Book of Common Prayer
Uwe tayari kwa ujio wa Bwana
5 Na sasa ndugu zangu, hatuna haja ya kuwaandikia juu ya nyakati na tarehe. 2 Ninyi mnafahamu vizuri kuwa siku ambayo Bwana atakuja itakuwa ya kushitukiza, kama mwizi anavyokuja usiku. 3 Watu watasema, “tuna amani na tuko salama.” Wakati huo ndipo uharibifu utakapowajia haraka, kama maumivu anayoyapata mwanamke anapojifungua. Na watu hao hawataweza kukwepa.
4 Lakini ninyi ndugu zangu, hamuishi katika giza. Na hivyo ile siku haitawashangaza kama mwivi. 5 Nyote ni watu wa nuru. Ni watu wa mchana. Hatuko katika usiku wala giza. 6 Hivyo tusiwe kama watu wengine. Tusiwe wasinziao. Tuwe macho na wenye kiasi. 7 Watu walalao, hulala usiku. Watu wanywao kupita kiasi, hunywa usiku. 8 Bali sisi ni watu wa mchana, hivyo tujitawale wenyewe. Tuvae imani na upendo vitulinde. Na tumaini la wokovu liwe kwetu kama kofia ya vita.
9 Mungu hakutuchagua tuangamie katika hasira yake. Mungu alituchagua tuwe na wokovu katika Bwana wetu Yesu Kristo. 10 Yesu alikufa kwa ajili yetu ili tuishi pamoja nae. Haijalishi kama tu hai au wafu atakapokuja. 11 Hivyo farijianeni ninyi kwa ninyi na msaidiane kukua imara katika imani, kama mnavyofanya sasa.
7 Na unapoomba usiwe kama watu wasiomjua Mungu. Wao kila wanapoomba wanarudia maneno yale yale, tena na tena, wakidhani kuwa wanapoyarudia maneno hayo mara nyingi watasikiwa na Mungu na kujibiwa maombi yao. 8 Msiwe kama wao. Baba yenu anajua yale mnayohitaji kabla hamjamwomba. 9 Hivyo, hivi ndivyo mnapaswa kuomba:
‘Baba yetu uliye mbinguni,
Jina lako lipewe utukufu.
10 Ufalme wako uje.
Mapenzi yako yafanyike hapa dunia,
kama yanavyofanyika huko mbinguni.
11 Utupe leo chakula tunachohitaji.
12 Utusamehe dhambi zetu,
kama tunavyowasamehe wale wanaotukosea.
13 Usiruhusu tukajaribiwa,
lakini utuokoe na Yule Mwovu.’[a]
14 Mkiwasemehe wengine makosa waliyowatendea, Baba yenu wa mbinguni naye atawasamehe makosa yenu pia. 15 Lakini msipowasamehe wengine, Baba Yenu wa mbinguni hatawasamehe ninyi.
© 2017 Bible League International