Old/New Testament
Yesu Ajaribiwa na Shetani
(Mt 4:1-11; Mk 1:12-13)
4 Akiwa amejaa Roho Mtakatifu, Yesu akarudi kutoka Mto Yordani. Kisha Roho Mtakatifu akamwongoza mpaka nyikani 2 kwa muda wa siku arobaini, alikojaribiwa na Ibilisi. Katika muda wote huo hakula chakula chochote na baadaye akahisi njaa sana.
3 Ibilisi akamwambia, “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate.”
4 Yesu akamjibu, “Maandiko yanasema, ‘Watu hawataishi kwa mkate tu.’”(A)
5 Kisha mwovu akamchukua Yesu na kwa muda mfupi akamwonyesha falme zote za ulimwengu. 6 Mwovu akamwambia, “Nitakufanya uwe mfalme wa sehemu zote hizi. Utakuwa na mamlaka juu yao, na utapata utukufu wote. Yote yametolewa kwangu. Ninaweza kumpa yeyote kadri ninavyopenda. 7 Nitakupa vyote hivi, ikiwa utaniabudu tu.”
8 Yesu akajibu, “Maandiko yanasema, ‘Ni lazima umwabudu Bwana Mungu wako, na umtumikie yeye peke yake.’”(B)
9 Ndipo Shetani akamwongoza Yesu mpaka Yerusalemu na kumweka mahali palipo juu katika mnara wa Hekalu. Akamwambia, “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, jirushe! 10 Kwani Maandiko yanasema,
‘Mungu atawaamuru
malaika zake wakulinde.’(C)
11 Pia imeandikwa kuwa,
‘Mikono yao itakudaka,
ili usijikwae mguu wako kwenye mwamba.’”(D)
12 Yesu akajibu, “Pia, Maandiko yanasema: ‘Usimjaribu Bwana Mungu wako.’”(E)
13 Shetani alipomaliza kumjaribu Yesu katika namna zote, alimwacha akaenda zake hadi wakati mwingine.
Yesu Aanza Kazi yake Galilaya
(Mt 4:12-17; Mk 1:14-15)
14 Yesu alirudi Galilaya akiwa na nguvu za Roho Mtakatifu. Habari zake zilisambaa katika eneo lote lililozunguka Galilaya. 15 Alianza kufundisha katika masinagogi na kila mtu alimsifu.
Yesu Aenda Kwenye Mji wa Kwao
(Mt 13:53-58; Mk 6:1-6)
16 Yesu alisafiri akaenda katika mji aliokulia wa Nazareti. Siku ya Sabato alikwenda kwenye sinagogi kama alivyokuwa akifanya. Alisimama ili asome. 17 Akapewa gombo la nabii Isaya. Akalivingirisha kulifungua na akapata mahali palipoandikwa haya:
18 “Roho wa Bwana yu juu yangu,
amenichagua ili
niwahubiri maskini habari njema.
Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao
na kuwaambia wasiyeona
kuwa wanaweza kuona tena.
Amenituma kuwapa uhuru wale wanaoteswa
19 na kutangaza kuwa wakati wa Bwana
kuonesha wema wake umefika.”(F)
20 Yesu akalivingirisha gombo akalifunga, akalirudisha kwa msaidizi na kuketi chini. Kwa kuwa kila mtu ndani ya sinagogi alimwangalia kwa makini, 21 Alianza kuzungumza nao. Akasema, “Maandiko haya yametimilika mlipokuwa mnanisikia nikiyasoma!”
22 Kila mtu pale akasema alipenda namna ambavyo Yesu alizungumza. Walishangaa kumsikia akisema maneno haya ya ajabu. Wakaulizana, “Inawezekanaje? Huyu si mwana wa Yusufu?”
23 Yesu akawaambia, “Ninafahamu mtaniambia mithali hii ya zamani: ‘Daktari, jitibu mwenyewe.’ Mnataka kusema ‘Tulisikia mambo yote uliyotenda Kapernaumu. Yatende pia hapa katika mji wako mwenyewe!’” 24 Lakini Yesu akasema, “Ukweli ni huu, nabii hakubaliki katika mji wa kwao.
25-26 Wakati wa Eliya mvua haikunyesha katika Israeli kwa miaka mitatu na nusu. Chakula hakikuwepo mahali popote katika nchi yote. Palikuwa wajane wengi katika Israeli wakati huo. Lakini Eliya hakutumwa kwenda kwa mmoja wa wajane waliokuwa katika Israeli bali kwa mjane aliyekuwa katika mji wa Sarepta, jirani na Sidoni.
27 Na, palikuwa wenye ugonjwa mbaya wa ngozi wengi walioishi katika Israeli wakati wa nabii Elisha, lakini hakuna aliyeponywa isipokuwa Naamani, aliyetoka katika nchi ya Shamu, siyo Israeli.”
28 Watu wote waliposikia hili, walikasirika sana. 29 Wakasimama na kumlazimisha Yesu atoke nje ya mji. Mji wao ulijengwa juu ya kilima. Wakamchukua Yesu mpaka ukingo wa kilima ili wamtupe. 30 Lakini alipita katikati yao na kwenda zake.
© 2017 Bible League International