M’Cheyne Bible Reading Plan
1 Salamu kutoka kwa Yuda, mtumwa wa Yesu Kristo na ndugu yake Yakobo. Kwa wale waliochaguliwa na kupendwa na Mungu Baba na kulindwa ndani ya Yesu Kristo.
2 Rehema, amani na upendo viwe pamoja nanyi zaidi na zaidi.
Mungu Atawaadhibu Watendao Mabaya
3 Rafiki wapendwa, nilitaka sana kuwaandikia kuhusu wokovu tunaoshiriki pamoja. Lakini nimejisikia kuwa ni muhimu niwaandikie kuhusu kitu kingine: Ninataka kuwatia moyo kuipigania kwa nguvu imani ambayo Mungu aliwapa watakatifu wake. Mungu alitoa imani hii mara moja na ni nzuri wakati wote. 4 Baadhi ya watu wamejiingiza kwa siri kwenye kundi lenu. Watu hawa wamekwisha kuhukumiwa kuwa wakosaji kwa sababu ya matendo yao. Zamani zilizopita manabii waliandika kuhusu watu hao. Wako kinyume na Mungu. Wameigeuza neema ya Mungu kujihalalishia kutenda chochote wanachotaka. Wanakataa kumtii Mkuu aliye peke yake, Bwana wetu Yesu Kristo.
5 Ninataka kuwasaidia mkumbuke baadhi ya vitu mnavyovifahamu tayari: Kumbukeni kwamba Bwana[a] aliwaokoa watu wake kwa kuwatoa katika nchi ya Misri. Lakini baadaye aliwaangamiza wale ambao hawakuamini. 6 Na kumbukeni malaika waliopoteza mamlaka yao ya kutawala. Waliacha mahali pao pa kuishi. Hivyo Bwana amewaweka gizani, wamefungwa kwa minyororo ya milele, mpaka watakapohukumiwa siku iliyo kuu. 7 Pia kumbukeni miji ya Sodoma na Gomora na miji mingine iliyoizunguka. Kama wale malaika, watu wa miji ile walikuwa na hatia ya dhambi ya uzinzi, hata wakataka kuzini na malaika. Na waliadhibiwa kwa moto wa milele. Miji hii ni mfano kwa waovu watakaoteseka kwa adhabu ya moto wa milele.
8 Ni sawasawa na watu hawa waliojiingiza kwenye kundi lenu. Wanaongozwa na ndoto, wanajichafua wenyewe kwa dhambi. Wanapuuza mamlaka ya Bwana na kusema mambo mabaya kinyume na walio watukufu.[b] 9 Hata malaika mkuu Mikaeli hakufanya hivi. Mikaeli alibishana na Ibilisi kuhusu nani angeuchukua mwili wa Musa. Lakini Mikaeli hakutamka hukumu kwa Ibilisi kwa mashitaka yake ya uongo. Badala yake, Mikaeli alisema, “Bwana mwenyewe akuadhibu!”
10 Lakini watu hawa hukashifu mambo wasiyoyaelewa. Wanaelewa baadhi ya mambo, isipokuwa wanayaelewa mambo haya si kwa kufikiri bali kwa kuhisi, kama wanyama wasiofikiri. Na haya ni mambo yanayowaangamiza. 11 Itakuwa vibaya kwao kwa kuwa wameifuata njia ambayo Kaini[c] aliitumia. Kwa kutafuta fedha, wamejiingiza katika kosa lile lile la Balaamu.[d] Wamepigana kinyume na Mungu kama alivyofanya Kora.[e] Na wataangamizwa vile vile kama Kora.
12 Watu hawa ni kama madoa machafu miongoni mwenu, wanawatia aibu mnapokutanika pamoja kuonesha upendo miongoni mwenu na kula chakula kwa pamoja kama kanisa. Pasipo kuwa na aibu wanakula pamoja nanyi. Wanajijali wao wenyewe tu. Wao ni kama mawingu yasiyo na mvua yanayosukumwa na upepo kila upande. Wako kama miti isiyo na matunda wakati wa mavuno ambayo hung'olewa kutoka ardhini. Hivyo wamekufa mara mbili. 13 Kama mapovu machafu juu ya mawimbi ya bahari, kila mtu anaweza kuona mambo ya aibu wanayoyafanya. Ni kama nyota zinazotangatanga angani. Nao wameandaliwa mahali penye giza kuu milele.
