Book of Common Prayer
9 Wenye uhai hawa wanne walikuwa wanampa utukufu, heshima na shukrani yule anayekaa kwenye kiti cha enzi, anayeishi milele na milele. Na kila wakati walifanya hivyo, 10 wazee ishirini na nne waliinama mbele ya[a] yule anayekaa kwenye kiti cha enzi. Wanamwabudu anayeishi milele na milele. Wanaweka taji zao mbele ya kiti cha enzi na kusema:
11 “Bwana wetu na Mungu!
Unastahili kupokea utukufu, heshima na nguvu.
Uliumba vitu vyote.
Kila kinachoishi kiliumbwa kwa sababu ulitaka.”
Nani anaweza kukifungua kitabu?
5 Kisha niliona kitabu[b] katika mkono wa kulia wa aliyekaa kwenye kiti cha enzi. Kitabu hiki kilikuwa na maandishi pande zote na kilikuwa kimefungwa kwa mihuri saba. 2 Na nikamwona malaika mwenye nguvu, aliyeita kwa sauti kubwa, “Ni nani anayestahili kuivunja mihuri na kukifungua kitabu?” 3 Lakini hakukuwa yeyote mbinguni au duniani au chini ya dunia ambaye angeweza kukifungua kitabu na kutazama ndani yake. 4 Nililia sana kwa sababu hakuwepo aliyestahili kukifungua kitabu na kuangalia ndani yake. 5 Lakini mmoja wa wazee akaniambia, “Usilie! Simba[c] kutoka kabila la Yuda ameshinda. Ni mzaliwa wa Daudi. Anaweza kukifungua kitabu na mihuri yake saba.”
Wanawali Kumi
25 Nyakati hizo, ufalme wa Mungu utafanana na wanawali kumi waliokwenda kusubiri kuwasili kwa bwana arusi wakiwa na taa zao. 2 Watano kati yao walikuwa na hekima, na watano walikuwa wajinga. 3 Wanawali wajinga walichukua taa zao bila ya kubeba mafuta ya ziada kwa ajili ya taa zao. 4 Wanawali wenye hekima walichukua taa zao pamoja na mafuta ya ziada kwa ajili ya taa zao katika chupa. 5 Bwana arusi alipochelewa sana, walichoka na wote wakasinzia.
6 Usiku wa manane ulipofika, ikatangazwa, ‘Bwana arusi anakuja! Njooni mumlaki!’
7 Wasichana wote waliamka. Wakatayarisha taa zao. 8 Lakini wanawali wajinga wakawaambia wanawali wenye hekima, ‘Tupeni mafuta kiasi kwa sababu mafuta katika taa zetu yamekwisha.’
9 Wanawali wenye hekima wakajibu, ‘Hapana! Mafuta tuliyonayo hayatatutosha sisi sote. Lakini nendeni kwa wauza mafuta mkanunue.’
10 Hivyo wanawali wajinga wakaenda kununua mafuta. Walipoondoka, bwana arusi akafika. Wanawali waliokuwa tayari wakaingia kwenye sherehe ya arusi pamoja na bwana arusi. Kisha mlango ukafungwa.
11 Baadaye wanawali waliokwenda kununua mafuta wakarudi. Wakasema, ‘bwana, bwana! Fungua mlango tuingie.’
12 Lakini bwana arusi akajibu, ‘Kwa hakika hapana! Wala siwajui ninyi.’
13 Hivyo iweni tayari kila wakati. Hamjui siku wala muda ambao Mwana wa Adamu atakuja.
© 2017 Bible League International