Book of Common Prayer
Jiwe Lililo Hai na Taifa Takatifu
2 Hivyo acheni uovu wote, pamoja na uongo, hali za unafiki na wivu na aina zote za kashfa. 2 Kama watoto wachanga, mnapaswa kuyatamani maziwa ya kiroho yaliyo safi, ili kwa ajili ya hayo muweze kukua na kuokolewa, 3 kwa vile mmekwisha kuujaribu wema wa Bwana.
4 Mkaribieni Bwana Yesu, aliye Jiwe lililo Hai, lililokataliwa na watu, bali kwa Mungu ni jiwe lililoteuliwa na kuheshimika. 5 Ninyi pia, kama mawe yaliyo hai mnajengwa ili kuwa hekalu la kiroho. Mmekuwa makuhani watakatifu mkimtumikia Mungu kwa kutoa sadaka za kiroho zinazokubalika kwake kwa njia ya Yesu Kristo. 6 Hivyo, Maandiko yanasema,
“Tazameni, naweka katika Sayuni Jiwe la msingi katika jengo,
lililoteuliwa na kuheshimika,
na yeyote anayeamini hataaibishwa.”(A)
7 Inamaanisha heshima kwenu mnaoamini, bali kwa wasioamini,
“jiwe walilolikataa wajenzi
limekuwa jiwe la muhimu kuliko yote.”(B)
8 Na,
“jiwe linalowafanya watu wajikwae
na mwamba unaowafanya watu waanguke.”(C)
Walijikwaa kwa sababu hawakuutii ujumbe wa Mungu, na Mungu alisema hilo litatokea wasipotii.
9 Lakini ninyi ni watu mlioteuliwa, ni Ukuhani unaomtumikia Mfalme. Ninyi ni taifa takatifu nanyi ni watu wa Mungu. Yeye aliwaita Ili muweze kutangaza matendo yake yenye nguvu. Naye aliwaita mtoke gizani na mwingie katika nuru yake ya ajabu.
10 Kuna wakati hamkuwa watu,
lakini sasa mmekuwa watu wa Mungu.
Kuna wakati hamkuoneshwa rehema,
lakini sasa mmeoneshwa rehema za Mungu.
Yesu ni Kama Mzabibu
15 Yesu akasema, “Mimi ndiye mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. 2 Yeye hulikata kutoka kwangu kila tawi lisilozaa matunda.[a] Pia hupunguza majani katika kila tawi linalozaa matunda ili kuliandaa liweze kuzaa matunda zaidi. 3 Ninyi mmewekwa tayari[b] kwa ajili ya kuzaa matunda[c] kutokana na mafundisho yale niliyowapa. 4 Hivyo mkae mkiwa mmeunganishwa kwangu, nami nitakaa nikiwa nimeunganishwa kwenu. Hakuna tawi linaloweza kuzaa matunda likiwa liko peke yake. Ni lazima liwe limeunganishwa katika mzabibu. Ndivyo ilivyo hata kwenu. Hamwezi kutoa matunda mkiwa peke yenu. Ni lazima muwe mmeunganishwa kwangu.
5 Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi. Mtatoa matunda mengi sana mkiwa mmeunganishwa kwangu, nami nimeunganishwa kwenu. Lakini mkitenganishwa mbali nami hamtaweza kufanya jambo lo lote. 6 Kama hamtaunganishwa nami, basi mtakuwa sawa na tawi lililotupwa pembeni nanyi mtakauka. Matawi yote yaliyokufa jinsi hiyo hukusanywa, hutupwa katika moto na kuchomwa. 7 Hivyo ninyi mbaki mmeunganishwa nami, na mfuate mafundisho yangu. Mkifanya hivyo, mnaweza kuomba kitu chochote mnachohitaji, nanyi mtapewa. 8 Ninyi mdhihirishe kuwa mmekuwa wafuasi wangu kwa kutoa matunda mengi. Kwani hiyo itamletea Baba utukufu.[d]
9 Mimi nimewapenda kama vile Baba alivyonipenda. Sasa mdumu katika upendo wangu. 10 Nimezitii amri za Baba yangu, naye anaendelea kunipenda. Kwa jinsi hiyo, nami nitaendelea kuwapenda mkizitii amri zangu. 11 Nimewaambia haya ili mpate furaha ya kweli kama ile niliyonayo mimi. Nami ninatamani muwe na furaha iliyo kamilifu.
© 2017 Bible League International