Read the New Testament in 24 Weeks
1 Salamu kutoka kwa Paulo na Timotheo, watumwa wa Kristo Yesu.[a]
Kwenu ninyi nyote, watakatifu wa Mungu mlioko Filipi, mlio wa Kristo Yesu, wakiwemo wazee[b] na mashemasi wenu.
2 Neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Kristo Yesu, Bwana wetu, iwe pamoja nanyi.
Maombi ya Paulo
3 Ninamshukuru Mungu kila wakati ninapowakumbuka. 4 Kila wakati ninapowaombea ninyi nyote, daima ninawaombea kwa furaha. 5 Ninamshukuru Mungu kwa namna mlivyonisaidia nilipokuwa ninawahubiri watu Habari Njema. Mlinisaidia tangu siku ya kwanza mlipoamini mpaka sasa. 6 Nina uhakika kwamba Mungu, aliyeianzisha kazi njema ndani yenu, ataiendeleza mpaka itakapomalizika siku ile ambayo Kristo Yesu atakuja tena.
7 Ninajua niko sahihi kwa namna ile ninayowawazia ninyi nyote kwa sababu mko karibu sana na moyo wangu. Mmechangia sehemu muhimu sana katika neema ya Mungu kwa ajili yangu wakati huu nikiwa gerezani, na wakati wowote ninapoutetea na kuuthibitisha ukweli wa Habari njema. 8 Mungu anajua kwamba ninataka sana kuwaona. Ninawapenda nyote kwa upendo wa Kristo Yesu.
9 Hili ndiyo ombi langu kwa ajili yenu:
Ya kwamba mkue zaidi na zaidi katika hekima na ufahamu kamili pamoja na upendo; 10 ya kwamba mjue tofauti kati ya kitu kilicho muhimu na kisicho muhimu ili muwe safi msio na lawama, mkiwa tayari kwa siku atakayokuja Kristo; 11 Maisha yenu yajaye matendo mengi mema yanayozalishwa na Kristo Yesu ili kumletea Mungu utukufu na sifa.
Matatizo Ya Paulo Yesaidia Kazi ya Bwana
12 Ndugu zangu, ninataka mjue kwamba yote yaliyonipata yamesaidia katika kusambaza Habari Njema, ingawa ninyi mnaweza kuwa mlitarajia kinyume chake. 13 Walinzi wote wa Kirumi na wengine wote hapa wanafahamu kuwa nimefungwa kwa sababu ninamtumikia Kristo. 14 Kufungwa kwangu gerezani kumesababisha waamini walio wengi hapa kuweka tumaini lao kwa Bwana, na kuhubiri ujumbe wa Mungu kwa ujasiri mwingi pasipo woga.
15 Baadhi ya watu wanahubiri ujumbe wa Kristo kwa sababu wananionea wivu na wanataka watu wawafuate wao badala yangu. Wengine wanahubiri kwa sababu wanataka kusaidia. 16 Wanahubiri kwa sababu ya upendo. Wanafahamu kuwa Mungu ameniweka humu gerezani ili kuitetea Habari Njema. 17 Lakini wengine wanahubiri kuhusu Kristo kwa sababu wanataka kujikweza wenyewe. Chachu yao si safi. Wanafanya hivi kwa kudhani kuwa itanisababishia uchungu mwingi niwapo gerezani. 18 Lakini hiyo haijalishi. Kitu cha muhimu ni kuwa wanawahubiri watu kuhusu Kristo, wakiwa na chachu safi au isiyo safi. Ninafurahi wanafanya hivyo.
