Add parallel Print Page Options

Yesu Amefufuka Kutoka Mauti

(Mt 28:1-8; Lk 24:1-12; Yh 20:1-10)

16 Sabato ilipomalizika, Mariamu Magdalena, Maria mama yake Yakobo, na Salome wakanunua manukato yenye harufu nzuri ili kuyapaka kwenye mwili wa Yesu. Alfajiri na mapema Jumapili, mara tu baada ya jua kuchomoza, walienda kwenye kaburi la Yesu. Nao walikuwa wakiambiana wao kwa wao, ni nani atakayelivingirisha jiwe litoke katika mlango wa kaburi kwa ajili yetu?

Kisha wakatazama juu na wakaona kuwa jiwe lile kubwa lilikuwa limevingirishwa tayari litoke mlangoni mwa kaburi la Yesu. Walipoingia kaburini, wakamwona kijana mmoja ameketi upande wa kulia naye alikuwa amevaa vazi jeupe, nao wakastaajabu.

Naye akamwambia, “Usistaajabu. Unamtafuta Yesu wa Nazareti, aliyesulubiwa? Tazama amefufuka! Hayupo hapa. Angalieni mahali walipokuwa wameweka mwili wake. Hata hivyo nendeni na kuwaeleza wafuasi wake pamoja na Petro kwamba: ‘Ametangulia mbele yenu kuelekea Galilaya. Mtamkuta kule, kama alivyowaambia.’”

Kwa hiyo wale wanawake walitoka na kukimbia kutoka kaburini, kwa sababu hofu na mshangao ulikuwa umewajia. Nao hawakusema chochote kwa mtu yeyote kwani waliogopa.[a]

Read full chapter

Footnotes

  1. 16:8 Kitabu kinaishia hapa katika nakala mbili za zamani za Kiyunani zilizopatikana. Nakala chache nyingine za baadaye zina mwisho huu mfupi: “Lakini mara wakampa maagizo yote Petro na wale waliokuwa pamoja naye. Kisha Yesu mwenyewe akawatuma watoke na kwenda mashariki na magharibi wakiwa na ujumbe mtakatifu ambao kamwe hautabadilika; kwamba watu wataokolewa milele.”