14 Henoko, mtu wa kizazi cha saba kutoka Adamu, alisema hivi kuhusu watu hawa: “Tazama! Bwana anakuja pamoja na maelfu ya malaika watakatifu. 15 Kumhukumu kila mmoja. Atawaadhibu wale wote walio kinyume naye kutokana na maovu waliyotenda kwa sababu ya kutokumheshimu. Ndiyo, Bwana atawaadhibu watenda dhambi wote hawa wasiomheshimu. Atawaadhibu kwa sababu ya mambo maovu waliyosema kinyume naye.”
16 Watu hawa daima hulalamika na kutafuta ubaya kwa wengine. Daima hutenda mambo maovu wanayotaka kufanya. Hujisifu wenyewe. Huwatendea vyema baadhi ya watu kuliko wengine ili wapate vitu wanavyovitaka.
Tahadhari na Mambo ya Kufanya
17 Rafiki wapendwa, kumbukeni mambo ambayo mitume wa Bwana Yesu Kristo walisema kuwa yatatokea. 18 Walisema, “Katika nyakati za mwisho kutakuwa watu wanaomcheka Mungu na kufanya yale wanayotaka kufanya tu, mambo ambayo ni kinyume na Mungu.” 19 Hawa ni watu wanaowagawa katika makundi. Si wa rohoni kwa sababu hawana Roho Mtakatifu.
20 Lakini ninyi, rafiki wapendwa, itumieni imani yenu takatifu zaidi kusaidiana ninyi kwa ninyi ili muwe imara zaidi katika imani. Ombeni kwa msaada wa Roho Mtakatifu. 21 Jiwekeni salama katika upendo wa Mungu, kadri mnavyomsubiri Bwana Yesu Kristo kuionesha rehema yake kwenu kwa kuwapa uzima wa milele.
22 Waonesheni rehema walio na mashaka. 23 Waokoeni wale wanaoishi katika hatari ya moto wa jehanamu. Muwatendee wengine kwa rehema, lakini muwe waangalifu kuwa maisha yao maovu yasichafue mwenendo wenu mwema.[f]
Msifuni Mungu
24 Mungu ana nguvu na anaweza kuwafanya msianguke. Anaweza kuwaingiza katika uwepo wa utukufu wake bila makosa yoyote ndani yenu na akawapa furaha kuu. 25 Ni Mungu peke yake, aliye Mwokozi wetu. Kwake uwepo utukufu, ukuu, nguvu na mamlaka kupitia Yesu Kristo kwa wakati uliopita, uliopo na milele. Amina.
Gavana Pilato Amhoji Yesu
(Mt 27:1-2,11-14; Mk 15:1-5; Yh 18:28-38)
23 Kisha kundi lote likasimama, wakampeleka Yesu kwa Pilato. 2 Wakaanza kumshitaki Yesu na kumwambia Pilato, “Tumemkamata mtu huyu akijaribu kuwapotosha watu wetu. Anasema tusilipe kodi kwa Kaisari. Anajiita Masihi, mfalme.”
3 Pilato akamwuliza Yesu, “Wewe ni mfalme wa Wayahudi?”
Yesu akajibu, “Ndiyo, unaweza kusema hivyo.”
4 Pilato akawaambia wakuu wa makuhani na watu, “Sioni kosa lolote kwa mtu huyu.”
5 Lakini waliendelea kusema, “Mafundisho yake yanasababisha matatizo katika Uyahudi yote. Alianzia Galilaya na sasa yupo hapa!”
Pilato Ampeleka Yesu Kwa Herode
6 Pilato aliposikia hili, akauliza, “Mtu huyu anatoka Galilaya?” 7 Akatambua kuwa Yesu yuko chini ya mamlaka ya Herode. Siku hizo Herode alikuwa Yerusalemu, hivyo Pilato alimpeleka Yesu kwake.
