Revised Common Lectionary (Semicontinuous)
68 “Asifiwe Bwana, Mungu wa Israeli,
kwa kuwa amekuja kuwasaidia
watu wake na kuwaweka huru.
69 Na ametuletea sisi Mwokozi Mwenye Nguvu,
kutoka katika ukoo wa mtumishi wake Daudi.
70 Hivi ndivyo alivyoahidi
kupitia manabii wake watakatifu tangu zamani.
71 Aliahidi kwa Agano kuwa atatuokoa na adui zetu
na milki za wote wanaotuchukia.
72 Ili kuonesha rehema kwa baba zetu,
na kulikumbuka agano lake takatifu aliloagana nao.
73 Agano hili ni kiapo alichomwapia
baba yetu Ibrahimu.
74 Alipoahidi kutuokoa kutoka katika nguvu za adui zetu,
ili tuweze kumwabudu Yeye bila hofu.
75 Katika namna iliyo takatifu na yenye haki
mbele zake siku zote za maisha yetu.
76 Sasa wewe, mtoto mdogo,
utaitwa nabii wa Mungu Aliye Juu Sana,
kwa sababu utamtangulia Bwana
kuandaa njia yake.
77 Utawaambia watu wake kwamba wataokolewa
kwa kusamehewa dhambi zao.
78 Kwa rehema ya upendo wa Mungu wetu,
siku mpya[a] itachomoza juu yetu kutoka mbinguni.
79 Kuwaangazia wale wanaoishi katika giza,
kwa hofu ya mauti,
na kuongoza hatua zetu
katika njia ya amani.”
Yesu Awatuma Kazi Mitume Wake
(Mt 10:5-15; Mk 6:7-13)
9 Yesu aliwaita mitume wake kumi na wawili pamoja, akawapa nguvu kuponya magonjwa na kutoa pepo kwa watu. 2 Akawatuma kwenda kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na kuponya wagonjwa. 3 Akawaambia, “Mnaposafiri, msibebe kitu chochote: msichukue fimbo ya kutembelea, msibebe mkoba, chakula au fedha. Chukueni nguo mlizovaa tu kwa ajili ya safari yenu. 4 Mkiingia katika nyumba; kaeni katika nyumba hiyo mpaka mtakapokuwa mnatoka katika mji huo. 5 Ikiwa watu katika mji mtakaoingia hawatawakaribisha, nendeni nje ya mji na kuyakung'uta mavumbi miguuni mwenu kama onyo kwao.”
6 Hivyo mitume wakaondoka. Walisafiri katika miji yote. Walihubiri Habari Njema na kuponya wagonjwa kila mahali.
© 2017 Bible League International