M’Cheyne Bible Reading Plan
Yohana Atayarisha Njia kwa Ajili ya Yesu
(Mt 3:1-12; Mk 1:1-8; Yh 1:19-28)
3 Katika mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Kaisari Tiberio, ambapo:
Pontio Pilato alikuwa gavana wa Uyahudi;
Herode alikuwa mtawala wa Galilaya;
Filipo ndugu yake Herode alikuwa mtawala wa Iturea na Trakoniti;
na Lisania, alikuwa mtawala wa Abilene.
2 Anasi na Kayafa walikuwa makuhani wakuu. Katika kipindi hiki, Yohana, mwana wa Zakaria, alikuwa akiishi jangwani na alipata ujumbe kutoka kwa Mungu. 3 Alipita katika maeneo yote yaliyo karibu na Mto Yordani akiwahubiri watu ujumbe kutoka kwa Mungu. Aliwaambia wabatizwe kuonesha kuwa wamekubali kubadili maisha yao ndipo dhambi zao zitasamehewa. 4 Hii ni kama maneno yaliyoandikwa katika kitabu cha nabii Isaya, yanayosema,
“Kuna mtu anayeipaza sauti yake kutokea nyikani:
‘Tayarisheni njia kwa ajili ya Bwana;
nyoosheni njia kwa ajili yake.
5 Kila bonde litajazwa,
na kila mlima na kilima vitasawazishwa.
Barabara zilizopinda zitanyooshwa,
na barabara zenye mashimo zitasawazishwa.
6 Na kila mtu ataona
jinsi Mungu atakavyowaokoa watu wake.’”(A)
7 Makundi ya watu walimwendea Yohana ili awabatize. Lakini aliwaambia, “Enyi nyoka! Ni nani aliyewaonya kuikimbia hukumu ya Mungu inayokuja? 8 Badilisheni mioyo yenu! Kisha onesheni ya kuwa mmebadilika kwa namna mnavyoishi. Ninajua mtasema kuwa, ‘Ibrahimu ni baba yetu.’ Hilo halijalishi chochote. Ninawaambia Mungu anaweza kumwumbia Ibrahimu watoto kutokana na mawe haya! 9 Na sasa shoka liko tayari kukata miti,[a] kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.”
10 Watu wakamwuliza Yohana, “Tufanye nini?”
11 Akajibu, “Ukiwa na mashati mawili mpe moja asiyekuwa na shati. Kama una chakula, kigawe pia.”
12 Hata watoza ushuru walikuja kwa Yohana. Walitaka wabatizwe. Walimwambia, “Mwalimu, tufanye nini sisi?”
13 Akawaambia, “Msitoze ushuru zaidi kuliko kiwango kilichoamriwa.”
14 Askari wakamwuliza, “Vipi kuhusu sisi? Tufanye nini?”
Akawaambia, “Msitumie nguvu au kutengeneza mashtaka ya uongo ili watu wawape pesa. Mtosheke na mishahara mnayopata.”
15 Kila mtu alitarajia kuja kwa Masihi,[b] na walijiuliza wakisema, “Labda Yohana ndiye Masihi.”
16 Yohana aliwajibu watu wote, akasema, “Ninawabatiza ninyi katika maji, lakini yupo mwingine ajaye baada yangu, mwenye nguvu zaidi kuliko mimi, huyo atafanya mengi zaidi yangu. Nami niliye mtumwa wa chini kabisa sistahili hata kuinama na kufungua kamba za viatu vyake. Yeye huyo atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto. 17 Yuko tayari sasa kuja kusafisha nafaka. Atatenganisha nafaka nzuri na makapi, na kuiweka katika ghala yake kisha ataichoma ile isiyofaa katika moto usiozimika.” 18 Hivi ndivyo ambavyo Yohana aliwahubiri watu Habari Njema. Aliwaonya sana kuwa wanatakiwa kubadili njia zao.
Kazi ya Yohana Ilivyomalizika Baadaye
19 Yohana alimkosoa Herode kwa sababu ya mambo mabaya aliyokuwa ameyafanya na Herodia, mkewe kaka yake Herode, na pia kwa mambo mengine mabaya aliyokuwa ameyafanya. 20 Hivyo Herode aliongeza jambo jingine baya katika matendo yake maovu. Alimfunga Yohana gerezani.
