Revised Common Lectionary (Semicontinuous)
9 Upendo wenu unapaswa kuwa halisi. Uchukieni uovu. Fanyeni yaliyo mema tu. 10 Pendaneni ninyi kwa ninyi kama wa familia moja. Na jitahidini kuwa wa kwanza katika kumpa heshima kila mmoja baina yenu. 11 Mnapoendelea kumtumikia Bwana, fanyeni kwa juhudi wala msiwe wavivu. Mchangamke juu ya utumishi wenu kwa Mungu.[a] 12 Mfurahi kwa sababu ya tumaini mlilonalo. Mvumilieni mnapokutana na mateso. Ombeni nyakati zote. 13 Washirikishe ulichonacho watu wa Mungu wanaohitaji msaada. Wakaribisheni katika nyumba zenu wale wanaosafiri au wanaohitaji msaada.
14 Watakieni mema wale wanaowafanyia mabaya. Mwombeni Mungu awabariki, na sio kuwalaani. 15 Furahini pamoja na wanaofurahi. Huzunikeni na wanaohuzunika. 16 Ishini kwa amani ninyi kwa ninyi. Msijivune, lakini iweni radhi kuwa rafiki wa wasio na umuhimu kwa wengine. Msijihesabu kuwa wenye akili kuliko wengine wote.
17 Mtu akikukosea, usimlipize ubaya. Mjaribu kufanya lile ambalo kila mtu anaona kuwa ni sahihi. 18 Mjitahidi kadri mwezavyo kuishi kwa amani na kila mtu. 19 Rafiki zangu, msijaribu kumwadhibu yeyote anayewakosea. Msubiri Mungu katika hasira yake awaadhibu. Katika Maandiko Bwana anasema, “Nitawaadhibu wao kwa ajili ya yale waliyofanya.”(A) 20 Badala yake,
“ikiwa una adui wenye njaa,
wapeni chakula wale.
Ikiwa wana kiu,
wapeni kinywaji wanywe.
Kwa kufanya hivyo mtawafanya wajisikie aibu.”[b](B)
21 Msiruhusu uovu uwashinde, bali ushindeni uovu kwa kutenda mema.
Yesu Asema ni Lazima Afe
(Mk 8:31-9:1; Lk 9:22-27)
21 Kuanzia wakati huo Yesu alianza kuwaambia wafuasi wake kuwa ni lazima aende Yerusalemu. Alifafanua kuwa Viongozi wazee wa Kiyahudi, viongozi wa makuhani na walimu wa sheria watamfanya apate mateso kwa mambo mengi. Na aliwaambia wafuasi wake kuwa lazima auawe. Na siku ya tatu atafufuka kutoka kwa wafu.
22 Petro akamchukua Yesu na kwenda naye faragha mbali na wafuasi wengine. Akaanza kumkosoa Yesu kwa akasema, “Mungu akuepushe mbali na mateso hayo, Bwana! Hilo halitakutokea!”
23 Ndipo Yesu akamwambia Petro, “Ondoka kwangu, Shetani![a] Hunisaidii! Hujali mambo ya Mungu. Unajali mambo ambayo wanadamu wanadhani ni ya muhimu.”
24 Kisha Yesu akawaambia wafuasi wake, “Ikiwa yeyote miongoni mwenu anataka kuwa mfuasi wangu, ni lazima aache kujiwazia yeye mwenyewe na mahitaji yake. Ni lazima awe radhi kuubeba msalaba aliopewa na kunifuata mimi. 25 Yeyote kati yenu anayetaka kuokoa uhai wake, ataupoteza. Lakini ninyi mlioyaacha maisha yenu kwa ajili yangu mtaupata uzima wa kweli. 26 Haina maana kwenu ninyi kuupata ulimwengu wote, ikiwa ninyi wenyewe mtapotea. Mtu atalipa nini ili kuyapata tena maisha yake baada ya kuyapoteza? 27 Mimi, Mwana wa Adamu, nitarudi katika utukufu wa Baba yangu pamoja na Malaika. Na nitamlipa kila mtu kutokana na matendo yake. 28 Niaminini ninaposema wapo watu waliopo hapa watakaoishi mpaka watakaponiona nikija kama Mwana wa Adamu kutawala kama mfalme.”
© 2017 Bible League International