Chronological
Simulizi Kuhusu Mkulima Aliyepanda Mbegu
(Mk 4:1-9; Lk 8:4-8)
13 Siku hiyo hiyo Yesu alitoka nje ya nyumba na kukaa kando ya ziwa. 2 Kundi kubwa wakakusanyika kumzunguka. Hivyo akapanda mtumbwini na kuketi. Watu wote wakabaki ufukweni. 3 Kisha Yesu akatumia simulizi kuwafundisha mambo mengi. Akawaambia simulizi hii:
“Mkulima alitoka kwenda kupanda mbegu. 4 Alipokuwa anatawanya mbegu, baadhi ziliangukia njiani. Ndege wakaja na kuzila zote. 5 Mbegu zingine ziliangukia kwenye ardhi yenye mawe, ambako hakukuwa na udongo wa kutosha. Zikakua haraka pale, kwa sababu udongo haukuwa na kina. 6 Lakini jua lilipowaka, likaichoma mimea. Mimea ikafa kwa sababu haikuwa na mizizi mirefu. 7 Baadhi ya mbegu ziliangukia katikati ya miiba. Miiba ikakua na kusababisha mimea mizuri kuacha kukua. 8 Lakini baadhi ya mbegu ziliangukia kwenye udongo wenye rutuba. Hapo zikakua na kuzaa nafaka. Baadhi ya mimea ikazaa nafaka mara mia zaidi, baadhi mara sitini na baadhi mara thelathini zaidi. 9 Ninyi watu mnaoweza kunisikia, nisikilizeni!”
Kwa nini Yesu Alitumia Simulizi Kufundisha
(Mk 4:10-12; Lk 8:9-10)
10 Wafuasi wake wakamwendea Yesu na kumuuliza, “Kwa nini unatumia simulizi hizi kuwafundisha watu?”
11 Yesu akawajibu, “Mungu amewapa ninyi ujuzi wa kuelewa siri za ufalme wa Mungu, lakini hajawapa watu hawa wengine ujuzi huu. 12 Kisha akawaambia, ‘Zingatieni kwa makini kile mnachokisikia. Kwani jinsi mnavyosikiliza kwa makini, ndivyo mtakavyoelewa na kuzidi kuelewa. Kwa kuwa kila aliye na uelewa kidogo ataongezewa zaidi. Lakini wale wasiosikiliza kwa makini watapoteza hata ule uelewa mdogo walio nao.’ 13 Ndiyo sababu ninatumia simulizi hizi kuwafundisha watu: Wanaona, lakini hakika hawaoni. Wanasikia, lakini hakika hawasikii au kuelewa. 14 Hiyo inathibitisha alichosema nabii Isaya kuhusu wao kuwa kweli:
‘Ninyi watu mtasikia na kusikia,
lakini hamtaelewa.
Mtatazama na kutazama,
lakini hakika hamtaona.
15 Ndiyo, akili za watu hawa sasa zimefungwa.
Wana masikio, lakini hawasikii vizuri.
Wana macho, lakini wameyafumba.
Iwapo akili zao zisingekuwa zimefungwa,
wangeona kwa macho yao;
wangesikia kwa masikio yao;
Iwapo wangeelewa kwa akili zao.
Kisha wangenigeukia na kuponywa.’(A)
16 Bahati gani mliyonayo ninyi. Mnaelewa mnachokiona kwa macho yenu. Na mnaelewa mnachosikia kwa masikio yenu. 17 Ninaweza kuwathibitishia, manabii na watakatifu wengi walitaka kuona mnayoyaona. Lakini hawakuyaona. Walitaka kusikia mnayosikia sasa. Lakini hawakuyasikia.
Yesu Afafanua Simulizi Kuhusu Mbegu
(Mk 4:13-20; Lk 8:11-15)
18 Hivyo sikilizeni maana ya simulizi hiyo kuhusu mkulima:
19 Vipi kuhusu mbegu zilizoangukia njiani? Hizo zinafanana na watu wanaosikia mafundisho kuhusu ufalme wa Mungu lakini hawauelewi. Mwovu huja na kuyachukua yaliyopandwa katika mioyo yao.