Yohana Ambatiza Yesu
(Mt 3:13-17; Mk 1:9-11)
21 Watu wote walipokuwa wakibatizwa, Yesu alikuja naye akabatizwa. Na alipokuwa akiomba, mbingu zilifunguka, 22 na Roho Mtakatifu aliyekuwa katika umbo la njiwa akashuka juu yake. Sauti ikasikika toka mbinguni, “Wewe ni mwanangu, ninayekupenda, napendezwa nawe sana.”
Ukoo wa Yesu
(Mt 1:1-17)
23 Yesu alipoanza kufundisha, alikuwa na umri kama wa miaka thelathini. Watu walidhani kuwa Yesu alikuwa Mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Eli.
24 Eli alikuwa mwana wa Mathati.
Mathati alikuwa mwana wa Lawi.
Lawi alikuwa mwana wa Melki.
Melki alikuwa mwana wa Yana.
Yana alikuwa mwana wa Yusufu.
25 Yusufu alikuwa mwana wa Matathia.
Matathia alikuwa mwana wa Amosi.
Amosi alikuwa mwana wa Nahumu.
Nahumu alikuwa mwana wa Esli.
Esli alikuwa mwana wa Nagai.
26 Nagai alikuwa mwana wa Maathi.
Maathi alikuwa mwana wa Matathia.
Matathia alikuwa mwana wa Semei.
Semei alikuwa mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Yoda.
27 Yoda alikuwa mwana wa Yoana.
Yoana alikuwa mwana wa Resa.
Resa alikuwa mwana wa Zerubabeli.
Zerubabeli alikuwa mwana wa Shealtieli.
Shealtieli alikuwa mwana wa Neri.
28 Neri alikuwa mwana wa Melki.
Melki alikuwa mwana wa Adi.
Adi alikuwa mwana wa Kosamu.
Kosamu alikuwa mwana wa Elmadamu,
Elmadamu alikuwa mwana wa Eri.
29 Eri alikuwa mwana wa Yoshua.
Yoshua alikuwa mwana wa Eliezeri.
Eliezeri alikuwa mwana wa Yorimu.
Yorimu alikuwa mwana wa Mathati.
Mathati alikuwa mwana wa Lawi.
30 Lawi alikuwa mwana wa Simeoni.
Simeoni alikuwa mwana wa Yuda.
Yuda alikuwa mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Yonamu.
Yonamu alikuwa mwana wa Eliakimu.
31 Eliakimu alikuwa mwana wa Melea.
Melea alikuwa mwana wa Mena.
Mena alikuwa mwana wa Matatha.
Matatha alikuwa mwana wa Nathani.
Nathani alikuwa mwana wa Daudi.
32 Daudi alikuwa mwana wa Yese.
Yese alikuwa mwana wa Obedi.
Obedi alikuwa mwana wa Boazi.
Boazi alikuwa mwana wa Salmoni.[c]
Salmoni alikuwa mwana wa Nashoni.
33 Nashoni alikuwa mwana wa Aminadabu.
Aminadabu alikuwa mwana wa Admini,
Admini alikuwa mwana wa Aramu.[d]
Aramu alikuwa mwana wa Hesroni.
Hesroni alikuwa mwana wa Peresi.
Peresi alikuwa mwana wa Yuda.
34 Yuda alikuwa mwana wa Yakobo.
Yakobo alikuwa mwana wa Isaka.
Isaka alikuwa mwana wa Ibrahimu.
Ibrahimu alikuwa mwana wa Tera.
Tera alikuwa mwana wa Nahori.
35 Nahori alikuwa mwana wa Serugi,
Serugi alikuwa mwana wa Ragau.
Ragau alikuwa mwana wa Pelegi.
Pelegi alikuwa mwana wa Eberi,
Eberi alikuwa mwana wa Sala.
36 Sala alikuwa mwana wa Kenani.
Kenani alikuwa mwana wa Arfaksadi.
Arfaksadi alikuwa mwana wa Shemu.
Shemu alikuwa mwana wa Nuhu.
Nuhu alikuwa mwana wa Lameki.
37 Lameki alikuwa mwana wa Methusela.
Methusela alikuwa mwana wa Henoko.
Henoko alikuwa mwana wa Yaredi.
Yaredi alikuwa mwana wa Mahalaleli.
Mahalaleli alikuwa mwana wa Kenani.
38 Kenani alikuwa mwana wa Enoshi.
Enoshi alikuwa mwana wa Sethi.
Sethi alikuwa mwana wa Adamu.
Adamu alikuwa mwana wa Mungu.
