Book of Common Prayer
Muwe Makini Jinsi Mnavyoishi
12 Mmekuwa dhaifu, hebu mjitie nguvu tena. 13 Muishi katika njia iliyo sahihi ili muweze kuokolewa na udhaifu wenu hautawasababisha ninyi kupotea.
14 Jitahidini kuishi kwa amani na kila mtu. Na mjitahidi kuyaweka mbali na dhambi maisha yenu. Yeyote ambaye maisha yake siyo matakatifu hawezi kumwona Bwana. 15 Muwe makini ili mtu asije akakosa kuipata neema ya Mungu. Muwe makini ili asiwepo atakayepoteza imani yake na kuwa kama gugu chungu linalomea miongoni mwenu. Mtu wa jinsi hiyo anaweza kuharibu kundi lenu lote. 16 Muwe makini ili asiwepo yeyote atakayefanya dhambi ya uzinzi au kushindwa kumheshimu Mungu moyoni kama alivyofanya Esau. Kama kijana mkubwa katika nyumba ya babaye, Esau angerithi sehemu kubwa ya vitu kutoka kwa baba yake. Lakini akauza kila kitu kwa mlo mmoja tu. 17 Mnakumbuka kwamba baada ya Esau kufanya hivi, akataka kupata baraka za baba yake. Akaitamani sana baraka ile kiasi kwamba akalia. Lakini baba yake akakataa kumpa baraka hiyo, kwa sababu Esau hakupata njia ya kubadili yale aliyotenda.
18 Ninyi ni watu wa Mungu, kama watu wa Israeli walipofika katika Mlima Sinai. Lakini hamjaufikia mlima halisi wa kuweza kushikwa. Mlima huo haupo kama ule waliouona, uliokuwa ukiwaka moto na kufunikwa na giza, utusitusi na dhoruba. 19 Haipo sauti ya tarumbeta au sauti iliyoyasema maneno kama hayo waliyoyasikia. Walipoisikia sauti, wakasihi kamwe wasisikie neno lingine. 20 Hawakutaka kusikia amri: “Kama chochote, hata mnyama, akigusa mlima, lazima kiuawe kwa kupigwa mawe.”(A) 21 Kile walichoona kilikuwa cha kutisha kiasi kwamba Musa akasema, “Natetemeka kwa hofu.”(B)[a]
22 Lakini mmeufikia Mlima Sayuni, kwenye mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni.[b] Mmefika mahali ambapo maelfu wa malaika wamekusanyika kusherehekea. 23 Mmefika katika kusanyiko la watoto wazaliwa wa kwanza wa Mungu. Majina yao yameandikwa mbinguni. Mmemfikia Mungu, hakimu wa watu wote. Na mmefika kwenye roho za watu wema ambao wamekamilishwa. 24 Mmemfikia Yesu; yeye aliyelileta kutoka kwa Mungu agano jipya kwenda kwa watu wake. Mmefika kwenye damu iliyonyunyizwa[c] ambayo inasema habari za mema zaidi kuliko damu ya Habili.
25 Muwe makini na msijaribu kupuuza kusikiliza Mungu anaposema. Watu wale walipuuza kumsikiliza yeye alipowaonya hapa duniani. Nao hawakuponyoka. Sasa Mungu anasema kutoka mbinguni. Hivyo sasa itakuwa vibaya zaidi kwa wale watakaopuuza kumsikiliza yeye. 26 Alipozungumza pale mwanzoni, sauti yake iliitetemesha dunia. Lakini sasa ameahidi, “Kwa mara nyingine tena nitaitetemesha dunia, lakini pia nitazitetemesha mbingu.”(C) 27 Maneno “Kwa mara nyingine” yanatuonyesha kwa uwazi kwamba kila kitu kilichoumbwa kitaangamizwa; yaani, vitu vinavyoweza kutetemeshwa. Na ni kile tu kisichoweza kutetemeshwa kitakachobaki.
28 Hivyo tunahitajika kuwa na shukrani kwa sababu tunao ufalme ambao hauwezi kutetemeshwa. Na kwa sababu sisi ni watu wa shukrani, tunahitajika kumwabudu Mungu kwa njia itakayompendeza yeye. Tunahitajika kufanya hivi kwa heshima na hofu, 29 kwa sababu “Mungu wetu yuko kama moto unaoweza kutuangamiza sisi.”(D)
Yesu Afundisha Yerusalemu
14 Sherehe ile ilipokaribia kuisha, Yesu akaenda katika maeneo ya Hekalu na kuanza kufundisha. 15 Viongozi wa Kiyahudi waliomsikiliza walishangazwa na kusema, “Mtu huyu amejifunza wapi mambo haya yote? Yeye hakuwahi kupata mafundisho kama yale tuliyonayo.”
