Beginning
Kuzaliwa kwa Yesu
(Mt 1:18-25)
2 Ulikuwa wakati ambapo amri ilitolewa na Kaisari Augusto kwamba watu wote wanaoishi katika utawala wote wa Rumi[a] wahesabiwe na kuorodheshwa[b] katika kumbukumbu za serikali. 2 Orodha hii ilikuwa ya kwanza tangu Kirenio alipokuwa gavana wa Shamu. 3 Kila mtu alikwenda katika mji aliozaliwa ili akahesabiwe na kuingizwa katika orodha hiyo.
4 Hivyo Yusufu alitoka Nazareti, mji uliokuwa katika jimbo la Galilaya na kwenda katika mji wa Bethlehemu uliokuwa katika jimbo la Uyahudi. Pia, mji huu ulijulikana kama mji wa Daudi. Yusufu alikwenda Bethlehemu kwa sababu alikuwa mzaliwa wa ukoo wa Daudi. 5 Yusufu alijiandikisha akiwa pamoja na Mariamu kwani alikuwa tayari amemchumbia ili amwoe. Na Mariamu alikuwa mjamzito. 6 Yusufu na Mariamu walipokuwa Bethlehemu, wakati wa Mariamu kujifungua ulifika. 7 Akamzaa mwanawe wa kwanza. Akamvingirishia nguo vizuri, kisha akamlaza katika hori la kulishia mifugo.[c] Walimweka humo kwa sababu chumba cha wageni kilikuwa kimejaa.
Wachungaji wa Mifugo Wajulishwa Kuhusu Yesu
8 Usiku ule, baadhi ya wachungaji walikuwa mashambani nje ya mji wa Bethlehemu wakilinda kondoo zao. 9 Malaika wa Bwana akawatokea ghafla, na utukufu wa Bwana ukaangaza kuwazunguka, wakaogopa sana. 10 Malaika akawaambia, “Msiogope, kwa kuwa nimewaletea habari njema zitakazowafurahisha watu wa Mungu wote. 11 Kwa sababu leo katika mji wa Daudi amezaliwa Mwokozi, ndiye Kristo,[d] Bwana. 12 Na hivi ndivyo mtakavyomtambua: Mtamkuta mtoto mchanga amevingirishiwa nguo na amelala katika hori la kulishia mifugo.”
13 Kisha malaika pamoja na jeshi kubwa la mbinguni wakaanza kumsifu Mungu, wakisema:
14 “Atukuzwe Mungu juu mbinguni,
na amani iwepo duniani
kwa watu wote wanaompendeza.”
15 Malaika walipoondoka kurudi mbinguni, wale wachungaji wakaambiana wakisema, “Twendeni Bethlehemu, tukalione jambo hili lililotokea, ambalo Bwana ametujulisha.”
16 Wakaenda haraka, wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala katika hori la kulishia mifugo. 17 Wachungaji walipomwona huyo mtoto, walisimulia kile walichoambiwa na malaika kuhusu mtoto. 18 Kila aliyesikia maelezo ya wachungaji, alishangaa. 19 Mariamu aliendelea kuyatafakari mambo haya, na kuyaweka moyoni. 20 Wachungaji waliirudia mifugo yao, wakawa wanamsifu na kumshukuru Mungu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona. Ilikuwa kama walivyoambiwa na malaika.
21 Ilipofika siku ya nane mtoto alitahiriwa, akaitwa Yesu. Hili ndilo jina alilopewa na malaika kabla mama yake hajaibeba mimba yake.
Yesu Atambulishwa Hekaluni
22 Muda wa kutakaswa ulimalizika, kama ilivyotakiwa na Sheria ya Musa baada ya mtoto kuzaliwa.[e] Baada ya hapo walimpeleka Yesu Yerusalemu na kumweka mbele za Bwana. 23 Kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana: Mzaliwa wa kwanza akiwa mtoto wa kiume, atolewe wakfu kwa ajili ya Bwana.[f] 24 Pia Mariamu na Yusufu walikwenda Yerusalemu kutoa dhabihu kama Sheria ya Bwana inavyosema kuwa, “Ni lazima utoe dhabihu ya jozi moja ya hua[g] au makinda mawili wa njiwa.”
