Book of Common Prayer
4 Na bado tunayo ahadi ambayo Mungu aliwapa watu wake. Ahadi hiyo ni kwamba tuweze kuingia katika sehemu ya pumziko. Hivyo tunapaswa kuwa waangalifu ili asiwepo atakayeikosa ahadi hiyo. 2 Ndiyo, habari njema kuhusu hilo zilielezwa kwetu kama ilivyokuwa kwao. Lakini ujumbe waliousikia haukuwasaidia. Waliusikia lakini hawakuupokea kwa imani. 3 Ni sisi tu tunaoamini tunaoweza kuingia katika sehemu ya pumziko ya Mungu. Kama Mungu alivyosema:
“Nilikasirika na nikaweka ahadi:
‘Hawataingia kamwe kwenye sehemu yangu ya pumziko.’”(A)
Lakini kazi ya Mungu ilikamilika tangu wakati ule alipoumba ulimwengu. 4 Ndiyo, mahali fulani katika Maandiko alizungumza juu ya siku ya saba ya juma. Alisema, “Hivyo katika siku ya saba, Mungu alipumzika kazi zake zote.”(B) 5 Lakini katika Maandiko ya hapo juu Mungu alisema, “Hawataingia kamwe katika sehemu yangu ya pumziko.”
6 Hivyo fursa bado ipo kwa baadhi kuingia na kufurahia pumziko la Mungu. Lakini waliosikia kwanza habari njema juu yake hawakuweza kuingia, kwa sababu hawakutii. 7 Hivyo Mungu akapanga siku nyingine maalumu. Inaitwa “leo.” Alizungumza juu ya siku hiyo kupitia kwa Daudi siku nyingi zilizopita kutumia maneno tuliyonukuu mwanzoni:
“Kama leo mtaisikia sauti ya Mungu,
msiifanye migumu mioyo yenu.”(C)
8 Tunajua kuwa Yoshua hakuwaongoza watu hadi sehemu ya pumziko ambayo Mungu aliwaahidi. Tunalijua hili kwa sababu Mungu alisema baadaye kuhusu siku ya pumziko. 9 Hii inaonesha kuwa pumziko la siku ya saba[a] kwa watu wa Mungu bado linakuja. 10 Mungu alipumzika alipokamilisha kazi yake. Hivyo kila mmoja anayeingia katika sehemu ya pumziko ya Mungu vilevile atapata pumziko kutoka katika kazi yake kama Mungu alivyofanya. 11 Hivyo hebu na tujitahidi tuwezavyo kuingia katika sehemu ya pumziko ya Mungu. Tunapaswa kujitahidi ili asiwepo miongoni mwetu atakayepotea kwa kufuata mfano wa wale waliokataa kumtii Mungu.
12 Neno la Mungu[b] liko hai na linatenda kazi. Lina ukali kupita upanga ulio na makali sana na hukata hadi ndani yetu. Hukata ndani hadi sehemu ambayo nafsi na roho huwa zimeunganishwa pamoja. Neno la Mungu hukata hadi katikati ya maungio na mifupa yetu. Linahukumu mawazo na hisia ndani ya mioyo yetu. 13 Hakuna chochote ulimwenguni mwote kinachoweza kufichika mbele za Mungu. Anaweza kuviona vitu vyote kwa uwazi kabisa. Kila kitu kiko wazi mbele zake. Na kwake tutapaswa kujieleza jinsi tulivyoishi.
Yesu Kristo Ndiye Kuhani Wetu Mkuu
14 Tunaye kuhani mkuu sana ambaye ameenda kuishi na Mungu kule mbinguni. Yeye ni Yesu Mwana wa Mungu. Hivyo tuendelee kuitamka imani yetu katika yeye. 15 Yesu, kuhani wetu mkuu, anaweza kuuelewa udhaifu wetu. Yesu alipoishi duniani, alijaribiwa katika kila njia. Alijaribiwa kwa njia hizo hizo tunazojaribiwa, lakini hakutenda dhambi. 16 Tukiwa na Yesu kama kuhani wetu mkuu, tunaweza kujisikia huru kuja mbele za kiti cha enzi cha Mungu ambako kuna neema. Hapo tunapata rehema na neema ya kutusaidia tunapokuwa tunahitaji.
Uzima Katika Roho
8 Hivyo mtu yeyote aliye wa Kristo Yesu hana hukumu ya kifo. 2 Hiyo ni kwa sababu kwa njia ya Kristo Yesu sheria ya Roho inayoleta uzima imewaweka ninyi[a] huru kutoka katika sheria inayoleta dhambi na kifo. 3 Ndiyo, sheria haikuwa na nguvu ya kutusaidia kwa sababu ya udhaifu wetu wa kibinadamu. Lakini Mungu akafanya kile ambacho sheria haikuweza kufanya: Alimtuma Mwanaye duniani akiwa na mwili ule ule tunaoutumia kutenda dhambi. Mungu alimtuma ili awe njia ya kuiacha dhambi. Alitumia maisha ya mwanadamu ili kuipa dhambi hukumu ya kifo. 4 Mungu alifanya hivi ili tuweze kuishi kama sheria inavyotaka. Sasa tunaweza kuishi hivyo kwa kumfuata Roho na si kwa jinsi ya udhaifu wa kibinadamu.
5 Watu wanaoishi kwa kufuata udhaifu wa kibinadamu[b] huyafikiri yale wanayoyataka tu. Lakini wale wanaoishi kwa kumfuata Roho huyafikiri yale Roho anayotaka wafanye. 6 Ikiwa fikra zenu zinaongozwa na udhaifu wa kibinadamu, kuna kifo cha kiroho. Lakini ikiwa fikra zenu zinaongozwa na Roho, kuna uhai na amani. 7 Je, hili ni kweli? Kwa sababu kila mtu ambaye fikra zake zinaongozwa na udhaifu wa kibinadamu yuko kinyume na Mungu maana hukataa kuitii sheria ya Mungu. Na kwa hakika hawawezi kutii. 8 Wale wanaotawaliwa na udhaifu wa kibinadamu hawawezi kumpendeza Mungu.
9 Lakini ninyi hamtawaliwi na udhaifu wenu wa kibinadamu, bali mnatawaliwa na Roho, ikiwa Roho huyo wa Mungu anakaa ndani yenu. Na mtu yeyote asiye na Roho wa Kristo, huyo si wa Kristo. 10 Miili yenu inaelekea kifo kwa sababu ya dhambi. Lakini ikiwa Kristo anaishi ndani yenu, basi Roho anawapa uzima kwa sababu ya uaminifu wa wema wa Mungu.[c] 11 Mungu alimfufua Yesu kutoka kwa wafu. Na ikiwa Roho wa Mungu anaishi ndani yenu, ataifanya hai tena miili yenu inayokufa. Ndiyo, Mungu ndiye aliyemfufua Kristo kutoka kwa wafu, naye atawafufua ninyi na kuwapa uzima kupitia Roho wake anayeishi ndani yenu.
© 2017 Bible League International