Book of Common Prayer
Msiwafuate Maadui wa Kristo
18 Wapendwa wanangu, mwisho umekaribia! Mmesikia kuwa adui wa Kristo anakuja. Na sasa maadui wengi wa Kristo tayari wapo hapa. Hivyo tunajua kwamba mwisho umekaribia. 19 Maadui hawa walikuwa miongoni mwetu, lakini walituacha. Hawakuwa wenzetu hasa. Kama wangelikuwa kweli wenzetu, wangebaki pamoja nasi. Lakini walituacha. Hii inaonesha kuwa hakuna hata mmoja wao aliyekuwa kwa hakika mwenzetu.
20 Mnayo karama[a] aliyowapa Yeye Aliye Mtakatifu.[b] Hivyo nyote mnaijua kweli. 21 Mnadhani ninawaandikia waraka huu kwa sababu hamuijui kweli? Hapana! Ninawaandikia kwa sababu mnaijua kweli. Na mnajua kuwa hakuna uongo utokao katika kweli.
22 Ni nani basi aliye mwongo? Ni yeye anayesema kuwa Yesu siyo Kristo. Yeyote anayesema hivyo ni adui wa Kristo. Yeye huyo asiyemwamini Baba wala Mwana. 23 Yeyote asiyemwamini Mwana hana Baba, ila yeye anayemkubali Mwana anaye Baba pia.
24 Mnapaswa kuendelea kuyafuata mafundisho mliyoyasikia tangu mwanzo. Kama mkifanya hivyo, mtakuwa siku zote katika Mwana na katika Baba. 25 Na hili ndilo ambalo Mwana ameliahidi kwetu sisi, uzima wa milele.
26 Ninawaandikia barua hii juu ya wale ambao wanataka kuwapotosha katika njia isiyo sahihi. 27 Kristo aliwapa karama maalumu.[c] Nanyi bado mngali na karama hiyo ndani yenu. Hivyo hamumhitaji yeyote kuwafundisha. Karama aliyowapa inawafundisha juu ya kila jambo. Ni karama ya kweli, si ya uongo. Hivyo endeleeni kuishi katika Kristo, kama karama yake ilivyowafundisha.
28 Ndiyo, wanangu wapendwa, ishini ndani yake. Kama tukifanya hivyo, hatutakuwa na hofu siku kristo atakapo kuja tena. Hatutahitaji kujificha na kuwa na aibu ajapo. 29 Mnajua ya kwamba daima Kristo alifanya yaliyo ya haki. Vivyo hivyo mnajua pia ya kwamba wote watendao haki ni watoto wa Mungu.
19 Kwa mara nyingine tena Wayahudi wakagawanyika juu ya yale aliyoyasema Yesu. 20 Wengi wao wakasema, “Pepo mchafu amemwingia na kumfanya awe mwendawazimu. Kwa nini sisi tumsikilize?”
21 Lakini wengine wakasema, “Haya siyo maneno ya mtu anayeendeshwa na pepo mchafu. Pepo mchafu hawezi kuponya macho ya mtu asiyeona.”
Viongozi wa Kiyahudi Wasimama Kinyume na Yesu
22 Ulikuwa ni wakati wa baridi, na wakati wa Sikukuu ya Kuweka Wakfu[a] kule Yerusalemu. 23 Yesu alikuwa katika eneo la Hekalu katika Ukumbi wa Sulemani. 24 Viongozi wa Kiyahudi wakakusanyika kumzunguka. Wakasema, “Ni mpaka lini utatuacha na mashaka juu yako? Kama wewe ndiwe Masihi, basi tuambie wazi wazi.”
25 Yesu akajibu, “Nilikwisha kuwaambia tayari, lakini hamkuamini. Nafanya miujiza katika jina la Baba yangu. Miujiza hii inaonesha mimi ni nani. 26 Lakini hamuamini, kwa sababu ninyi siyo kondoo wangu. 27 Kondoo wangu huisikia sauti yangu. Nami nawajua, nao hunifuata. 28 Mimi nawapa kondoo wangu uzima wa milele. Nao hawatakufa kamwe, na tena hakuna atakayemchukua yeyote kutoka mkononi mwangu. 29 Baba yangu ndiye aliyenipa hao, naye ni mkuu kuliko wote.[b] Hakuna anayeweza kuwaiba kondoo wangu kutoka mkononi mwangu. 30 Mimi na Baba tu umoja.”
© 2017 Bible League International