8 Herode alipomwona Yesu alifurahi sana. Alikuwa akisikia habari zake na kwa muda mrefu alikuwa anataka kukutana na Yesu. Herode alitaka kuona muujiza, hivyo alitegemea kwamba Yesu angefanya muujiza mmoja. 9 Akamwuliza Yesu maswali mengi, lakini Yesu hakusema chochote. 10 Viongozi wa makuhani na walimu wa sheria walikuwa wamesimama pale wakipaza sauti zao wakimshitaki kwa Herode. 11 Ndipo Herode na askari wake wakamcheka. Wakamfanyia mzaha kwa kumvalisha mavazi kama ambayo wafalme huvaa. Kisha Herode akamrudisha Yesu kwa Pilato. 12 Nyakati za nyuma Pilato na Herode walikuwa maadui daima. Kuanzia siku ile wakawa marafiki.
Pilato Ajaribu Kumwachia Huru Yesu
(Mt 27:15-26; Mk 15:6-15; Yh 18:39-19:16)
13 Pilato aliwaita viongozi wa makuhani, viongozi wa Kiyahudi na watu wote pamoja. 14 Akawaambia, “Mlimleta mtu huyu kwangu. Mlisema alikuwa anawapotosha watu. Lakini nimemchunguza mbele yenu nyote na sijaona hatia juu ya kitu chochote mnachomshitakia. 15 Hata Herode hakumwona kuwa ana hatia yo yote. Akamrudisha kwetu. Tazameni, hajafanya jambo lolote baya linalostahili adhabu ya kifo. 16 Kwa hiyo, baada ya kumwadhibu kidogo nitamwacha aende zake.” 17 [a]
18 Lakini wote walipaza sauti zao pamoja, “Mwue! Mwachie huru Baraba!” 19 (Baraba alifungwa gerezani kwa sababu ya kuanzisha fujo mjini na kwa mauaji.)
20 Pilato alitaka amwachie huru Yesu. Hivyo Pilato akawaambia atamwachilia. 21 Lakini walipaza sauti tena wakisema, “Mwue, Mwue msalabani!”
22 Mara ya tatu Pilato akawaambia watu, “Kwa nini? Amefanya kosa gani? Hana hatia. Sioni sababu ya kumwua. Hivyo nitamwachia huru baada ya kumwadhibu kidogo.”
23 Lakini watu waliendelea kupaza sauti. Walidai Yesu auawe msalabani. Kelele zao zikawa kubwa kiasi kwamba 24 Pilato aliamua kuwapa kile walichotaka. 25 Walitaka Baraba aliyekuwa gerezani kwa sababu ya kuanzisha fujo na mauaji aachiwe huru. Pilato akamwachia Baraba. Na kumtoa Yesu ili auawe. Hili ndilo watu walitaka.
Yesu Awambwa Msalabani
(Mt 27:32-44; Mk 15:21-32; Yh 19:17-27)
26 Askari wakamwongoza Yesu kumtoa nje ya mji. Wakati huo huo mtu mmoja kutoka Kirene alikuwa anaingia mjini kutoka maeneo nje ya Yerusalemu. Askari wakamlazimisha kuubeba msalaba wa Yesu na kumfuata Yesu kwa nyuma.
27 Kundi kubwa wakamfuata Yesu. Baadhi ya wanawake waliokuwemo kwenye kundi walilia na kuomboleza. Walimwonea huruma. 28 Lakini Yesu aligeuka na kuwaambia, “Wanawake wa Yerusalemu, msinililie. Jililieni ninyi wenyewe na watoto wenu. 29 Wakati unakuja ambapo watu watasema, ‘Wanawake wasioweza kuwa na watoto ndio ambao Mungu amewabariki. Hakika ni baraka kwamba hawana watoto wa kutunza.’ 30 Watu wataiambia milima, ‘Tuangukieni!’ Wataviambia vilima, ‘Tufunikeni!’(A) 31 Kama hili linaweza kutokea kwa mtu aliye mwema, nini kitatokea kwa wenye hatia?”
32 Walikuwepo pia wahalifu wawili waliotolewa nje ya mji pamoja na Yesu ili wauawe. 33 Walipelekwa mahali palipoitwa “Fuvu la Kichwa.” Askari walimpigilia Yesu msalabani pale. Waliwapigilia misalabani wahalifu pia, mmoja aliwekwa upande wa kulia na mwingine kushoto kwa Yesu.
