Revised Common Lectionary (Complementary)
13 Hivyo wenye karama ya kusema kwa lugha waombe ili waweze kufasiri yale wanayosema. 14 Ninapoomba kwa lugha zingine, roho yangu inaomba, lakini akili yangu haifanyi chochote. 15 Hivyo nifanye nini? Nitaomba kwa roho yangu, lakini pia nitaomba kwa akili yangu. Nitaimba kwa roho yangu, lakini pia nitaimba kwa akili yangu. 16 Unaweza ukawa unamshukuru Mungu kwa roho yako. Lakini mtu mwingine ambaye haielewi lugha unayotumia hawezi kusema “Amina” kwa maombi yako ya shukrani. 17 Unaweza ukawa unamshukuru Mungu katika njia nzuri, lakini isiwasaidie wengine kuwa imara.
18 Ninamshukuru Mungu kwamba nimepewa karama ya kusema lugha aina nyingi mbalimbali kuliko yeyote kati yenu. 19 Lakini wakati wa mikutano ya kanisa napenda kuzungumza maneno matano ninayoyaelewa kuliko maelfu ya maneno katika lugha zingine. Ni afadhali nizungumze nikiwa katika uelewa wangu ili niwafundishe wengine.
20 Ndugu zangu, msiwaze kama watoto wadogo. Iweni kama watoto wachanga katika mambo maovu, lakini katika kuwaza kwenu muwe kama watu wazima, waliokua. 21 Kama Maandiko[a] yanavyosema,
“Kwa kutumia wanaozungumza lugha tofauti
na kutumia midomo ya wageni,
nitazungumza na watu hawa,
hata hivyo, hawatanitii.”(A)
Hivi ndivyo Bwana anasema.
22 Na kutokana na hili tunaona kwamba matumizi ya lugha zingine ni ishara kuonesha namna ambavyo Mungu anawashughulikia wasioamini, na si walioamini. Na unabii unaonesha namna ambavyo Mungu hutenda kazi kupitia wanaoamini, na si wasioamini. 23 Chukulieni kuwa kanisa lote limekusanyika nanyi nyote mkaanza kusema kwa lugha zingine. Ikiwa baadhi ya watu wasio sehemu ya kundi lenu au wasio waamini wataingia katika kusanyiko lenu, watasema ninyi ni wendawazimu. 24 Lakini chukulieni kuwa ninyi nyote mnatabiri na mtu asiyeamini ama asiyekuwa sehemu ya kundi lenu akaingia. Dhambi zao zitawekwa wazi kwao, na watahukumiwa kwa kila kitu mtakachosema. 25 Mambo ya siri katika mioyo yao yatajulikana. Na watapiga magoti na kumwabudu Mungu. Watakiri na kusema, “Pasipo shaka, Mungu yuko hapa pamoja nanyi.”[b]
© 2017 Bible League International