Simeoni Amwona Yesu
25 Alikuwepo mtu mmoja aliyeishi katika mji wa Yerusalemu, mtu huyu aliitwa Simeoni. Alikuwa mtu mwema na mcha Mungu na Roho Mtakatifu alikuwa pamoja naye. Alikuwa akiusubiri wakati ambao Mungu angeisaidia Israeli. 26 Roho Mtakatifu alimwambia kwamba asingekufa kabla ya kumwona Masihi kutoka kwa Bwana. 27 Roho Mtakatifu alimwongoza mpaka Hekaluni. Hivyo, alikuwemo Hekaluni wakati Mariamu na Yusufu walipomleta mtoto Yesu ili wamfanyie kama ilivyotakiwa katika Sheria ya Kiyahudi. 28 Simeoni alimbeba mtoto Yesu mikononi mwake, akamshukuru Mungu na kusema,
29 “Sasa, Bwana, niruhusu mimi mtumishi wako nife kwa amani
kwa kuwa umeitimiza ahadi yako kwangu.
30 Nimeona kwa macho yangu namna utakavyowaokoa watu wako.
31 Sasa watu wote wanaweza kuuona mpango wako.
32 Yeye ni mwanga wa kuionesha njia yako kwa mataifa mengine,
na atawaletea heshima watu wako Israeli.”
33 Mariamu na Yusufu walishangazwa sana na maneno aliyosema Simeoni kuhusu Yesu. 34 Kisha Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu; “Wayahudi wengi wataanguka na wengi watainuka kwa sababu ya mtoto huyu. Atakuwa ishara kutoka kwa Mungu, lakini baadhi ya watu watamkataa. 35 Mawazo ya siri ya watu wengi yatajulikana. Na mambo yatakayotokea yatakuumiza, kama upanga unaokuchoma moyoni.”
Ana Amwona Yesu
36 Alikuwapo nabii aliyeitwa Ana binti Fanueli, kutoka katika kabila la Asheri. Alikuwa mwanamke mzee sana. Aliishi na mume wake kwa miaka saba, 37 kabla ya mume wake kufa na kumwacha peke yake. Na sasa alikuwa na umri wa miaka themanini na nne. Ana alikuwa Hekaluni daima, hakutoka. Alimwabudu Mungu kwa kufunga na kuomba usiku na mchana.
38 Simeoni alipokuwa anazungumza na Yusufu na Mariamu, Ana alikwenda walipokuwa na akaanza kumsifu Mungu na kuwaambia kuhusu Yesu watu wote waliokuwa wanasubiri Mungu kuikomboa Yerusalemu.
Yusufu, Mariamu na Yesu Warudi Nyumbani
39 Yusufu na Mariamu walipotimiza mambo yote yanayotakiwa katika sheria ya Bwana, walirudi Galilaya, katika mji wao wa Nazareti. 40 Mtoto Yesu aliendelea kukua na kuwa kijana mwenye nguvu na aliyejaa hekima nyingi. Na Mungu alikuwa anambariki.
Yesu Akiwa Mvulana
41 Kila mwaka wazazi wa Yesu walikwenda Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu ya Pasaka. 42 Yesu alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili, walikwenda kwenye sikukuu kama ilivyokuwa desturi ya Kiyahudi. 43 Sikukuu ilipokwisha, walirudi nyumbani, lakini Yesu alibaki Yerusalemu bila wazazi wake kutambua. 44 Walianza kumtafuta kwa jamaa na rafiki zao baada ya kusafiri kutwa nzima, wakidhani kuwa alikuwa pamoja nao katika msafara. 45 Walipomkosa, walirudi Yerusalemu kumtafuta.
46 Ikawa baada ya siku tatu wakamkuta Hekaluni, amekaa katikati ya walimu wa dini, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47 Na wote waliomsikiliza walishangazwa sana kwa ufahamu wake na majibu yake ya busara. 48 Wazazi wake walipomwona walishangaa pia, ndipo mama yake akamwambia, “Mwanangu, kwa nini umefanya hivi? Mimi na baba yako tulikuwa na wasiwasi sana, na tumekuwa tukikutafuta.”
49 Yesu akawaambia, “Kwa nini mlikuwa mnanitafuta? Mnapaswa kujua kuwa inanilazimu kuwemo nyumbani mwa Baba yangu?” 50 Lakini wao hawakuelewa alichowaambia.
51 Yesu alirudi pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii. Mama yake aliendelea kuyaweka mambo haya yote moyoni mwake. 52 Naye Yesu akakua katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.