34 Na Yesu alikuwa anasema, “Baba uwasamehe watu hawa, kwa sababu hawajui wanalofanya.”
Askari waligawana nguo zake kwa kutumia kamari. 35 Watu walisimama pale wakiangalia kila kitu kilichokuwa kinatokea. Viongozi wa Kiyahudi walimcheka Yesu. Walisema, “Kama kweli yeye ni Masihi, Mfalme Mteule wa Mungu, basi ajiokoe. Je, hakuwaokoa wengine?”
36 Hata askari walimcheka Yesu na kumfanyia mizaha. Walikuja na kumpa siki ya mvinyo. 37 Wakasema, “Ikiwa wewe ni mfalme wa Wayahudi, jiokoe mwenyewe!” 38 Waliandika maneno haya kwenye kibao msalabani juu ya kichwa chake: “Huyu ni Mfalme wa Wayahudi”.
39 Mmoja wa wahalifu aliyekuwa ananing'inia pale akaanza kumtukana Yesu: “Wewe siye Masihi? Basi jiokoe na utuokoe sisi pia!”
40 Lakini mhalifu mwingine alimnyamazisha asiendelee kumtukana Yesu. Akasema, “Unapaswa kumwogopa Mungu. Sisi sote tutakufa muda si mrefu. 41 Wewe na mimi tuna hatia, tunastahili kufa kwa sababu tulitenda mabaya. Lakini mtu huyu hajafanya chochote kibaya.” 42 Kisha akamwambia Yesu, “Unikumbuke utakapoanza kutawala kama mfalme!”
43 Yesu akamwambia, “Ninakwambia kwa uhakika, leo utakuwa pamoja nami Paradiso.”
Yesu Afariki
(Mt 27:45-56; Mk 15:33-41; Yh 19:28-30)
44 Ilikuwa yapata saa sita mchana, lakini kulibadilika kukawa giza mpaka saa tisa alasiri, 45 kwa sababu jua liliacha kung'aa. Pazia ndani ya Hekalu lilichanika vipande viwili. 46 Yesu alipaza sauti akasema, “Baba, ninaiweka roho yangu mikononi mwako!”(B) Baada ya Yesu kusema haya, akafa.
47 Mkuu wa askari wa Kirumi aliyekuwa pale alipoona yaliyotokea, alimsifu Mungu, akisema, “Ninajua mtu huyu alikuwa mtu mwema!”
48 Watu wengi walikuwa wametoka mjini kuja kuona tukio hili. Walipoona, wakahuzunika, wakaondoka wakiwa wanapiga vifua vyao. 49 Watu waliokuwa marafiki wa karibu wa Yesu walikuwepo pale. Pia, walikuwepo baadhi ya wanawake waliomfuata Yesu kutoka Galilaya. Walisimama mbali kutoka msalabani, waliyaona mambo haya.
Yesu Azikwa
(Mt 27:57-61; Mk 15:42-47; Yh 19:38-42)
50-51 Mtu mmoja aliyeitwa Yusufu kutoka mji wa Uyahudi ulioitwa Arimathaya alikuwapo pale. Alikuwa mtu mwema, aliyeishi namna Mungu alivyotaka. Alikuwa anausubiri ufalme wa Mungu uje. Yusufu alikuwa mjumbe wa baraza la Kiyahudi. Lakini hakukubali pale viongozi wengine wa Kiyahudi walipoamua kumwua Yesu. 52 Alikwenda kwa Pilato na kumwomba mwili wa Yesu. 53 Aliushusha mwili kutoka msalabani na kuufunga kwenye nguo. Kisha akauweka ndani ya kaburi lililochimbwa katika ukuta wa mwamba. Kaburi hili lilikuwa halijatumika bado. 54 Ilikuwa jioni Siku ya Maandalizi ya Sabato. Sabato ilikuwa ianze baada ya jua kuzama.
55 Wanawake waliotoka Galilaya pamoja na Yesu walimfuata Yusufu. Wakaliona kaburi. Ndani yake wakaona mahali alipouweka mwili wa Yesu. 56 Kisha wakaenda kuandaa manukato yanayonukia vizuri ili kuupaka mwili wa Yesu.
Siku ya Sabato walipumzika, kama ilivyoamriwa katika Sheria ya Musa.
© 2017 Bible League International