M’Cheyne Bible Reading Plan
1 Kutoka kwa Petro, mtume wa Yesu Kristo.
Kwa wateule wa Mungu, ambao huonekana kama ni wageni kutoka nchi nyingine, waliotawanyika katika majimbo yote ya Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia. 2 Kwa kadri ya mpango wa Mungu Baba alioufanya muda mrefu uliopita, mliteuliwa muwe wake kwa kufanywa watakatifu na Roho Mtakatifu. Mliteuliwa kuwa waatiifu kwa Mungu na kutakaswa na kujumuishwa miongoni mwa watu wa Agano Jipya kwa kunyunyiziwa damu ya Yesu Kristo.[a]
Neema na amani ya Mungu viwe pamoja nanyi kwa wingi.
Tumaini Lililo Hai
3 Atukuzwe Mungu Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo! Katika rehema zake kuu, Mungu alitufanya sisi tuzaliwe upya ili tuwe na tumaini lililo hai, kwa njia ya ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa waliokufa, 4 na ili kuwa na urithi usioharibika, ulio safi na usiofifia, uliotunzwa kwa ajili yenu kule mbinguni.
5 Ni kwa ajili yenu ninyi ambao kwa njia ya imani, mnalindwa na nguvu za Mungu ili mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho. 6 Hili linawafanya mfurahi sana, hata kama kwa sasa imewalazimu mhuzunishwe kwa kipindi kifupi kwa masumbufu na mateso ya aina mbali mbali. 7 Kwa masumbufu haya imani yenu inajaribiwa na kuithibitishwa kuwa ni ya kweli. Hii inafananishwa na dhahabu pale inapopitishwa kwenye moto kuthibitisha uhalisi wake. Lakini hata dhahabu ya kweli inaweza kuharibiwa. Hivyo imani ina thamani zaidi kuliko dhahabu. Pale imani yenu inapothibitika kuwa ni ya kweli, matokeo yake ni sifa, utukufu na heshima kwa Mungu wakati wa kurudi kwake Yesu Kristo.
8 Hata kama hamjamwona Yesu, lakini mnampenda. Hata kama hamuwezi kumuona kwa sasa, lakini mnamwamini yeye na mmejazwa na furaha ya ajabu isiyoweza kuelezwa kwa maneno. 9 Mnaupokea wokovu wenu ambao ni lengo la imani yenu.
10 Manabii waliotabiri juu ya neema ambayo ingeoneshwa kwenu, walipeleleza kwa makini na kwa uangalifu wakaulizia habari za wokovu huu. 11 Roho wa Kristo alikuwa ndani yao, naye aliwapa ushuhuda mapema kuhusu Kristo kwamba itamlazimu kuteswa na baada ya hapo atapokea utukufu. Manabii waliuliza kutaka kujua wakati gani na katika mazingira gani mambo haya yangetokea.
12 Ilifunuliwa kwao kwamba walikuwa hawajitumikii wenyewe. Badala yake, waliwatumikia ninyi walipotabiri juu ya mambo haya. Na sasa mmesikia juu ya mambo haya kutoka kwa wale waliyowaambia habari Njema kwa msaada wa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. Hata malaika wangetamani sana kufahamu zaidi juu ya mambo haya mliyoambiwa.
Mwito Kwa Maisha Matakatifu
13 Hivyo mkeshe katika fahamu zenu na kuwa na kiasi. Yawekeni kikamilifu matumaini yenu katika baraka mtakazopewa wakati Yesu Kristo atakapofunuliwa. 14 Kama watoto watiifu, msiyaache maisha yenu yandelee kutawaliwa na tamaa mbaya mlizokuwa nazo awali mlipokuwa wajinga. 15 Badala yake, kama ambavyo yeye Mungu aliyewaita alivyo mtakatifu, hata ninyi muwe watakatifu katika kila mnalotenda. 16 Hivyo Maandiko yanasema: “Iweni watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.”(A)
17 Na kama Baba mnayemwita Mungu anayewahukumu watu bila upendeleo kwa kadri ya matendo ya kila mtu, muishi maisha ya utauwa na hofu kwa Mungu katika miaka yenu ya kukaa humu duniani kama wageni. 18 Mnajua kwamba siyo kwa mambo yaharibikayo kama fedha au dhahabu, kwamba mliokolewa kutoka katika maisha yasiyofaa mliyoyapokea kutoka kwa babu zenu, 19 bali kwa damu ya thamani ya Kristo, kama ile ya mwanakondoo asiye na dosari wala ila. 20 Kristo alichaguliwa kabla ya uumbaji wa ulimwengu, lakini alidhihirishwa katika siku hizi za mwisho kwa ajili yenu. 21 Kupitia Kristo mmekuwa waamini katika Mungu, aliyemfufua kutoka kwa wafu na kumpatia utukufu. Ili imani yenu na matumaini yawekwe katika Mungu.