Yohana Atayarisha Njia kwa Ajili ya Yesu
(Mt 3:1-12; Mk 1:1-8; Yh 1:19-28)
3 Katika mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Kaisari Tiberio, ambapo:
Pontio Pilato alikuwa gavana wa Uyahudi;
Herode alikuwa mtawala wa Galilaya;
Filipo ndugu yake Herode alikuwa mtawala wa Iturea na Trakoniti;
na Lisania, alikuwa mtawala wa Abilene.
2 Anasi na Kayafa walikuwa makuhani wakuu. Katika kipindi hiki, Yohana, mwana wa Zakaria, alikuwa akiishi jangwani na alipata ujumbe kutoka kwa Mungu. 3 Alipita katika maeneo yote yaliyo karibu na Mto Yordani akiwahubiri watu ujumbe kutoka kwa Mungu. Aliwaambia wabatizwe kuonesha kuwa wamekubali kubadili maisha yao ndipo dhambi zao zitasamehewa. 4 Hii ni kama maneno yaliyoandikwa katika kitabu cha nabii Isaya, yanayosema,
“Kuna mtu anayeipaza sauti yake kutokea nyikani:
‘Tayarisheni njia kwa ajili ya Bwana;
nyoosheni njia kwa ajili yake.
5 Kila bonde litajazwa,
na kila mlima na kilima vitasawazishwa.
Barabara zilizopinda zitanyooshwa,
na barabara zenye mashimo zitasawazishwa.
6 Na kila mtu ataona
jinsi Mungu atakavyowaokoa watu wake.’”(A)
7 Makundi ya watu walimwendea Yohana ili awabatize. Lakini aliwaambia, “Enyi nyoka! Ni nani aliyewaonya kuikimbia hukumu ya Mungu inayokuja? 8 Badilisheni mioyo yenu! Kisha onesheni ya kuwa mmebadilika kwa namna mnavyoishi. Ninajua mtasema kuwa, ‘Ibrahimu ni baba yetu.’ Hilo halijalishi chochote. Ninawaambia Mungu anaweza kumwumbia Ibrahimu watoto kutokana na mawe haya! 9 Na sasa shoka liko tayari kukata miti,[h] kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.”
10 Watu wakamwuliza Yohana, “Tufanye nini?”
11 Akajibu, “Ukiwa na mashati mawili mpe moja asiyekuwa na shati. Kama una chakula, kigawe pia.”
12 Hata watoza ushuru walikuja kwa Yohana. Walitaka wabatizwe. Walimwambia, “Mwalimu, tufanye nini sisi?”
13 Akawaambia, “Msitoze ushuru zaidi kuliko kiwango kilichoamriwa.”
14 Askari wakamwuliza, “Vipi kuhusu sisi? Tufanye nini?”
Akawaambia, “Msitumie nguvu au kutengeneza mashtaka ya uongo ili watu wawape pesa. Mtosheke na mishahara mnayopata.”
15 Kila mtu alitarajia kuja kwa Masihi,[i] na walijiuliza wakisema, “Labda Yohana ndiye Masihi.”
16 Yohana aliwajibu watu wote, akasema, “Ninawabatiza ninyi katika maji, lakini yupo mwingine ajaye baada yangu, mwenye nguvu zaidi kuliko mimi, huyo atafanya mengi zaidi yangu. Nami niliye mtumwa wa chini kabisa sistahili hata kuinama na kufungua kamba za viatu vyake. Yeye huyo atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto. 17 Yuko tayari sasa kuja kusafisha nafaka. Atatenganisha nafaka nzuri na makapi, na kuiweka katika ghala yake kisha ataichoma ile isiyofaa katika moto usiozimika.” 18 Hivi ndivyo ambavyo Yohana aliwahubiri watu Habari Njema. Aliwaonya sana kuwa wanatakiwa kubadili njia zao.
Kazi ya Yohana Ilivyomalizika Baadaye
19 Yohana alimkosoa Herode kwa sababu ya mambo mabaya aliyokuwa ameyafanya na Herodia, mkewe kaka yake Herode, na pia kwa mambo mengine mabaya aliyokuwa ameyafanya. 20 Hivyo Herode aliongeza jambo jingine baya katika matendo yake maovu. Alimfunga Yohana gerezani.
