Chronological
Ukoo wa Yesu
(Lk 3:23-38)
1 Hii ni historia ya ukoo wa Yesu, Masihi.[a] Alitoka katika ukoo wa Daudi, aliyetoka katika ukoo wa Ibrahimu.
2 Ibrahimu alikuwa baba yake Isaka.
Isaka alikuwa baba yake Yakobo.
Yakobo alikuwa baba wa Yuda na ndugu zake.
3 Yuda alikuwa baba wa Peresi na Zera. (Mama yao alikuwa Tamari.)
Peresi alikuwa baba yake Hezroni.
Hezroni alikuwa baba yake Ramu.
4 Ramu alikuwa baba yake Aminadabu.
Aminadabu alikuwa baba yake Nashoni.
Nashoni alikuwa baba yake Salmoni.
5 Salmoni alikuwa baba yake Boazi. (Mama yake Boazi alikuwa Rahabu.)
Boazi alikuwa baba yake Obedi. (Mama yake Obedi alikuwa Ruthu.)
Obedi alikuwa baba yake Yese.
6 Yese alikuwa baba yake Mfalme Daudi.
Daudi alikuwa baba yake Sulemani. (Mama yake Sulemani alikuwa mke wa Uria.)
7 Sulemani alikuwa baba yake Rehoboamu.
Rehoboamu alikuwa baba yake Abiya.
Abiya alikuwa baba yake Asa.
8 Asa alikuwa baba yake Yehoshafati.
Yehoshafati alikuwa baba yake Yoramu.
Yoramu alikuwa baba yake Uzia.
9 Uzia alikuwa baba yake Yothamu.
Yothamu alikuwa baba yake Ahazi.
Ahazi alikuwa baba yake Hezekia.
10 Hezekia alikuwa baba yake Manase.
Manase alikuwa baba yake Amoni.
Amoni alikuwa baba yake Yosia.
11 Yosia alikuwa baba wa Yekonia[b] na ndugu zake.
Walioishi wakati ambao watu walipelekwa utumwani Babeli.
12 Baada ya uhamisho wa Babeli,
Yekonia akawa baba yake Shealtieli.
Shealtieli alikuwa babu wa Zerubabeli.
13 Zerubabeli alikuwa baba yake Abiudi.
Abiudi alikuwa baba yake Eliakimu.
Eliakimu alikuwa baba yake Azori.
14 Azori alikuwa baba yake Sadoki.
Sadoki alikuwa baba yake Akimu.
Akimu alikuwa baba yake Eliudi.
15 Eliudi alikuwa baba yake Eliazari.
Eliazari alikuwa baba yake Matani.
Matani alikuwa baba yake Yakobo.
16 Yakobo alikuwa baba yake Yusufu,
Yusufu alikuwa mume wa Mariamu.
Na Mariamu alimzaa Yesu, anayeitwa Masihi.
17 Kulikuwa na vizazi kumi na nne kuanzia kwa Ibrahimu mpaka kwa Daudi. Na kulikuwa na vizazi kumi na nne kuanzia kwa Daudi mpaka wakati wa uhamisho wa Babeli. Na palikuwa na vizazi kumi na nne tangu uhamisho wa Babeli mpaka wakati alipozaliwa Yesu, Masihi.
Kuzaliwa kwa Yesu, Masihi
(Lk 2:1-7)
18 Kuzaliwa kwa Yesu Masihi, kulikuwa hivi: Mariamu mama yake alikuwa amechumbiwa na Yusufu. Kabla hawajaoana, Yusufu aligundua kuwa Mariamu alikuwa mja mzito. (Yeye alipata mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu.) 19 Kwa kuwa Yusufu alitaka kufanya kile kilichokuwa, alikusudia kumwacha Mariamu kwa siri bila ya kumvunjia heshima.