20 Na vipi kuhusu mbegu zilizoangukia kwenye udongo wenye mawe? Hizo zinafanana na watu wanaosikia mafundisho haraka na kwa furaha huyapokea. 21 Lakini hawaruhusu mafundisho kutawala maisha yao. Huyatunza kwa muda mfupi. Mara tatizo au mateso yanapokuja kwa sababu ya mafundisho waliyoyapokea, wanaacha kuyafuata.
22 Na vipi kuhusu mbegu zilizoanguka katikati ya miiba? Hizo zinafanana na watu wanaosikia mafundisho lakini huyaruhusu mahangaiko ya maisha na kutaka utajiri, hufanya mafundisho yasikue. Hivyo mafundisho hayazai mazao mazuri katika maisha yao.
23 Lakini vipi kuhusu mbegu zilizoanguka kwenye udongo wenye rutuba? Hizo ni sawa na watu wanaosikia mafundisho na kuyaelewa. Hukua na kuzaa mazao mazuri, wakati mwingine mara mia, wakati mwingine mara sitini, na wakati mwingine mara thelathini zaidi.”
Simulizi Kuhusu Ngano na Magugu
24 Kisha Yesu akatumia simulizi nyingine kuwafundisha. Yesu akasema, “Ufalme wa Mungu unafanana na mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. 25 Usiku ule, kila mtu alipokuwa amelala, adui wa yule mtu akaja na kupanda magugu katikati ya ngano kisha akaondoka. 26 Baadaye, ngano ikakua na vichwa vya nafaka vikaota juu ya mimea. Kisha mtumishi akayaona magugu. 27 Watumwa wa mwenye shamba wakaja na akasema, ‘Bwana ulipanda mimea mizuri kwenye shamba lako. Magugu yametoka wapi?’
28 Yule mtu akajibu, ‘Adui alipanda magugu.’
Wale watumwa wakauliza, ‘Je, unataka twende na kung'oa magugu?’
29 Akajibu, ‘Hapana, kwa sababu mtakapokuwa mnang'oa magugu, mtaweza pia kung'oa ngano. 30 Yaacheni magugu na ngano vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati wa mavuno nitawaambia wafanyakazi hivi: Kwanza, yakusanyeni magugu na kuyafunga pamoja ili myachome. Kisha kusanyeni ngano na kuileta ghalani mwangu.’”
Simulizi Nyingine ya Ufalme
(Mk 4:30-34; Lk 13:18-21)
31 Kisha Yesu akawaambia watu simulizi nyingine: “Ufalme wa Mungu unafanana na mbegu ya mharadali ambayo mtu alipanda katika shamba lake. 32 Ni mbegu ndogo sana kuliko mbegu zote. Lakini unapokua, ni kubwa kuliko mimea yote ya bustanini. Unakuwa mti mkubwa unaotosha ndege kuja na kutengeneza viota kwenye matawi yake.”
33 Kisha Yesu akawaambia simulizi nyingine: “Ufalme wa Mungu unafanana na chachu ambayo mwanamke huichanganya katika bakuli kubwa la unga ili atengeneze mkate. Chachu hufanya kinyunya chote kiumuke.”
34 Yesu alitumia simulizi akasema mambo yote haya kwa watu. Daima alitumia simulizi kuwafundisha. 35 Hii ilikuwa kuweka wazi maana halisi kama manabii walivyosema:
“Nitazungumza kwa kutumia simulizi;
Nitayasema mambo ambayo yamekuwa siri
tangu ulimwengu ulipoumbwa.”(B)
Yesu Afafanua Simulizi Kuhusu Magugu
36 Kisha Yesu akawaacha watu na kuingia katika nyumba. Wafuasi wake wakamwendea na akasema, “Tufafanulie maana ya simulizi kuhusu magugu ndani ya shamba.”