Nitaendelea kufurahi, 19 kwa sababu ninajua kwamba kupitia maombi yenu na kipawa cha Roho wa Yesu Kristo mazingira haya magumu hatimaye yataniletea uhuru wangu. 20 Nimejaa tumaini na uhakika, sina sababu yeyote ya kuona haya. Nina uhakika nitaendelea kuwa na ujasiri wa kuhubiri kwa uhuru kama ambavyo nimekuwa. Na Kristo atatukuzwa kwa ninayoyafanya katika mwili wangu, ikiwa nitaishi au nitakufa. 21 Sababu yangu pekee ya kuishi ni kumtumikia Kristo. Kifo kingekuwa bora zaidi. 22 Nikiendelea kuishi hapa ulimwenguni, nitaweza kumfanyia kazi Bwana. Lakini kati ya kufa na kuishi, sijui ningechagua kipi. 23 Ungekuwa uchaguzi mgumu. Ninataka kuyaacha maisha haya ili niwe na Kristo. Hiyo ingekuwa bora zaidi kwangu; 24 hata hivyo, mnanihitaji hapa nikiwa hai. 25 Nina uhakika juu ya hili, hivyo ninajua nitakaa hapa ili niwe nanyi na niwasaidie kukua na kuwa na furaha katika imani yenu. 26 Mtafurahi sana nitakapokuwa hapo pamoja nanyi tena kutokana na kile ambacho Kristo Yesu amefanya ili kunisaidia.
27 Zaidi ya yote, hakikisheni kuwa mnaishi pamoja kama jamii ya watu wa Mungu katika namna inayoiletea heshima Habari Njema kuhusu Kristo. Kisha, ikiwa nitakuja kuwatembelea au ikiwa nitakuwa mbali nanyi na kuyasikia tu mambo kuhusu ninyi, nitajua ya kuwa mmesimama pamoja katika roho moja na kwamba mnafanya kazi pamoja kwa moyo mmoja kama timu moja, katika kuwasaidia wengine kuiamini Habari Njema. 28 Na hamtawaogopa wale walio kinyume nanyi. Imani yenu thabiti itakuwa kama ishara kwao ya kuangamia kwenu. Lakini kwa hakika ni ishara ya wokovu wenu. Na hiki ni kipawa kutoka kwa Mungu. 29 Mungu amewabariki ninyi kwa heshima si ya kumwamini Kristo tu, lakini pia ya kupata mateso kwa ajili yake. 30 Mliyaona magumu mengi niliyokabiliana nayo, na mnasikia kwamba bado nakabiliwa na masumbufu mengi. Ninyi nanyi imewapasa kuyakabili masumbufu hayo pia.
Iweni katika Umoja na Msaidiane
2 Fikirini kuhusu kile ambacho tulichonacho kwa sababu tunamilikiwa na Kristo: hamasa aliyotuletea, faraja ya upendo wake, ushirika katika Roho wake, huruma na wema aliotuonyesha. Ikiwa mnazifurahia baraka hizi, 2 basi fanyeni yale yatakayoikamilisha furaha yangu: iweni na nia moja na mpendane ninyi kwa ninyi. Iweni na umoja katika malengo yenu na katika kufikiri kwenu. 3 Msiruhusu ubinafsi au kiburi viwe dira yenu. Badala yake muwe wanyenyekevu mkiwathamini wengine kuliko ninyi wenyewe. 4 Kila mmoja wenu asijishugulishe kwa mema yake yeye mwenyewe bali kwa mema ya wengine.
5 Hivi ndivyo mnapaswa kufikiri, kuhisi na kutenda katika maisha yenu kwa pamoja, kama vile Kristo Yesu alivyofikiri:
6 Alikuwa sawa na Mungu katika namna zote,
lakini hakufikiri kwamba kuwa sawa na Mungu
kilikuwa kitu cha manufaa kwake.
7 Badala yake, aliacha kila kitu,
hata sehemu yake pamoja na Mungu.
Akakubali kuwa kama mtumwa,
akiwa katika umbo la binadamu.
Wakati wa maisha yake kama mtu,
8 Alijinyenyekeza na akawa mtiifu kabisa kwa Mungu,
hata jambo hilo liliposababisha kifo chake msalabani.
9 Hivyo ndiyo sababu Mungu alimpa mahali pa heshima sana,
na akampa jina lililo kuu kuliko majina yote.
10 Hivyo kila mtu atasujudu kumheshimu Yesu.
Kila mmoja aliye mbinguni, duniani na wale walio chini ya dunia.
