachofanya tunakifanya ili muwe imara. 20 Ninafanya hivi kwa sababu ninaogopa kuwa nitakapokuja, hamtakuwa kama vile ninavyotaka muwe. Na pia nina wasiwasi kuwa sitakuwa kwa namna ile mnayotaka mimi niwe. Nina hofu kuwa nitawakuta mkibishana, wenye wivu, wenye hasira, mkipigana kwa ubinafsi wenu, wenye misemo mibaya, watetaji, wenye kiburi, na machafuko huko. 21 Nina wasiwasi kuwa nitakapokuja kwenu, Mungu wangu ataninyenyekeza tena mbele yenu. Nitalazimika kuomboleza kwa ajili ya wale ambao wametenda dhambi. Wengi wao hawajarejea na kutubia maisha yao ya uovu, dhambi za zinaa, na mambo ya aibu waliyotenda.
Yesu Aulilia Mji wa Yerusalemu
41 Yesu alipoukaribia mji wa Yerusalemu, akautazama kisha akaanza kuulilia, 42 akisema, “Laiti ungelijua leo kile kinachokuletea amani. Lakini kimefichwa kwako usikijue sasa. 43 Wakati unakuja, ambao adui zako watajenga ukuta kukuzunguka na kukuzingira pande zote. 44 Watakuteketeza wewe na watu wako wote. Hakuna jiwe hata moja katika majengo yako litaachwa juu ya jiwe jingine. Haya yote yatatokea kwa sababu hukujua wakati ambao Mungu alikuja kukuokoa.”
Yesu Asafisha Eneo la Hekalu
(Mt 21:12-17; Mk 11:15-19; Yh 2:13-22)
45 Yesu aliingia katika eneo la Hekalu. Akaanza kuwafukuza watu waliokuwa wanauza vitu humo. 46 Akasema, “Maandiko yanasema, ‘Hekalu langu litakuwa nyumba ya sala.’(A) Lakini mmeligeuza kuwa ‘maficho ya wezi.’”(B)
47 Yesu aliwafundisha watu kila siku katika eneo la Hekalu. Viongozi wa makuhani, walimu wa sheria na baadhi ya viongozi wa watu walikuwa wakitafuta namna ya kumwua. 48 Lakini hawakujua namna ambavyo wangefanya, kwa sababu alikuwa anazungukwa na watu kila wakati waliokuwa wakimsikiliza. Kila mtu alifurahia yale ambayo Yesu alikuwa anasema, hawakuacha kumsikiliza.
© 2017 Bible League International