16 Yesu akajibu, “Ninayofundisha siyo yangu. Mafundisho yangu yanatoka kwake Yeye aliyenituma. 17 Watu wanaotaka kufanya kwa uhakika kama anavyotaka Mungu watafahamu kuwa mafundisho yangu yanatoka kwa Mungu. Watafahamu kwamba mafundisho haya siyo yangu. 18 Kama ningeyafundisha mawazo yangu, ningekuwa najitafutia heshima yangu mwenyewe. Lakini kama najaribu kumletea heshima Yeye aliyenituma, basi naweza kuaminiwa. Yeyote anayefanya kama hivyo hawezi kusema uongo. 19 Musa aliwapa sheria, sivyo? Lakini hamuitii hiyo sheria. Kama mnaitii, kwa nini basi mnataka kuniua?”
20 Watu wakamjibu Yesu, “Pepo amekuchanganya akili! Sisi hatuna mipango ya kukuua!”
21 Yesu akawambia, “Nilitenda ishara moja siku ya Sabato, na wote mkashangaa. 22 Lakini mnatii sheria aliyowapa Musa kuhusu kutahiriwa; nanyi mnatahiri hata siku ya Sabato! (Lakini hakika, Musa siye aliyewatahiri. Tohara Ilitoka kwa baba zenu walioishi kabla ya Musa.) Ndiyo, siku zote mnatahiri wana wenu hata siku ya Sabato. 23 Hii inaonesha kuwa mtu anaweza kutahiriwa siku ya Sabato ili kuitimiza sheria ya Musa. Sasa kwa nini mnanikasirikia mimi kwa kuuponya mwili wote wa mtu siku ya Sabato? 24 Acheni kuhukumu mambo ya watu kwa jinsi mnavyoyaona. Muwe makini kutoa kuhukumu kwa njia ya haki kabisa.”
Watu Wajiuliza Ikiwa Yesu Ni Masihi
25 Kisha baadhi ya watu waliokuwepo Yerusalemu wakasema, “Huyo ndiye mtu wanayetaka kumuua. 26 Lakini anafundisha mahali ambapo kila mtu anaweza kumwona na kumsikia. Wala hakuna anayejaribu kumzuia kufundisha. Inawezekana viongozi wamekubali kuwa kweli yeye ni Masihi. 27 Lakini Masihi halisi atakapokuja, hakuna atakayejua anakotoka. Nasi tunajua nyumbani kwake mtu huyu ni wapi.”
28 Yesu alikuwa bado anafundisha katika eneo la Hekalu aliposema kwa sauti, “Ni kweli mnanijua mimi na kule ninakotoka? Niko hapa, lakini siyo kwa matakwa yangu. Nilitumwa na Yeye aliye wa kweli. Lakini ninyi hamumjui. 29 Mimi namfahamu kwa sababu ninatoka kwake. Naye Ndiye aliyenituma.”
30 Yesu aliposema hivi, watu wakajaribu kumkamata. Lakini hakuna aliyethubutu hata kumgusa, kwa sababu wakati unaofaa kufanya hivyo ulikuwa bado haujafika. 31 Hata hivyo watu wengi wakamwamini Yesu. Wakasema, “Je, tunafikiri kuna haja ya kuendelea kumngojea Masihi mwingine aje atakayetenda ishara nyingine zaidi ya zile alizotenda mtu huyu?”
Viongozi wa Kiyahudi Wajaribu Kumkamata Yesu
32 Mafarisayo wakasikia yale ambayo watu walikuwa wakiyasema juu ya Yesu. Kwa sababu hiyo viongozi wa makuhani na Mafarisayo wakawatuma walinzi wa Hekalu kwenda kumkamata. 33 Kisha Yesu akasema, “Nitakuwa nanyi kwa muda mfupi. Kisha nitarudi kwake Yeye aliyenituma. 34 Ninyi mtanitafuta, lakini hamtaniona. Nanyi hamwezi kuja kule nitakapokuwa.”
35 Hawa Wayahudi wakaambiana wao kwa wao, “Huyu mtu atakwenda wapi sisi tusikoweza kufika? Je, anaweza kwenda kwenye miji ya Wayunani wanamoishi watu wetu? Je, atawafundisha Wayunani katika miji hiyo? 36 Anasema, ‘Mtanitafuta, lakini hamtaniona.’ Vile vile anasema, ‘Hamwezi kuja kule nitakapokwenda.’ Maana yake ni nini?”
© 2017 Bible League International