11 Wote watakiri kwamba, “Yesu Kristo ni Bwana,”
na hili litamtukuza Mungu Baba.
Iweni Kama Mungu Anavyotaka
12 Rafiki zangu wapendwa, daima mnatii yale mliyofundishwa. Kama mlivyotii nilipokuwa pamoja nanyi, ni muhimu zaidi na zaidi kwamba mtii wakati huu ambapo sipo pamoja nanyi. Hivyo ni lazima mwendelee kuishi katika namna inayoleta maana kwa wokovu wenu. Fanyeni hivi kwa wingi wa heshima na utii kwa Mungu. 13 Ndiyo, Mungu ndiye anayetenda kazi ndani na miongoni mwenu. Anawasaidia ninyi kutaka kutenda yanayomfurahisha, naye anawapa nguvu ya kuyatenda.
14 Fanyeni mambo yote pasipo kulalamika wala kubishana. 15 Nanyi mtakuwa watoto wa Mungu wasiolaumiwa na wasio na hatia. Ijapokuwa mnaishi mkiwa mmezungukwa na watu wasio waaminifu wasiojali thamani haki. Katikati ya watu hao mnang'ara kama mianga katika ulimwengu wenye giza, 16 nanyi mnawapa mafundisho yanayotoa uhai. Hivyo nitaona fahari juu yenu wakati Kristo atakapokuja tena. Ninyi ndiyo mtakaothibitisha kuwa kazi niliyoifanya haikukosa matokeo, ya kwamba nilishindana mbio na nikashinda.
17 Imani yenu inayatoa maisha yenu kama sadaka katika kumtumikia Mungu. Hata kama ni kweli kwamba sasa ninajimimina mimi mwenyewe kama sadaka ya kinywaji pamoja na sadaka yenu, ninayo furaha, na nitawashirikisha ninyi nyote furaha yangu. 18 Ninyi pia mnapaswa kufurahi na kunishirikisha furaha yenu.
Habari Kuhusu Timotheo na Epafrodito
19 Kwa baraka za Bwana Yesu, ninategemea kuwa nitamtuma Timotheo kwenu hivi karibuni. Naye atarejesha kwangu taarifa kuhusu ninyi ili nifurahi. 20 Sina mtu mwingine yeyote kama Timotheo, ambaye kwa dhati kabisa anayajali mambo yanayowahusu. 21 Wengine wote wanajishughulisha na maisha yao wenyewe. Hawajali kazi ya Yesu Kristo. 22 Mnafahamu Timotheo amejithibitisha kuwa ni mtu wa aina gani. Ametumika pamoja nami katika kuhubiri Habari Njema kwa njia ambavyo mwana angemtumikia baba yake. 23 Ninategemea kumtuma aje kwenu haraka baada ya kujua yatakayonipata. 24 Bwana hunifanya niwe jasiri ili niweze pia kuja kwenu haraka.
25 Kwa sasa, nadhani ni lazima nimrudishe Epafrodito kwenu. Ni mtumishi na mtenda kazi pamoja nami na askari mwenzangu katika jeshi la Bwana. Nilipotaka msaada, mlimtuma kwangu. Kama mjumbe wenu, alinihudumia mahitaji yangu. 26 Lakini sasa anataka kuwaona ninyi nyote tena. Ana wasiwasi sana kwa sababu mlisikia kuwa alikuwa mgonjwa. 27 Alikuwa mgonjwa karibu ya kufa. Lakini Mungu alimsaidia yeye na mimi ili nisiwe na huzuni zaidi. 28 Hivyo ninataka sana kumtuma kwenu. Ili mtakapomwona, mfurahi. Nami nitaacha kuwa na wasiwasi juu yenu. 29 Mkaribisheni kwa furaha nyingi katika Bwana. Waheshimuni watu kama Epafrodito. 30 Anapaswa kuheshimiwa kwa sababu alikaribia kufa akifanya kazi kwa ajili ya Kristo. Aliyaweka maisha yake katika hatari ili aweze kunisaidia. Ni msaada ambao msingeweza kunisaidia.
© 2017 Bible League International