Book of Common Prayer
19-20 Hivyo ndivyo tunavyojua kuwa sisi tu wa ile njia ya kweli. Pale mioyo yetu inapotufanya tujisikie kuwa na hatia, bado tunaweza kuwa na amani mbele za Mungu, kwa sababu Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu. Yeye anajua kila kitu.
21 Rafiki zangu wapendwa, ikiwa hatujisikii kuwa tunatenda yasiyo haki, basi hatupaswi kuwa na hofu tunapoenda kwa Mungu. 22 Na Mungu anatupa kile tunachomwomba. Nasi tunapokea kwa sababu tunazitii amri za Mungu na kufanya yanayompendeza. 23 Hili ndilo Mungu analoliamuru: Kwamba tumwamini Mwanaye Yesu Kristo, na kwamba tupendane sisi kwa sisi kama alivyoamuru. 24 Wote wanaozitii amri za Mungu wanaishi ndani ya Mungu. Na Mungu anaishi ndani yao. Tunajuaje kuwa Mungu anaishi ndani yetu? Tunajua kwa sababu ya Roho aliyetupa sisi.
Yohana Aonya juu ya Walimu wa Uongo
4 Rafiki zangu wapenzi, manabii wengi wa uongo wapo duniani sasa. Hivyo msiiamini kila roho, lakini zijaribuni hizo roho ili muone kama zinatoka kwa Mungu. 2 Hivi ndivyo mwezavyo kuitambua Roho ya Mungu. Roho inayosema, “Naamini kuwa Yesu ni Masihi aliye kuja duniani na akafanyika mwanadamu.” Roho hiyo inatoka kwa Mungu. 3 Roho inayokataa kutamka hayo juu ya Yesu, hii ni roho iliyo adui kwa Kristo. Mmesikia kuwa adui wa kristo anakuja, na sasa amekwishakuja naye yupo tayari ulimwenguni.
4 Wanangu wapenzi, ninyi ni wa Mungu, hivyo mmeshawashinda tayari hawa manabii wa uongo. Hii ni kwa sababu yule aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliyeko duniani. 5 Wao ni wa ulimwengu. Hivyo kile wanachokisema ni cha ulimwengu pia. Na ulimwengu husikia kile wanachokisema. 6 Lakini sisi tunatokana na Mungu. Kwa hiyo watu wanaomjua Mungu hutusikia sisi. Lakini watu wasiotokana na Mungu hawatusikii sisi. Hivi ndivyo tunavyiojua Roho iliyo ya kweli na ile iliyo ya uongo.
Yesu Aanza Kazi yake Galilaya
(Mt 4:12-17; Mk 1:14-15)
14 Yesu alirudi Galilaya akiwa na nguvu za Roho Mtakatifu. Habari zake zilisambaa katika eneo lote lililozunguka Galilaya. 15 Alianza kufundisha katika masinagogi na kila mtu alimsifu.
Yesu Aenda Kwenye Mji wa Kwao
(Mt 13:53-58; Mk 6:1-6)
16 Yesu alisafiri akaenda katika mji aliokulia wa Nazareti. Siku ya Sabato alikwenda kwenye sinagogi kama alivyokuwa akifanya. Alisimama ili asome. 17 Akapewa gombo la nabii Isaya. Akalivingirisha kulifungua na akapata mahali palipoandikwa haya:
18 “Roho wa Bwana yu juu yangu,
amenichagua ili
niwahubiri maskini habari njema.
Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao
na kuwaambia wasiyeona
kuwa wanaweza kuona tena.
Amenituma kuwapa uhuru wale wanaoteswa
19 na kutangaza kuwa wakati wa Bwana
kuonesha wema wake umefika.”(A)
20 Yesu akalivingirisha gombo akalifunga, akalirudisha kwa msaidizi na kuketi chini. Kwa kuwa kila mtu ndani ya sinagogi alimwangalia kwa makini, 21 Alianza kuzungumza nao. Akasema, “Maandiko haya yametimilika mlipokuwa mnanisikia nikiyasoma!”
22 Kila mtu pale akasema alipenda namna ambavyo Yesu alizungumza. Walishangaa kumsikia akisema maneno haya ya ajabu. Wakaulizana, “Inawezekanaje? Huyu si mwana wa Yusufu?”
23 Yesu akawaambia, “Ninafahamu mtaniambia mithali hii ya zamani: ‘Daktari, jitibu mwenyewe.’ Mnataka kusema ‘Tulisikia mambo yote uliyotenda Kapernaumu. Yatende pia hapa katika mji wako mwenyewe!’” 24 Lakini Yesu akasema, “Ukweli ni huu, nabii hakubaliki katika mji wa kwao.
25-26 Wakati wa Eliya mvua haikunyesha katika Israeli kwa miaka mitatu na nusu. Chakula hakikuwepo mahali popote katika nchi yote. Palikuwa wajane wengi katika Israeli wakati huo. Lakini Eliya hakutumwa kwenda kwa mmoja wa wajane waliokuwa katika Israeli bali kwa mjane aliyekuwa katika mji wa Sarepta, jirani na Sidoni.
27 Na, palikuwa wenye ugonjwa mbaya wa ngozi wengi walioishi katika Israeli wakati wa nabii Elisha, lakini hakuna aliyeponywa isipokuwa Naamani, aliyetoka katika nchi ya Shamu, siyo Israeli.”
28 Watu wote waliposikia hili, walikasirika sana. 29 Wakasimama na kumlazimisha Yesu atoke nje ya mji. Mji wao ulijengwa juu ya kilima. Wakamchukua Yesu mpaka ukingo wa kilima ili wamtupe. 30 Lakini alipita katikati yao na kwenda zake.
© 2017 Bible League International