Mitume wa Kristo Yesu
4 Tuchukulieni sisi kuwa ni watumishi wa Kristo, ambao Mungu ametuamini tufanye kazi ya kuwaambia wengine siri zake za kweli. 2 Wale walioaminiwa kwa kazi muhimu kama hii imewapasa kuonesha ya kuwa wao ni waaminifu. 3 Lakini siichukulii hukumu yenu kuhusu hili kuwa kitu. Hata hukumu yo yote katika mahakama ya kibinadamu isingekuwa na maana yoyote. Sijihukumu hata mimi mwenyewe. 4 Sikumbuki kosa lolote nililofanya, lakini hiyo hainifanyi mimi kujihesabia haki. Bwana pekee ndiye anayepaswa kunihukumu ikiwa nimefanya vyema au la. 5 Hivyo, msimhukumu mtu yeyote sasa. Hukumu itakuwa wakati Bwana atakaporudi. Ataangaza mwanga kwa kila kitu kilichofichwa gizani. Ataziweka wazi nia za siri za mioyo yetu. Ndipo sifa ambayo kila mtu anapaswa kuipata itatoka kwa Mungu.
6 Ndugu zangu, nimemtumia Apolo na mimi mwenyewe kama mfano kwa ajili yenu. Nimefanya hivi ili mjifunze kutoka kwetu maana ya maneno yanayosema, “Uwe mwangalifu kufuata kilichoandikwa.”[a] 7 Kwa nini mnajisifu? Mlipewa kila kitu mlicho nacho. Sasa, ikiwa mlipewa kila kitu mlicho nacho, kwa nini mnajisifu kana kwamba mlipata vitu vyote kwa nguvu zenu wenyewe?
8 Mnadhani kwamba tayari mna kila kitu mnachohitaji. Mnadhani kwamba mmekwisha tajirika. Laiti mngekwisha fanywa wafalme, kwa sababu tungekuwa wafalme pamoja nanyi. 9 Lakini inaonekana kana kwamba Mungu amenipa mimi na mitume wengine mahali pa mwisho. Sisi ni kama wafungwa waliohukumiwa kufa, waliosimamishwa katika gwaride ili ulimwengu wote uwaone, si watu tu bali hata malaika pia. 10 Tu wapumbavu kwa kuwa sisi ni wa Kristo, lakini mnadhani kuwa ninyi ni wenye hekima katika Kristo. Sisi ni dhaifu, lakini mnadhani kuwa mna nguvu. Watu wanawaheshimu ninyi, na hawatuheshimu sisi. 11 Hata sasa hatuna vyakula vya kutosha kula au kunywa, na hatuna nguo za kutosha. Mara kwa mara tunapigwa na hatuna makazi. 12 Tunafanya kazi sana kwa mikono yetu ili tupate chakula. Watu wanapotutukana, tunamwomba Mungu awabariki. Watu wanapotutendea vibaya, tunavumilia. 13 Watu wanaposema mabaya juu yetu, tunawajibu kwa upole. Lakini watu wanaendelea kutuona kama takataka.
14 Siwaambii haya ili kuwatahayarisha, lakini ninaandika haya ili kuwaonya kama watoto wangu mwenyewe ninaowapenda. 15 Mnaweza kuwa na walimu elfu kumi katika Kristo, lakini hamna baba wengi. Kupitia Habari Njema mimi nilifanyika baba kwenu katika Kristo Yesu. 16 Ndiyo sababu ninawahimiza mfuate mfano wangu. 17 Ndiyo sababu ninamtuma Timotheo kwenu. Ni mwanangu katika Bwana. Ninampenda na ni mwaminifu. Atawasaidia ili mkumbuke namna ninavyoishi kama mfuasi wa Kristo Yesu, kama ninavyofundisha katika kila kanisa kila mahali ninakokuwa.
18 Baadhi yenu mnajivuna, mkidhani kuwa sitakuja kuwatembelea tena. 19 Lakini nitakuja kwenu hivi karibuni ikiwa Bwana atanijalia. Ndipo nitajua ikiwa hawa wanaojivuna wana nguvu za kutenda jambo lolote zaidi ya kuzungumza. 20 Mungu huonesha kuwa anatawala katika maisha kwa yale wanayoweza kufanya na si kwa maneno yao. 21 Je, nitakapokuja kwenu, nije nikiwa na adhabu au nije kwa upendo na upole?
© 2017 Bible League International