22 Sasa kwa vile mmejitakasa wenyewe kwa kuitii kweli hadi mwisho kwamba mtaonesha upendo wa kweli wa kindugu, jitahidini kupendana ninyi kwa ninyi kwa mioyo iliyo safi. 23 Mmezaliwa upya sio kama matokeo ya mbegu inayoharibika, lakini kama matokeo ya mbegu isiyoharibika. Mmezaliwa upya kwa njia ya ujumbe wa Mungu, ambao unaleta uzima ndani yenu. 24 Hivyo, kama Maandiko yanavyosema:
“Watu wote ni kama manyasi,
na utukufu wao wote ni kama maua pori katika manyasi.
Manyasi yananyauka na kukauka,
na maua yanapukutika,
25 bali ujumbe wa Bwana unadumu milele.”(B)
Na ujumbe huo ni habari njema iliyohubiriwa kwenu.
Yesu Akiwa Galilaya
8 Siku iliyofuata, Yesu alisafiri kupitia katika baadhi ya miji na vijiji. Yesu aliwahubiri watu Habari Njema kuhusu ufalme wa Mungu. Mitume kumi na wawili walikuwa pamoja naye. 2 Walikuwepo pia baadhi ya wanawake ambao Yesu aliwaponya magonjwa na pepo wabaya. Mmoja wao alikuwa Mariamu aitwaye Magdalena ambaye alitokwa na pepo saba; 3 Pia pamoja na wanawake hawa alikuwepo Yoana mke wa Kuza (msimamizi wa mali za Herode), Susana, na wanawake wengine wengi. Wanawake hawa walitumia fedha zao kuwahudumia Yesu na mitume wake.
Simulizi Kuhusu Mkulima Aliyepanda Mbegu
(Mt 13:1-17; Mk 4:1-12)
4 Kundi kubwa la watu lilikusanyika. Watu walimjia Yesu kutoka katika kila mji, naye Yesu akawaambia fumbo hili:
5 “Mkulima alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akizitawanya, baadhi zilianguka kandokando ya njia. Watu wakazikanyaga, na ndege wa angani wakazila. 6 Zingine zikaanguka kwenye udongo wenye mawe. Zilipoanza kukua zikafa kwa sababu ya kukosa maji. 7 Mbegu zingine ziliangukia kwenye miiba. Miiba ikakua pamoja nazo, miiba ikazisongasonga na hazikukua. 8 Zilizosalia ziliangukia kwenye udongo mzuri wenye rutuba. Mbegu hizi zikaota na kuzaa kila moja mia.”
Yesu akamalizia fumbo. Kisha akapaza sauti, akasema, “Ninyi watu mnaonisikia, sikilizeni!”
9 Wafuasi wake wakamwuliza, “Fumbo hili linamaanisha nini?”
10 Akasema, “Mmechaguliwa kujua kweli za siri kuhusu ufalme wa Mungu. Lakini ninatumia mafumbo kuzungungumza na watu wengine. Ninafanya hivi ili,
‘Watazame,
lakini wasiweze kuona.
Wasikia,
lakini wasielewe.’(A)
Yesu Afafanua Simulizi Kuhusu Mbegu
(Mt 13:18-23; Mk 4:13-20)
11 Hii ndiyo maana ya fumbo hili: Mbegu ni Neno la Mungu. 12 Watu wengine ni kama mbegu zilizoanguka njiani. Husikia mafundisho ya Mungu, lakini Shetani huja na kuwafanya waache kuyatafakari. Hii huwafanya kutoamini na kuokoka. 13 Wengine wanafanana na mbegu zilizoanguka kwenye udongo wenye mawe. Ni watu ambao huyasikia mafundisho ya Mungu na kuyapokea kwa furaha, lakini kwa kuwa hawana mizizi yenye kina, huamini kwa muda mfupi. Majaribu yanapokuja, humwacha Mungu.