37 Akajibu, “Mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba ni Mwana wa Adamu. 38 Shamba ni ulimwengu. Mbegu nzuri ni watoto katika ufalme wa Mungu. Magugu ni watu wa Yule Mwovu. 39 Na adui aliyepanda mbegu mbaya ni ibilisi. Mwisho wa nyakati ndiyo wakati wa mavuno. Wafanyakazi wanaokusanya ni malaika wa Mungu.
40 Magugu hung'olewa na kuchomwa motoni. Itakuwa vivyo hivyo nyakati za mwisho. 41 Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watawatafuta watu wanaosababisha dhambi na wale wote watendao maovu. Malaika watawatoa watu hao katika ufalme wa Mungu. 42 Watawatupia katika tanuru la moto. Huko watu watakuwa wakilia na kusaga meno kwa maumivu. 43 Kisha wenye haki watang'aa kama jua. Watakuwa katika ufalme wa baba yao. Ninyi watu, mlio na masikio, sikilizeni!
Simulizi Kuhusu Hazina na Lulu
44 Ufalme wa Mungu unafanana na hazina iliyofichwa shambani. Siku moja mtu alipoiona aliificha tena; na kwa sababu alikuwa na furaha sana alikwenda kuuza kila kitu alichonacho na kulinunua shamba.
45 Pia, ufalme wa Mungu unafanana na mchuuzi anayetafuta lulu safi. 46 Siku moja alipoipata, alikwenda na akauza kila kitu alichokuwa nacho ili kuinunua.
Simulizi Kuhusu Wavu wa Kuvulia Samaki
47 Pia, ufalme wa Mungu unafanana na nyavu kubwa iliyowekwa katika ziwa. Nyavu ile ikavua aina nyingi tofauti ya samaki. 48 Ikajaa, hivyo wavuvi wakaivuta mpaka pwani. Wakakaa chini na kutoa samaki wote wazuri na kuwaweka kwenye kikapu. Kisha wakawatupa samaki wabaya. 49 Itakuwa hivyo wakati wa mwisho. Malaika watakuja na kuwatenganisha waovu na watakatifu. 50 Watawatupa waovu katika tanuru la moto. Huko watu watalia na kusaga meno yao kwa sababu ya maumivu.”
51 Kisha Yesu akawauliza wafuasi wake, “Mnaelewa mambo yote haya?”
Wakasema, “Ndiyo, tunaelewa.”
52 Kisha Yesu akawaambia wafuasi wake, “Hivyo kila mwalimu wa sheria aliyejifunza kuhusu ufalme wa Mungu ana baadhi ya vitu vizuri vya kufundisha. Ni kama mmiliki wa nyumba, aliye na vitu vipya na vya zamani nyumbani mwake. Na huvitoa nje vipya na vya zamani.”
Yesu Aenda Kwenye Mji wa Kwao
(Mk 6:1-6; Lk 4:16-30)
53 Yesu alipomaliza kufundisha kwa simulizi hizi, aliondoka pale. 54 Alikwenda katika mji wa kwao. Aliwafundisha watu katika sinagogi lao, nao walishangaa. Walisema, “Mtu huyu alipata wapi hekima na nguvu hii ya kutenda miujiza? 55 Je, yeye si mwana wa seremala tunayemfahamu? Je, jina la mamaye si Mariamu na wadogo zake ni Yakobo, Yusufu, Simoni na Yuda? 56 Na dada zake bado wanaishi hapa katika mji huu? Anawezaje kutenda mambo haya?” 57 Hivyo wakawa na mashaka kumpokea.
Lakini Yesu akawaambia, “Watu kila mahali huwaheshimu manabii, lakini katika mji wake au katika nyumba yake nabii hapati heshima yoyote.” 58 Yesu hakufanya miujiza mingi huko, kwa sababu watu hawakumwamini.
