Book of Common Prayer
37 Watu waliposikia hili wakahuzunika sana. Wakawauliza Petro na mitume wengine, “Ndugu zetu, tufanye nini?”
38 Petro akawaambia, “Geuzeni mioyo na maisha yenu na kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo. Ndipo Mungu atawasamehe dhambi zenu, na mtapokea zawadi ya Roho Mtakatifu. 39 Ahadi hii ni kwa ajili yenu ninyi, watoto wenu na vizazi vijavyo. Ni kwa kila mtu ambaye Bwana Mungu wetu anamwita kwake mwenyewe.”
40 Petro aliwaonya kwa maneno mengine mengi; aliwasihi, akawaambia, “Jiokoeni na uovu unaofanywa na watu wanaoishi sasa!” 41 Ndipo wale walioyakubali yale aliyosema Petro wakabatizwa. Yapata watu elfu tatu waliongezwa kwenye kundi la waamini siku ile.
Ushirika wa Waamini
42 Waamini walitumia muda wao kusikiliza mafundisho ya mitume. Walishirikiana kila kitu kwa pamoja. Walikula[a] na kuomba pamoja. 43 Maajabu mengi na ishara nyingi zilikuwa zinatokea kupitia mitume, na hivyo kila mtu aliingiwa na hofu na akamtukuza Mungu. 44 Waamini wote walikaa pamoja, na kushirikiana kila kitu. 45 Waliuza mashamba yao na vitu walivyomiliki, kisha wakatoa fedha na kuwapa wenye kuhitaji. 46 Waamini waliendelea kukutana pamoja katika eneo la Hekalu. Pia walikula pamoja katika nyumba zao. Walikuwa na furaha kushirikiana chakula chao na walikula kwa mioyo mikunjufu. 47 Waamini walimsifu Mungu na waliheshimiwa na watu wote. Watu wengi zaidi waliokolewa kila siku, na Bwana alikuwa akiwaongeza kwenye kundi lao.
Yesu ni Neno la Mungu la Milele
1 Mwanzoni Kabla ulimwengu haujaumbwa
alikuwepo Neno.[a]
Huyo Neno alikuwa pamoja na Mungu,
na Neno alikuwa Mungu.
2 Alikuwepo pamoja na Mungu
toka mwanzo.
3 Kila kitu kilifanyika kupitia kwake.
Hakuna chochote katika uumbaji wa Mungu
kilichofanyika bila yeye.
4 Ndani yake Neno kulikuwemo na uzima,
na uzima huo ulikuwa nuru
kwa ajili ya watu wa ulimwenguni.
5 Nuru[b] hiyo yamulika gizani,
na giza halikuishinda.[c]
6 Alikuwepo mtu aliyeitwa Yohana, aliyetumwa na Mungu. 7 Alikuja kuwaambia watu kuhusu nuru. Ili kupitia kwake watu wote waweze kusikia kuhusu yule aliye nuru na wamwamini. 8 Yohana mwenyewe hakuwa nuru. Lakini alikuja kuwaambia watu kuhusu nuru.
9 Nuru ya kweli,
anayeleta mwangaza kwa watu wote,
alikuwa tayari kuonekana kwa ulimwengu.
10 Huyo Neno alikuwapo tayari ulimwenguni.
Ulimwengu uliumbwa kupitia yeye,
lakini ulimwengu haukumkubali.
11 Alikuja kwa ulimwengu ulio wake,
na watu wake mwenyewe hawakumkubali.
12 Lakini baadhi ya watu walimkubali wakamwamini
na akawapa haki ya kuwa watoto wa Mungu.
13 Ndiyo, walikuwa watoto wa Mungu,
lakini si kwa kuzaliwa kimwili.
Haikuhusisha matamanio
ya kibinadamu.
Mungu mwenyewe aliwafanya
kuwa watoto wake.
14 Neno akafanyika kuwa mwanadamu
na akaishi pamoja nasi.
Tuliouna ukuu wa uungu wake;
utukufu alionao Mwana pekee wa Baba.
15 Yohana alizungumza kuhusu yeye alipopaza sauti na kusema, “Huyu ndiye niliyemzungumzia habari zake niliposema, ‘Anayekuja baada yangu ni mkuu kuliko mimi, kwa sababu alikuwepo mwanzoni, zamani kabla sijazaliwa.’”
16 Alikuwa amejaa neema na kweli ya Mungu,
tulipokea kutoka baraka moja
baada ya nyingine[d] kutoka kwake.
17 Hiyo ni kusema kuwa,
sheria ililetwa kwetu kupitia Musa.
Lakini neema na kweli imekuja
kupitia Yesu Kristo.
18 Hakuna aliyewahi kumwona Mungu
isipokuwa Mwana peke yake,
ambaye yeye mwenyewe ni Mungu,
ametuonesha jinsi Mungu alivyo.
Yuko karibu sana na Baba
kiasi kwamba tunapomwona,
tumemwona Mungu.
© 2017 Bible League International