Book of Common Prayer
Joka na Mwanamke Anayezaa
12 Jambo la ajabu lilionekana mbinguni: Mwanamke aliyevalishwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu yake alionekana. Alikuwa na taji yenye nyota kumi na mbili kichwani pake. 2 Alikuwa na mimba na alilia kwa uchungu kwa sababu alikuwa karibu ya kuzaa.
3 Kisha ajabu nyingine ikaonekana mbinguni: Alikuweko huko joka mkubwa mwekundu. Joka huyo alikuwa na vichwa saba na alikuwa na taji juu ya kila kichwa. Na alikuwa na pembe kumi. 4 Mkia wake ulizoa theluthi ya nyota na kuziangusha duniani. Joka hili lilisimama mbele ya mwanamke aliyekuwa karibu ya kuzaa mtoto. Lilitaka kumla mtoto mara atakapozaliwa.
5 Mwanamke alimzaa mtoto wa kiume, atakayewatawala mataifa yote kwa fimbo yake ya chuma. Na mwana wa mwanamke huyu alichukuliwa juu mbinguni kwa Mungu, kwenye kiti chake cha enzii. 6 Mwanamke alikimbilia jangwani mpaka mahali ambako Mungu amemwandalia. Huko angetunzwa kwa siku 1,260.
7 Kisha kulikuwa vita mbinguni. Mikaeli[a] na malaika zake walipigana na joka. Nalo joka na malaika zake wakapigana na Mikaeli pamoja na malaika zake, 8 lakini joka na malaika zake hawakuwa na nguvu za kutosha kushinda, na hivyo wakapoteza nafasi zao mbinguni. 9 Likatupwa chini kutoka mbinguni. (Joka hili kubwa ni nyoka yule wa zamani, aitwaye Ibilisi au Shetani, anayeudanganya ulimwengu wote.) Joka na malaika zake walitupwa duniani.
10 Kisha nilisikia sauti kubwa mbinguni ikisema:
“Ushindi na uweza na ufalme wa Mungu wetu
na mamlaka ya Masihi wake umekuja sasa,
kwa sababu mshitaki wa kaka na dada zetu
ametupwa chini.
Ndiye aliyewashitaki kwa Mungu,
mchana na usiku.
11 Walimshinda kwa sadaka ya damu ya Mwanakondoo
na kwa ujumbe wa Mungu waliowaambia watu.
Hawakuyapenda maisha yao sana.
Hawakuogopa kifo.
12 Hivyo furahi, ewe mbingu
na wote waishio humo!
Lakini ole kwa nchi na bahari,
kwa sababu Ibilisi ameshuka kwako.
Amejaa ghadhabu.
Anajua ana muda mchache.”
Yesu Aenda Kwenye Mji wa Kwao
(Mk 6:1-6; Lk 4:16-30)
53 Yesu alipomaliza kufundisha kwa simulizi hizi, aliondoka pale. 54 Alikwenda katika mji wa kwao. Aliwafundisha watu katika sinagogi lao, nao walishangaa. Walisema, “Mtu huyu alipata wapi hekima na nguvu hii ya kutenda miujiza? 55 Je, yeye si mwana wa seremala tunayemfahamu? Je, jina la mamaye si Mariamu na wadogo zake ni Yakobo, Yusufu, Simoni na Yuda? 56 Na dada zake bado wanaishi hapa katika mji huu? Anawezaje kutenda mambo haya?” 57 Hivyo wakawa na mashaka kumpokea.
Lakini Yesu akawaambia, “Watu kila mahali huwaheshimu manabii, lakini katika mji wake au katika nyumba yake nabii hapati heshima yoyote.” 58 Yesu hakufanya miujiza mingi huko, kwa sababu watu hawakumwamini.
© 2017 Bible League International