Yesu Akiwa Galilaya
8 Siku iliyofuata, Yesu alisafiri kupitia katika baadhi ya miji na vijiji. Yesu aliwahubiri watu Habari Njema kuhusu ufalme wa Mungu. Mitume kumi na wawili walikuwa pamoja naye. 2 Walikuwepo pia baadhi ya wanawake ambao Yesu aliwaponya magonjwa na pepo wabaya. Mmoja wao alikuwa Mariamu aitwaye Magdalena ambaye alitokwa na pepo saba; 3 Pia pamoja na wanawake hawa alikuwepo Yoana mke wa Kuza (msimamizi wa mali za Herode), Susana, na wanawake wengine wengi. Wanawake hawa walitumia fedha zao kuwahudumia Yesu na mitume wake.
Simulizi Kuhusu Mkulima Aliyepanda Mbegu
(Mt 13:1-17; Mk 4:1-12)
4 Kundi kubwa la watu lilikusanyika. Watu walimjia Yesu kutoka katika kila mji, naye Yesu akawaambia fumbo hili:
5 “Mkulima alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akizitawanya, baadhi zilianguka kandokando ya njia. Watu wakazikanyaga, na ndege wa angani wakazila. 6 Zingine zikaanguka kwenye udongo wenye mawe. Zilipoanza kukua zikafa kwa sababu ya kukosa maji. 7 Mbegu zingine ziliangukia kwenye miiba. Miiba ikakua pamoja nazo, miiba ikazisongasonga na hazikukua. 8 Zilizosalia ziliangukia kwenye udongo mzuri wenye rutuba. Mbegu hizi zikaota na kuzaa kila moja mia.”
Yesu akamalizia fumbo. Kisha akapaza sauti, akasema, “Ninyi watu mnaonisikia, sikilizeni!”
9 Wafuasi wake wakamwuliza, “Fumbo hili linamaanisha nini?”
10 Akasema, “Mmechaguliwa kujua kweli za siri kuhusu ufalme wa Mungu. Lakini ninatumia mafumbo kuzungungumza na watu wengine. Ninafanya hivi ili,
‘Watazame,
lakini wasiweze kuona.
Wasikia,
lakini wasielewe.’(A)
Yesu Afafanua Simulizi Kuhusu Mbegu
(Mt 13:18-23; Mk 4:13-20)
11 Hii ndiyo maana ya fumbo hili: Mbegu ni Neno la Mungu. 12 Watu wengine ni kama mbegu zilizoanguka njiani. Husikia mafundisho ya Mungu, lakini Shetani huja na kuwafanya waache kuyatafakari. Hii huwafanya kutoamini na kuokoka. 13 Wengine wanafanana na mbegu zilizoanguka kwenye udongo wenye mawe. Ni watu ambao huyasikia mafundisho ya Mungu na kuyapokea kwa furaha, lakini kwa kuwa hawana mizizi yenye kina, huamini kwa muda mfupi. Majaribu yanapokuja, humwacha Mungu.
14 Zilizoanguka katika miiba, zinafanana na watu wanaoyasikia Mafundisho ya Mungu, lakini wanaruhusu wasiwasi, mali na anasa za maisha haya kuwasimamisha na hawaendelei kukua. Hivyo mafundisho hayazalishi matokeo mazuri katika maisha yao.[a] 15 Na zile zilizoangukia katika udongo mzuri, ni wale ambao huyasikia mafundisho ya Mungu kwa moyo safi na mnyoofu. Huyatii na kwa uvumilivu wao huzaa mazao mazuri.
Zingatieni Nuru
(Mk 4:21-25)
16 Hakuna mtu anayewasha taa na kuifunika kwa bakuli au kuificha uvunguni mwa kitanda. Badala yake huiweka kwenye kinara cha taa mahali palipo wazi, ili wanaoingia ndani wapate nuru ya kuwawezesha kuona. 17 Kila jambo lililofichwa litawekwa wazi na kila siri itajulikana na kila mtu ataiona. 18 Hivyo yatafakarini kwa umakini yale mnayosikia. Watu wenye uelewa kiasi watapokea zaidi. Lakini wale wasio na uelewa watapoteza hata ule wanaodhani kuwa wanao.”