20 Lakini baada ya Yusufu kuliwazia jambo hili, Malaika wa Bwana alimjia katika ndoto na akamwambia, “Yusufu mwana wa Daudi, usiogope kumchukua Mariamu awe mke wako. Mimba aliyonayo ameipata kwa uweza wa Roho Mtakatifu. 21 Atamzaa mwana, nawe utamwita Yesu.[c] Utampa jina hilo Yesu kwa sababu yeye atawaokoa watu wake kutoka dhambi zao.”
22 Haya yote yalitokea ili kutimiza maneno ambayo Bwana aliyasema kupitia kwa nabii aliposema:
23 “Sikiliza! Msichana bikira atapata mimba
na atazaa mtoto wa kiume.
Mtoto huyo ataitwa Emanueli.”(A)
(Yaani “Mungu yu pamoja nasi”.)
24 Yusufu alipoamka alifanya kama alivyoelekezwa na Malaika wa Bwana. Alimuoa Mariamu. 25 Lakini hakukutana naye kimwili mpaka Mariamu alipomzaa mwana. Na Yusufu akamwita Yesu.
Kuzaliwa kwa Yesu
(Mt 1:18-25)
2 Ulikuwa wakati ambapo amri ilitolewa na Kaisari Augusto kwamba watu wote wanaoishi katika utawala wote wa Rumi[a] wahesabiwe na kuorodheshwa[b] katika kumbukumbu za serikali. 2 Orodha hii ilikuwa ya kwanza tangu Kirenio alipokuwa gavana wa Shamu. 3 Kila mtu alikwenda katika mji aliozaliwa ili akahesabiwe na kuingizwa katika orodha hiyo.
4 Hivyo Yusufu alitoka Nazareti, mji uliokuwa katika jimbo la Galilaya na kwenda katika mji wa Bethlehemu uliokuwa katika jimbo la Uyahudi. Pia, mji huu ulijulikana kama mji wa Daudi. Yusufu alikwenda Bethlehemu kwa sababu alikuwa mzaliwa wa ukoo wa Daudi. 5 Yusufu alijiandikisha akiwa pamoja na Mariamu kwani alikuwa tayari amemchumbia ili amwoe. Na Mariamu alikuwa mjamzito. 6 Yusufu na Mariamu walipokuwa Bethlehemu, wakati wa Mariamu kujifungua ulifika. 7 Akamzaa mwanawe wa kwanza. Akamvingirishia nguo vizuri, kisha akamlaza katika hori la kulishia mifugo.[c] Walimweka humo kwa sababu chumba cha wageni kilikuwa kimejaa.
Wachungaji wa Mifugo Wajulishwa Kuhusu Yesu
8 Usiku ule, baadhi ya wachungaji walikuwa mashambani nje ya mji wa Bethlehemu wakilinda kondoo zao. 9 Malaika wa Bwana akawatokea ghafla, na utukufu wa Bwana ukaangaza kuwazunguka, wakaogopa sana. 10 Malaika akawaambia, “Msiogope, kwa kuwa nimewaletea habari njema zitakazowafurahisha watu wa Mungu wote. 11 Kwa sababu leo katika mji wa Daudi amezaliwa Mwokozi, ndiye Kristo,[d] Bwana. 12 Na hivi ndivyo mtakavyomtambua: Mtamkuta mtoto mchanga amevingirishiwa nguo na amelala katika hori la kulishia mifugo.”
13 Kisha malaika pamoja na jeshi kubwa la mbinguni wakaanza kumsifu Mungu, wakisema:
14 “Atukuzwe Mungu juu mbinguni,
na amani iwepo duniani
kwa watu wote wanaompendeza.”
15 Malaika walipoondoka kurudi mbinguni, wale wachungaji wakaambiana wakisema, “Twendeni Bethlehemu, tukalione jambo hili lililotokea, ambalo Bwana ametujulisha.”