14 Zilizoanguka katika miiba, zinafanana na watu wanaoyasikia Mafundisho ya Mungu, lakini wanaruhusu wasiwasi, mali na anasa za maisha haya kuwasimamisha na hawaendelei kukua. Hivyo mafundisho hayazalishi matokeo mazuri katika maisha yao.[a] 15 Na zile zilizoangukia katika udongo mzuri, ni wale ambao huyasikia mafundisho ya Mungu kwa moyo safi na mnyoofu. Huyatii na kwa uvumilivu wao huzaa mazao mazuri.
Zingatieni Nuru
(Mk 4:21-25)
16 Hakuna mtu anayewasha taa na kuifunika kwa bakuli au kuificha uvunguni mwa kitanda. Badala yake huiweka kwenye kinara cha taa mahali palipo wazi, ili wanaoingia ndani wapate nuru ya kuwawezesha kuona. 17 Kila jambo lililofichwa litawekwa wazi na kila siri itajulikana na kila mtu ataiona. 18 Hivyo yatafakarini kwa umakini yale mnayosikia. Watu wenye uelewa kiasi watapokea zaidi. Lakini wale wasio na uelewa watapoteza hata ule wanaodhani kuwa wanao.”
Wafuasi wa Yesu ni Familia Yake Halisi
(Mt 12:46-50; Mk 3:31-35)
19 Mama yake Yesu na wadogo zake wakaenda kumwona, lakini walishindwa kumfikia kwa sababu walikuwepo watu wengi sana. 20 Mtu mmoja akamwambia Yesu, “Mama yako na wadogo zako wamesimama nje. Wanataka kukuona.”
21 Yesu akawajibu “Mama yangu na wadogo zangu ni wale wanaolisikia na kulitii Neno la Mungu.”
Yesu Atuliza Dhoruba
(Mt 8:23-27; Mk 4:35-41)
22 Siku moja Yesu na wafuasi wake walipanda mashua. Akawaambia, “Tuvuke mpaka upande mwingine wa ziwa.” Wakaanza safari kuvuka ziwa. 23 Walipokuwa wanasafiri, Yesu alisinzia. Tufani kubwa ikalikumba ziwa na mashua ikaanza kujaa maji, wakawa katika hatari. 24 Wafuasi wakamwendea, wakamwamsha, wakasema, “Mkuu, mkuu, tutazama!”
Yesu akasimama, akaukemea upepo na mawimbi ya maji. Upepo ukakoma na ziwa likatulia. 25 Ndipo Yesu akawaambia wafuasi wake, “Imani yenu iko wapi?”
Lakini wao waliogopa na kustaajabu, wakanong'onezana, “Huyu ni mtu wa namna gani? Anaamuru upepo na maji, na vinamtii?”
Yesu Amweka Huru Mtu Kutoka Pepo Wachafu
(Mt 8:28-34; Mk 5:1-20)
26 Yesu na wafuasi wake wakasafiri mpaka katika nchi walimoishi Wagerasi[b] iliyokuwa ng'ambo ya ziwa Galilaya. 27 Yesu alipotoka katika mashua, mwanaume mmoja kutoka katika mji ule alimwendea. Mtu huyu alikuwa na mapepo ndani yake. Kwa muda mrefu hakuwahi kuvaa nguo na aliishi makaburini.
28-29 Pepo aliyekuwa ndani yake alikuwa akimpagaa mara nyingi na alikuwa akifungwa gerezani, mikono na miguu yake ikiwa imefungwa kwa minyororo. Lakini kila mara aliivunja. Pepo ndani yake alikuwa anamlazimisha kwenda nje ya mji mahali pasipoishi watu. Yesu alimwamuru kumtoka mtu yule. Alipomwona Yesu, alianguka mbele yake huku akipiga kelele kwa sauti, “Unataka nini kwangu, Yesu, Mwana wa Mungu Mkuu Aliye Juu? Tafadhali usiniadhibu!”
30 Yesu akamwuliza, “Jina lako nani?”
Mtu yule akajibu, “Jeshi.”[c] (Alisema jina lake ni “Jeshi” kwa sababu pepo wengi walikuwa wamemwingia.) 31 Pepo wale wakamsihi Yesu asiwaamuru kwenda shimoni.[d] 32 Katika kilima kile, kulikuwa kundi kubwa la nguruwe wakichungwa. Pepo wakamsihi Yesu awaruhusu wawaingie wale nguruwe. Hivyo Yesu akawaruhusu. 33 Pepo wakamtoka yule mtu, na kuwaingia nguruwe. Kundi lote la wale nguruwe likakimbia kutelemkia ziwani kwa kasi, nguruwe wakazama na kufia humo.