Wafuasi wa Yesu ni Familia Yake Halisi
(Mt 12:46-50; Mk 3:31-35)
19 Mama yake Yesu na wadogo zake wakaenda kumwona, lakini walishindwa kumfikia kwa sababu walikuwepo watu wengi sana. 20 Mtu mmoja akamwambia Yesu, “Mama yako na wadogo zako wamesimama nje. Wanataka kukuona.”
21 Yesu akawajibu “Mama yangu na wadogo zangu ni wale wanaolisikia na kulitii Neno la Mungu.”
Yesu Atuliza Dhoruba
(Mt 8:23-27; Mk 4:35-41)
22 Siku moja Yesu na wafuasi wake walipanda mashua. Akawaambia, “Tuvuke mpaka upande mwingine wa ziwa.” Wakaanza safari kuvuka ziwa. 23 Walipokuwa wanasafiri, Yesu alisinzia. Tufani kubwa ikalikumba ziwa na mashua ikaanza kujaa maji, wakawa katika hatari. 24 Wafuasi wakamwendea, wakamwamsha, wakasema, “Mkuu, mkuu, tutazama!”
Yesu akasimama, akaukemea upepo na mawimbi ya maji. Upepo ukakoma na ziwa likatulia. 25 Ndipo Yesu akawaambia wafuasi wake, “Imani yenu iko wapi?”
Lakini wao waliogopa na kustaajabu, wakanong'onezana, “Huyu ni mtu wa namna gani? Anaamuru upepo na maji, na vinamtii?”
Yesu Amweka Huru Mtu Kutoka Pepo Wachafu
(Mt 8:28-34; Mk 5:1-20)
26 Yesu na wafuasi wake wakasafiri mpaka katika nchi walimoishi Wagerasi[b] iliyokuwa ng'ambo ya ziwa Galilaya. 27 Yesu alipotoka katika mashua, mwanaume mmoja kutoka katika mji ule alimwendea. Mtu huyu alikuwa na mapepo ndani yake. Kwa muda mrefu hakuwahi kuvaa nguo na aliishi makaburini.
28-29 Pepo aliyekuwa ndani yake alikuwa akimpagaa mara nyingi na alikuwa akifungwa gerezani, mikono na miguu yake ikiwa imefungwa kwa minyororo. Lakini kila mara aliivunja. Pepo ndani yake alikuwa anamlazimisha kwenda nje ya mji mahali pasipoishi watu. Yesu alimwamuru kumtoka mtu yule. Alipomwona Yesu, alianguka mbele yake huku akipiga kelele kwa sauti, “Unataka nini kwangu, Yesu, Mwana wa Mungu Mkuu Aliye Juu? Tafadhali usiniadhibu!”
30 Yesu akamwuliza, “Jina lako nani?”
Mtu yule akajibu, “Jeshi.”[c] (Alisema jina lake ni “Jeshi” kwa sababu pepo wengi walikuwa wamemwingia.) 31 Pepo wale wakamsihi Yesu asiwaamuru kwenda shimoni.[d] 32 Katika kilima kile, kulikuwa kundi kubwa la nguruwe wakichungwa. Pepo wakamsihi Yesu awaruhusu wawaingie wale nguruwe. Hivyo Yesu akawaruhusu. 33 Pepo wakamtoka yule mtu, na kuwaingia nguruwe. Kundi lote la wale nguruwe likakimbia kutelemkia ziwani kwa kasi, nguruwe wakazama na kufia humo.
