Revised Common Lectionary (Complementary)
Luka Aandika Kitabu Kingine
1 Mpendwa Theofilo:
Katika kitabu cha kwanza niliandika kuhusu kila kitu ambacho Yesu alitenda na kufundisha tangu mwanzo 2 mpaka siku alipochukuliwa juu mbinguni. Kabla hajaondoka, alizungumza na mitume aliowachagua kwa msaada wa Roho Mtakatifu kuhusu mambo waliyotakiwa kufanya. 3 Hii ilikuwa baada ya kifo chake, ambapo aliwathibitishia kwa namna nyingi kuwa alikuwa hai. Mitume walimwona Yesu mara nyingi kwa muda wa siku arobaini baada ya kufufuka kutoka kwa wafu. Naye Yesu alizungumza nao kuhusu ufalme wa Mungu. 4 Wakati mmoja Yesu alipokuwa akila pamoja nao, aliwaambia wasiondoke Yerusalemu. Aliwaambia, “Kaeni hapa mpaka mtakapopokea kile ambacho Baba aliahidi kutuma. Kumbukeni, niliwaambia juu yake. 5 Yohana aliwabatiza watu kwa maji, lakini baada ya siku chache mtabatizwa kwa Roho Mtakatifu.”
Yesu Achukuliwa Juu Mbinguni
6 Mitume walipokuwa pamoja, walimwuliza Yesu, “Bwana, huu ni wakati wako wa kuwarudishia Waisraeli ufalme wao tena?”
7 Yesu akawaambia, “Baba peke yake ndiye mwenye mamlaka ya kuamua tarehe na nyakati. Si juu yenu kujua. 8 Lakini Roho Mtakatifu atawajia na kuwapa nguvu. Nanyi mtakuwa mashahidi wangu. Mtawahubiri watu kuhusu mimi kila mahali, kuanzia humu Yerusalemu, Uyahudi yote, katika Samaria na hatimaye kila mahali ulimwenguni.”
9 Baada ya kusema haya, alichukuliwa juu mbinguni. Walipokuwa wanaangalia juu angani, wingu lilimficha na hawakuweza kumwona. 10 Walikuwa bado wanatazama angani alipokuwa anakwenda. Ghafla malaika wawili waliovaa mavazi meupe wakasimama pembeni mwao. 11 Wakasema, “Enyi watu wa Galilaya, kwa nini mmesimama hapa na mnatazama angani? Mlimwona Yesu akichukuliwa kutoka kwenu kwenda mbinguni. Atarudi katika namna hii hii kama mlivyomwona akienda.”
Sala ya Paulo
15-16 Ndiyo sababu daima ninawakumbuka katika maombi yangu na ninamshukuru Mungu kwa ajili yenu. Nimekuwa nikifanya hivi tangu niliposikia kuhusu imani yenu katika Bwana Yesu na upendo wenu kwa watu wote wa Mungu. 17 Daima ninamwomba Baba aliye mkuu na mwenye utukufu, Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Ninaomba awape Roho anakayewawezesha kuijua kweli kuhusu Mungu na awasaidie kuzielewa kweli hizo ili mweze kumjua vyema.
18 Ninaomba Mungu afungue mioyo yenu ili mwone kweli yake. Kisha mtalijua tumaini alilochagua kwa ajili yetu. Mtajua kuwa baraka ambazo Mungu amewaahidi watu wake ni nyingi na zimejaa utukufu. 19 Na mtajua kuwa uweza wa Mungu ni mkuu sana kwetu sisi tunaoamini. Ni sawa na nguvu zake kuu 20 alizotumia kumfufua Kristo kutoka kwa wafu na kumweka akae upande wa kulia wa kiti chake cha enzi huko mbinguni. 21 Amemweka Kristo juu ya watawala wote, mamlaka zote, nguvu zote na wafalme wote. Amempa mamlaka juu ya kila kitu chenye nguvu katika ulimwengu huu na ujao. 22 Mungu alikiweka kila kitu chini ya nguvu za Kristo na kumfanya kuwa kichwa cha kila kitu kwa manufaa ya kanisa. 23 Kanisa ndiyo mwili wa Kristo, yeye ndiye amejaa ndani ya kanisa. Anakikamilisha kila kitu katika kila namna.
44 Yesu akawaambia, “Mnakumbuka nilipokuwa pamoja nanyi? Nilisema kila kitu kilichoandikwa kuhusu mimi katika Sheria ya Musa, vitabu vya manabii na Zaburi lazima kitimilike.”
45 Kisha Yesu akawafafanulia Maandiko ili waelewe maana yake halisi. 46 Yesu akawaambia, “Imeandikwa kuwa Masihi atauawa na atafufuka kutoka kwa wafu siku ya tatu. 47-48 Mliona mambo haya yakitokea, ninyi ni mashahidi. Na maandiko yanasema inawapasa mwende na kuwahubiri watu kuwa ni lazima wabadilike na kumgeukia Mungu, ili awasamehe. Ni lazima mwanzie Yerusalemu na mhubiri ujumbe huu kwa jina langu kwa watu wa mataifa yote. 49 Kumbukeni kwamba nitamtuma kwenu yule ambaye Baba yangu aliahidi. Kaeni jijini mpaka mtakapopewa nguvu hiyo kutoka mbinguni.”
Yesu Arudi Mbinguni
(Mk 16:19-20; Mdo 1:9-11)
50 Yesu akawaongoza wafuasi wake kutoka nje ya Yerusalemu hadi karibu na Bethania. Akanyenyua mikono yake na kuwabariki wafuasi wake. 51 Alipokuwa anawabariki, alitenganishwa nao na kuchukuliwa mbinguni. 52 Wafuasi wake walimwabudu, kisha wakarudi Yerusalemu wakiwa na furaha sana. 53 Walikuwa katika Hekalu wakati wote, wakimsifu Mungu.
© 2017 Bible League International