16 Wakaenda haraka, wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala katika hori la kulishia mifugo. 17 Wachungaji walipomwona huyo mtoto, walisimulia kile walichoambiwa na malaika kuhusu mtoto. 18 Kila aliyesikia maelezo ya wachungaji, alishangaa. 19 Mariamu aliendelea kuyatafakari mambo haya, na kuyaweka moyoni. 20 Wachungaji waliirudia mifugo yao, wakawa wanamsifu na kumshukuru Mungu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona. Ilikuwa kama walivyoambiwa na malaika.
21 Ilipofika siku ya nane mtoto alitahiriwa, akaitwa Yesu. Hili ndilo jina alilopewa na malaika kabla mama yake hajaibeba mimba yake.
Yesu Atambulishwa Hekaluni
22 Muda wa kutakaswa ulimalizika, kama ilivyotakiwa na Sheria ya Musa baada ya mtoto kuzaliwa.[e] Baada ya hapo walimpeleka Yesu Yerusalemu na kumweka mbele za Bwana. 23 Kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana: Mzaliwa wa kwanza akiwa mtoto wa kiume, atolewe wakfu kwa ajili ya Bwana.[f] 24 Pia Mariamu na Yusufu walikwenda Yerusalemu kutoa dhabihu kama Sheria ya Bwana inavyosema kuwa, “Ni lazima utoe dhabihu ya jozi moja ya hua[g] au makinda mawili wa njiwa.”
Simeoni Amwona Yesu
25 Alikuwepo mtu mmoja aliyeishi katika mji wa Yerusalemu, mtu huyu aliitwa Simeoni. Alikuwa mtu mwema na mcha Mungu na Roho Mtakatifu alikuwa pamoja naye. Alikuwa akiusubiri wakati ambao Mungu angeisaidia Israeli. 26 Roho Mtakatifu alimwambia kwamba asingekufa kabla ya kumwona Masihi kutoka kwa Bwana. 27 Roho Mtakatifu alimwongoza mpaka Hekaluni. Hivyo, alikuwemo Hekaluni wakati Mariamu na Yusufu walipomleta mtoto Yesu ili wamfanyie kama ilivyotakiwa katika Sheria ya Kiyahudi. 28 Simeoni alimbeba mtoto Yesu mikononi mwake, akamshukuru Mungu na kusema,
29 “Sasa, Bwana, niruhusu mimi mtumishi wako nife kwa amani
kwa kuwa umeitimiza ahadi yako kwangu.
30 Nimeona kwa macho yangu namna utakavyowaokoa watu wako.
31 Sasa watu wote wanaweza kuuona mpango wako.
32 Yeye ni mwanga wa kuionesha njia yako kwa mataifa mengine,
na atawaletea heshima watu wako Israeli.”
33 Mariamu na Yusufu walishangazwa sana na maneno aliyosema Simeoni kuhusu Yesu. 34 Kisha Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu; “Wayahudi wengi wataanguka na wengi watainuka kwa sababu ya mtoto huyu. Atakuwa ishara kutoka kwa Mungu, lakini baadhi ya watu watamkataa. 35 Mawazo ya siri ya watu wengi yatajulikana. Na mambo yatakayotokea yatakuumiza, kama upanga unaokuchoma moyoni.”
Ana Amwona Yesu
36 Alikuwapo nabii aliyeitwa Ana binti Fanueli, kutoka katika kabila la Asheri. Alikuwa mwanamke mzee sana. Aliishi na mume wake kwa miaka saba, 37 kabla ya mume wake kufa na kumwacha peke yake. Na sasa alikuwa na umri wa miaka themanini na nne. Ana alikuwa Hekaluni daima, hakutoka. Alimwabudu Mungu kwa kufunga na kuomba usiku na mchana.
38 Simeoni alipokuwa anazungumza na Yusufu na Mariamu, Ana alikwenda walipokuwa na akaanza kumsifu Mungu na kuwaambia kuhusu Yesu watu wote waliokuwa wanasubiri Mungu kuikomboa Yerusalemu.
© 2017 Bible League International