Yohana Ambatiza Yesu
(Mt 3:13-17; Mk 1:9-11)
21 Watu wote walipokuwa wakibatizwa, Yesu alikuja naye akabatizwa. Na alipokuwa akiomba, mbingu zilifunguka, 22 na Roho Mtakatifu aliyekuwa katika umbo la njiwa akashuka juu yake. Sauti ikasikika toka mbinguni, “Wewe ni mwanangu, ninayekupenda, napendezwa nawe sana.”
Ukoo wa Yesu
(Mt 1:1-17)
23 Yesu alipoanza kufundisha, alikuwa na umri kama wa miaka thelathini. Watu walidhani kuwa Yesu alikuwa Mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Eli.
24 Eli alikuwa mwana wa Mathati.
Mathati alikuwa mwana wa Lawi.
Lawi alikuwa mwana wa Melki.
Melki alikuwa mwana wa Yana.
Yana alikuwa mwana wa Yusufu.
25 Yusufu alikuwa mwana wa Matathia.
Matathia alikuwa mwana wa Amosi.
Amosi alikuwa mwana wa Nahumu.
Nahumu alikuwa mwana wa Esli.
Esli alikuwa mwana wa Nagai.
26 Nagai alikuwa mwana wa Maathi.
Maathi alikuwa mwana wa Matathia.
Matathia alikuwa mwana wa Semei.
Semei alikuwa mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Yoda.
27 Yoda alikuwa mwana wa Yoana.
Yoana alikuwa mwana wa Resa.
Resa alikuwa mwana wa Zerubabeli.
Zerubabeli alikuwa mwana wa Shealtieli.
Shealtieli alikuwa mwana wa Neri.
28 Neri alikuwa mwana wa Melki.
Melki alikuwa mwana wa Adi.
Adi alikuwa mwana wa Kosamu.
Kosamu alikuwa mwana wa Elmadamu,
Elmadamu alikuwa mwana wa Eri.
29 Eri alikuwa mwana wa Yoshua.
Yoshua alikuwa mwana wa Eliezeri.
Eliezeri alikuwa mwana wa Yorimu.
Yorimu alikuwa mwana wa Mathati.
Mathati alikuwa mwana wa Lawi.
30 Lawi alikuwa mwana wa Simeoni.
Simeoni alikuwa mwana wa Yuda.
Yuda alikuwa mwana wa Yusufu.
Yusufu alikuwa mwana wa Yonamu.
Yonamu alikuwa mwana wa Eliakimu.
31 Eliakimu alikuwa mwana wa Melea.
Melea alikuwa mwana wa Mena.
Mena alikuwa mwana wa Matatha.
Matatha alikuwa mwana wa Nathani.
Nathani alikuwa mwana wa Daudi.
32 Daudi alikuwa mwana wa Yese.
Yese alikuwa mwana wa Obedi.
Obedi alikuwa mwana wa Boazi.
Boazi alikuwa mwana wa Salmoni.[j]
Salmoni alikuwa mwana wa Nashoni.
33 Nashoni alikuwa mwana wa Aminadabu.
Aminadabu alikuwa mwana wa Admini,
Admini alikuwa mwana wa Aramu.[k]
Aramu alikuwa mwana wa Hesroni.
Hesroni alikuwa mwana wa Peresi.
Peresi alikuwa mwana wa Yuda.
34 Yuda alikuwa mwana wa Yakobo.
Yakobo alikuwa mwana wa Isaka.
Isaka alikuwa mwana wa Ibrahimu.
Ibrahimu alikuwa mwana wa Tera.
Tera alikuwa mwana wa Nahori.
35 Nahori alikuwa mwana wa Serugi,
Serugi alikuwa mwana wa Ragau.
Ragau alikuwa mwana wa Pelegi.
Pelegi alikuwa mwana wa Eberi,
Eberi alikuwa mwana wa Sala.
36 Sala alikuwa mwana wa Kenani.
Kenani alikuwa mwana wa Arfaksadi.
Arfaksadi alikuwa mwana wa Shemu.
Shemu alikuwa mwana wa Nuhu.
Nuhu alikuwa mwana wa Lameki.
37 Lameki alikuwa mwana wa Methusela.
Methusela alikuwa mwana wa Henoko.
Henoko alikuwa mwana wa Yaredi.
Yaredi alikuwa mwana wa Mahalaleli.
Mahalaleli alikuwa mwana wa Kenani.
38 Kenani alikuwa mwana wa Enoshi.
Enoshi alikuwa mwana wa Sethi.
Sethi alikuwa mwana wa Adamu.
Adamu alikuwa mwana wa Mungu.
© 2017 Bible League International