34 Wachungaji wa nguruwe walipoona lililotokea, walikimbia, wakaenda kutoa taarifa mjini na mashambani. 35 Watu wakaenda kuona lililotokea. Walipofika alipokuwa Yesu wakamwona mtu yule aliyetokwa na pepo ameketi karibu na Yesu, amevaa nguo, akiwa na akili zake timamu; pepo walikuwa wamemtoka. Jambo hili likawaogopesha watu. 36 Wale walioona mambo haya yalivyotokea waliwaambia wengine namna Yesu alivyomponya yule mtu. 37 Watu wote waliokuwa wakiishi eneo lote la Gerasi wakamtaka Yesu aondoke kwa sababu waliogopa.
Hivyo Yesu akapanda mashua na kurudi Galilaya. 38 Mtu aliyeponywa alimsihi amfuate Yesu. Lakini Yesu akamtuma, akamwambia, 39 “Rudi nyumbani, ukawaeleze watu mambo ambayo Mungu amekutendea.”
Hivyo mtu yule alikwenda sehemu zote za mji akieleza mambo ambayo Yesu amemtendea.
Yesu Anampa Uhai Msichana Aliyekufa na Kumponya Mwanamke Mgonjwa
(Mt 9:18-26; Mk 5:21-43)
40 Yesu aliporudi Galilaya, watu walimkaribisha. Kila mtu alikuwa anamsubiri. 41-42 Mtu mmoja jina lake Yairo, aliyekuwa mkuu wa sinagogi alimwendea. Alikuwa na binti mmoja tu mwenye umri wa miaka kumi na mbili na alikuwa mgonjwa sana katika hali ya kufa. Hivyo Yairo alisujudu miguuni pa Yesu na akamsihi aende nyumbani kwake.
Yesu alipokuwa akienda nyumbani kwa Yairo, watu walimzonga kila upande. 43 Mwanamke aliyekuwa akitokwa damu kwa miaka kumi na mbili alikuwepo katika umati huo. Alikuwa ametumia mali zake zote kwa madaktari,[e] lakini hakuna daktari aliyeweza kumponya. 44 Alikwenda nyuma ya Yesu na kugusa pembe ya vazi lake. Wakati huo huo damu ikaacha kumtoka. 45 Ndipo Yesu akasema, “Nani amenigusa?”
Kila mtu alikataa kuwa hajamgusa, Petro akasema, “Mkuu, watu wamekuzunguka na wanakuzongazonga kila upande.”
46 Lakini Yesu akasema, “Kuna mtu amenigusa. Nimesikia nguvu ikinitoka.” 47 Yule mwanamke alipoona ya kwamba hataweza kujificha akajitokeza akitetemeka. Akasujudu mbele ya Yesu. Huku kila mmoja akisikia, akaeleza sababu iliyomfanya amguse, na kwamba alipona wakati ule ule alipomgusa. 48 Yesu alimwambia, “Binti yangu umeponywa kwa sababu uliamini. Nenda kwa amani.”
49 Yesu alipokuwa bado anaongea, mtu mmoja kutoka nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi alikuja na akasema, “Binti yako amekwisha kufa! Hakuna haja ya kuendelea kumsumbua Mwalimu.”
50 Yesu aliposikia maneno hayo, alimwambia Yairo, “Usiogope! Amini tu na binti yako ataponywa.”
51 Yesu akaenda nyumbani, alipofika akaruhusu Petro, Yohana, Yakobo pamoja na baba na mama wa yule mtoto tu kuingia ndani pamoja naye. 52 Kila mtu alikuwa akilia na kusikia huzuni kwa sababu msichana alikuwa amekufa. Lakini Yesu akasema, “Msilie. Hajafa. Amelala usingizi tu.”
53 Watu wakamcheka, kwa sababu walijua kuwa amekwisha kufa. 54 Lakini Yesu akamshika mkono na kumwambia, “Mtoto inuka!” 55 Roho yake ikamrudia, akasimama hapo hapo. Yesu akasema, “Mpeni chakula.” 56 Wazazi wa yule binti wakashangaa. Yesu akawakataza wasimwambie mtu yeyote lililotokea.
© 2017 Bible League International