34 Wachungaji wa nguruwe walipoona lililotokea, walikimbia, wakaenda kutoa taarifa mjini na mashambani. 35 Watu wakaenda kuona lililotokea. Walipofika alipokuwa Yesu wakamwona mtu yule aliyetokwa na pepo ameketi karibu na Yesu, amevaa nguo, akiwa na akili zake timamu; pepo walikuwa wamemtoka. Jambo hili likawaogopesha watu. 36 Wale walioona mambo haya yalivyotokea waliwaambia wengine namna Yesu alivyomponya yule mtu. 37 Watu wote waliokuwa wakiishi eneo lote la Gerasi wakamtaka Yesu aondoke kwa sababu waliogopa.
Hivyo Yesu akapanda mashua na kurudi Galilaya. 38 Mtu aliyeponywa alimsihi amfuate Yesu. Lakini Yesu akamtuma, akamwambia, 39 “Rudi nyumbani, ukawaeleze watu mambo ambayo Mungu amekutendea.”
Hivyo mtu yule alikwenda sehemu zote za mji akieleza mambo ambayo Yesu amemtendea.
Yesu Anampa Uhai Msichana Aliyekufa na Kumponya Mwanamke Mgonjwa
(Mt 9:18-26; Mk 5:21-43)
40 Yesu aliporudi Galilaya, watu walimkaribisha. Kila mtu alikuwa anamsubiri. 41-42 Mtu mmoja jina lake Yairo, aliyekuwa mkuu wa sinagogi alimwendea. Alikuwa na binti mmoja tu mwenye umri wa miaka kumi na mbili na alikuwa mgonjwa sana katika hali ya kufa. Hivyo Yairo alisujudu miguuni pa Yesu na akamsihi aende nyumbani kwake.
Yesu alipokuwa akienda nyumbani kwa Yairo, watu walimzonga kila upande. 43 Mwanamke aliyekuwa akitokwa damu kwa miaka kumi na mbili alikuwepo katika umati huo. Alikuwa ametumia mali zake zote kwa madaktari,[e] lakini hakuna daktari aliyeweza kumponya. 44 Alikwenda nyuma ya Yesu na kugusa pembe ya vazi lake. Wakati huo huo damu ikaacha kumtoka. 45 Ndipo Yesu akasema, “Nani amenigusa?”
Kila mtu alikataa kuwa hajamgusa, Petro akasema, “Mkuu, watu wamekuzunguka na wanakuzongazonga kila upande.”
46 Lakini Yesu akasema, “Kuna mtu amenigusa. Nimesikia nguvu ikinitoka.” 47 Yule mwanamke alipoona ya kwamba hataweza kujificha akajitokeza akitetemeka. Akasujudu mbele ya Yesu. Huku kila mmoja akisikia, akaeleza sababu iliyomfanya amguse, na kwamba alipona wakati ule ule alipomgusa. 48 Yesu alimwambia, “Binti yangu umeponywa kwa sababu uliamini. Nenda kwa amani.”
49 Yesu alipokuwa bado anaongea, mtu mmoja kutoka nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi alikuja na akasema, “Binti yako amekwisha kufa! Hakuna haja ya kuendelea kumsumbua Mwalimu.”
50 Yesu aliposikia maneno hayo, alimwambia Yairo, “Usiogope! Amini tu na binti yako ataponywa.”
51 Yesu akaenda nyumbani, alipofika akaruhusu Petro, Yohana, Yakobo pamoja na baba na mama wa yule mtoto tu kuingia ndani pamoja naye. 52 Kila mtu alikuwa akilia na kusikia huzuni kwa sababu msichana alikuwa amekufa. Lakini Yesu akasema, “Msilie. Hajafa. Amelala usingizi tu.”
53 Watu wakamcheka, kwa sababu walijua kuwa amekwisha kufa. 54 Lakini Yesu akamshika mkono na kumwambia, “Mtoto inuka!” 55 Roho yake ikamrudia, akasimama hapo hapo. Yesu akasema, “Mpeni chakula.” 56 Wazazi wa yule binti wakashangaa. Yesu akawakataza wasimwambie mtu yeyote lililotokea.
© 2017 Bible League International