Book of Common Prayer
Tumaini Lililo Hai
3 Atukuzwe Mungu Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo! Katika rehema zake kuu, Mungu alitufanya sisi tuzaliwe upya ili tuwe na tumaini lililo hai, kwa njia ya ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa waliokufa, 4 na ili kuwa na urithi usioharibika, ulio safi na usiofifia, uliotunzwa kwa ajili yenu kule mbinguni.
5 Ni kwa ajili yenu ninyi ambao kwa njia ya imani, mnalindwa na nguvu za Mungu ili mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho. 6 Hili linawafanya mfurahi sana, hata kama kwa sasa imewalazimu mhuzunishwe kwa kipindi kifupi kwa masumbufu na mateso ya aina mbali mbali. 7 Kwa masumbufu haya imani yenu inajaribiwa na kuithibitishwa kuwa ni ya kweli. Hii inafananishwa na dhahabu pale inapopitishwa kwenye moto kuthibitisha uhalisi wake. Lakini hata dhahabu ya kweli inaweza kuharibiwa. Hivyo imani ina thamani zaidi kuliko dhahabu. Pale imani yenu inapothibitika kuwa ni ya kweli, matokeo yake ni sifa, utukufu na heshima kwa Mungu wakati wa kurudi kwake Yesu Kristo.
8 Hata kama hamjamwona Yesu, lakini mnampenda. Hata kama hamuwezi kumuona kwa sasa, lakini mnamwamini yeye na mmejazwa na furaha ya ajabu isiyoweza kuelezwa kwa maneno. 9 Mnaupokea wokovu wenu ambao ni lengo la imani yenu.
Yesu Awafariji Wafuasi Wake
14 Yesu akasema, “Msisumbuke. Mwaminini Mungu, na mniamini na mimi. 2 Kuna vyumba vya kutosha katika nyumba ya Baba yangu. Nisingewaambia hivi ikiwa isingelikuwa kweli. Ninaenda huko kuandaa mahali kwa ajili yenu. 3 Nitakapomaliza kuandaa, nitarudi. Kisha nitawachukua ili muwe pamoja nami mahali niliko. 4 Mnaijua njia iendayo kule ninakokwenda.”
5 Thomaso akasema, “Bwana, hatujui unakokwenda, sasa tutaijuaje njia?”
6 Yesu akajibu, “Mimi ndiye njia, kweli, na uzima. Njia pekee ya kwenda kwa Baba ni kupitia kwangu. 7 Kwa kuwa sasa ninyi nyote mmenijua, mtamjua Baba yangu pia. Kwa kweli, sasa mnamjua Baba na mmekwisha kumwona.”
© 2017 Bible League International