Old/New Testament
Yesu Azungumza na Mwanamke Msamaria
4 Yesu akatambua ya kwamba Mafarisayo wamesikia habari kuwa alikuwa anapata wafuasi wengi kuliko Yohana na kuwabatiza. 2 (Lakini kwa hakika, Yesu mwenyewe hakumbatiza mtu yeyote huko; bali wafuasi wake ndiyo waliowabatiza watu kwa niaba yake.) 3 Hivyo akaondoka Uyahudi na kurudi Galilaya.
4 Barabara ya kuelekea Galilaya ilimpitisha Yesu katikati ya nchi ya Samaria. 5 Akiwa Samaria Yesu akafika katika mji wa Sikari, ulio karibu na shamba ambalo Yakobo alimpa mwanawe Yusufu. 6 Mahali hapo ndipo kilikuwapo kisima cha Yakobo. Kutokana na safari yake kuwa ndefu Yesu alichoka, hivyo akakaa chini kando ya kisima. Nayo ilikuwa saa sita adhuhuri. 7 Baadaye mwanamke Msamaria akaja kisimani hapo kuchota maji, na Yesu akamwambia, “Tafadhali nipe maji ninywe.” 8 Hili lilitokea wakati wafuasi wake walipokuwa mjini kununua chakula.
9 Mwanamke yule akajibu, “Nimeshangazwa wewe kuniomba maji unywe! Wewe ni Myahudi nami ni mwanamke Msamaria!” (Wayahudi hawana uhusiano na Wasamaria.[a])
10 Yesu akajibu, “Hujui kile Mungu anachoweza kukukirimu. Na hunijui mimi ni nani, niliyekuomba maji ninywe. Kama ungejua, nawe ungekuwa umeniomba tayari, nami ningekupa maji yaletayo uzima.”
11 Mwanamke akasema, “Bwana, utayapata wapi maji yaliyo hai? Kisima hiki kina chake ni kirefu sana, nawe huna kitu cha kuchotea. 12 Je, wewe ni mkuu kumzidi baba yetu Yakobo? Yeye ndiye aliyetupa kisima hiki. Yeye alikunywa kutoka kisima hiki, na wanawe, na wanyama wake wote.”
13 Yesu akajibu, “Kila anayekunywa maji haya ataona kiu tena. 14 Bali yeyote anayekunywa maji ninayompa mimi hatapata kiu tena. Maji ninayowapa watu yatakuwa kama chemichemi inayobubujika ndani yao. Hayo yatawaletea uzima wa milele.”
15 Mwanamke akamwambia Yesu, “Bwana, nipe maji hayo. Kisha sitapata kiu na sitapaswa kuja tena hapa kuchota maji.”
16 Yesu akamwambia, “Nenda kamwite mumeo kisha urudi naye hapa.”
17 Mwanamke akajibu, “Lakini mimi sina mume.”
Yesu akamwambia, “Uko sahihi kusema kuwa huna mume. 18 Hiyo ni kwa sababu, hata kama umekuwa na waume watano, mwanaume unayeishi naye sasa sio mume wako. Huo ndiyo ukweli wenyewe.”
19 Yule mwanamke akasema, “Bwana, naona ya kuwa wewe ni nabii. 20 Baba zetu waliabudu katika mlima huu. Lakini ninyi Wayahudi mnasema kuwa Yerusalemu ndipo mahali ambapo watu wanapaswa kuabudia.”
21 Yesu akasema, “Mwanamke! Niamini mimi, wakati unakuja ambapo hamtakwenda Yerusalemu wala kuja kwenye mlima huu kumwabudu Baba. 22 Ninyi Wasamaria hamwelewi mambo mengi kuhusu yule mnayemwabudu. Sisi Wayahudi tunamfahamu vizuri tunayemwabudu, kwa maana njia yake ya kuuokoa ulimwengu imepatikana kupitia Wayahudi. 23 Lakini wakati unakuja wenye nia halisi ya kuabudu watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa hakika, wakati huo sasa umekwishafika. Na hao ndiyo watu ambao Baba anataka wamwabudu. 24 Mungu ni roho. Hivyo wote wanaomwabudu wanapaswa kumwabudu katika roho na kweli.”
25 Mwanamke akasema, “Naelewa kwamba Masihi anakuja.” (Ndiye anayeitwa Kristo.)
“Atakapokuja, atatufafanulia kila kitu.”
26 Kisha Yesu akasema, “Mimi ninayezungumza nawe sasa, ndiye Masihi.”
27 Wakati huo huo wafuasi wa Yesu wakarudi toka mjini. Nao walishangaa kwa sababu walimwona Yesu akiongea na mwanamke. Lakini hakuna aliyemwuliza yule mwanamke, “Unataka nini?” Wala Yesu, “Kwa nini unaongea naye?”
28 Yule mwanamke akauacha mtungi wake wa maji na kurudi mjini. Akawaambia watu kule, 29 “Mwanaume mmoja amenieleza mambo yote niliyowahi kuyafanya. Njooni mkamwone. Inawezekana yeye ndiye Masihi.” 30 Hivyo wale watu wakatoka mjini wakaenda kumwona Yesu!
© 2017 Bible League International