Book of Common Prayer
7 Kisha kulikuwa vita mbinguni. Mikaeli[a] na malaika zake walipigana na joka. Nalo joka na malaika zake wakapigana na Mikaeli pamoja na malaika zake, 8 lakini joka na malaika zake hawakuwa na nguvu za kutosha kushinda, na hivyo wakapoteza nafasi zao mbinguni. 9 Likatupwa chini kutoka mbinguni. (Joka hili kubwa ni nyoka yule wa zamani, aitwaye Ibilisi au Shetani, anayeudanganya ulimwengu wote.) Joka na malaika zake walitupwa duniani.
10 Kisha nilisikia sauti kubwa mbinguni ikisema:
“Ushindi na uweza na ufalme wa Mungu wetu
na mamlaka ya Masihi wake umekuja sasa,
kwa sababu mshitaki wa kaka na dada zetu
ametupwa chini.
Ndiye aliyewashitaki kwa Mungu,
mchana na usiku.
11 Walimshinda kwa sadaka ya damu ya Mwanakondoo
na kwa ujumbe wa Mungu waliowaambia watu.
Hawakuyapenda maisha yao sana.
Hawakuogopa kifo.
12 Hivyo furahi, ewe mbingu
na wote waishio humo!
Lakini ole kwa nchi na bahari,
kwa sababu Ibilisi ameshuka kwako.
Amejaa ghadhabu.
Anajua ana muda mchache.”
13 Joka alipoona amekwisha tupwa chini duniani, alimkimbiza mwanamke aliyemzaa mtoto wa kiume. 14 Lakini mwanamke alipewa mabawa mawili ya tai mkuu. Aliweza kuruka mpaka mahali palipoandaliwa kwa ajili yake jangwani. Huko atatunzwa kwa muda wa miaka mitatu na nusu akiwa mbali na joka. 15 Kisha joka lilitoa maji kama mto kutoka katika kinywa chake kuelekea kwa mwanamke ili mafuriko yamchukue. 16 Lakini nchi ilimsaidia mwanamke. Nchi ilifungua kichwa chake na kumeza mto uliotoka kwenye kinywa cha joka. 17 Kisha joka lilimkasirikia sana mwanamke. Likaenda kufanya vita na watoto wake wengine. Watoto wa mwanamke ni wale wanaozitii amri za Mungu na wanayo kweli ambayo Yesu aliifundisha.
53 Yesu alipotoka humo, walimu wa sheria na Mafarisayo walianza kumpinga sana. Walianza kumjaribu ili awajibu maswali kuhusu mambo mengi, 54 ili Yesu akisema jambo isivyo sahihi waweze kupata sababu ya kumkosoa.
Msiwe Kama Mafarisayo
12 Maelfu wengi wa watu walikusanyika. Walikuwepo watu wengi sana kiasi ambacho walikuwa wakikanyagana. Kabla Yesu hajaanza kuzungumza na watu wale, aliwaambia wafuasi wake, “Iweni waangalifu dhidi ya chachu ya Mafarisayo. Ninamaanisha kuwa hao ni wanafiki. 2 Kila kitu kilichofichwa kitawekwa wazi, na kila kitu kilicho sirini kitajulikana. 3 Mnachokisema sirini kitasemwa mbele za watu. Na mliyonong'onezana katika vyumba vyenu, yatahubiriwa sehemu za wazi ambako kila mtu atasikia.”
Mwogopeni Mungu, Siyo Watu
(Mt 10:28-31)
4 Kisha Yesu akawaambia watu, “Ninawaambia ninyi, rafiki zangu, msiwaogope watu. Wanaweza kuua mwili, lakini baada ya hilo hawawezi kufanya chochote cha kuwaumiza. 5 Mwogopeni Mungu maana Yeye ndiye mwenye nguvu ya kuwaua na kuwatupa Jehanamu. Ndiyo, mnapaswa kumwogopa yeye.
6 Ndege wanapouzwa, ndege watano wadogo wanagharimu senti mbili tu za shaba. Lakini Mungu hasahau hata mmoja wao. 7 Ndiyo, Mungu anajua hata idadi ya nywele mlizonazo kwenye vichwa vyenu. Msiogope ninyi ni wa thamani kuliko ndege wengi.
Msiionee Haya Imani Yenu
(Mt 10:32-33; 12:32; 10:19-20)
8 Ninawaambia, mkinikiri mbele za watu, ndipo nami[a] nitakiri kuwa ninyi ni wangu mbele za Mungu na malaika. 9 Na atakayenikataa mimi mbele za watu, nami nitamkataa mbele za Mungu na malaika.
10 Kila asemaye neno kinyume na Mwana wa Adamu atasamehewa. Lakini atakayesema kinyume na Roho Mtakatifu hatasamehewa.
11 Watakapowapeleka ninyi katika masinagogi mbele ya viongozi na wenye mamlaka, msihangaike mtasema nini. 12 Roho Mtakatifu atawafundisha wakati huo huo mnachopaswa kusema.”
© 2017 Bible League International