Revised Common Lectionary (Semicontinuous)
Yesu ni Neno la Mungu la Milele
1 Mwanzoni Kabla ulimwengu haujaumbwa
alikuwepo Neno.[a]
Huyo Neno alikuwa pamoja na Mungu,
na Neno alikuwa Mungu.
2 Alikuwepo pamoja na Mungu
toka mwanzo.
3 Kila kitu kilifanyika kupitia kwake.
Hakuna chochote katika uumbaji wa Mungu
kilichofanyika bila yeye.
4 Ndani yake Neno kulikuwemo na uzima,
na uzima huo ulikuwa nuru
kwa ajili ya watu wa ulimwenguni.
5 Nuru[b] hiyo yamulika gizani,
na giza halikuishinda.[c]
6 Alikuwepo mtu aliyeitwa Yohana, aliyetumwa na Mungu. 7 Alikuja kuwaambia watu kuhusu nuru. Ili kupitia kwake watu wote waweze kusikia kuhusu yule aliye nuru na wamwamini. 8 Yohana mwenyewe hakuwa nuru. Lakini alikuja kuwaambia watu kuhusu nuru.
9 Nuru ya kweli,
anayeleta mwangaza kwa watu wote,
alikuwa tayari kuonekana kwa ulimwengu.
10 Huyo Neno alikuwapo tayari ulimwenguni.
Ulimwengu uliumbwa kupitia yeye,
lakini ulimwengu haukumkubali.
11 Alikuja kwa ulimwengu ulio wake,
na watu wake mwenyewe hawakumkubali.
12 Lakini baadhi ya watu walimkubali wakamwamini
na akawapa haki ya kuwa watoto wa Mungu.
13 Ndiyo, walikuwa watoto wa Mungu,
lakini si kwa kuzaliwa kimwili.
Haikuhusisha matamanio
ya kibinadamu.
Mungu mwenyewe aliwafanya
kuwa watoto wake.
14 Neno akafanyika kuwa mwanadamu
na akaishi pamoja nasi.
Tuliouna ukuu wa uungu wake;
utukufu alionao Mwana pekee wa Baba.
15 Yohana alizungumza kuhusu yeye alipopaza sauti na kusema, “Huyu ndiye niliyemzungumzia habari zake niliposema, ‘Anayekuja baada yangu ni mkuu kuliko mimi, kwa sababu alikuwepo mwanzoni, zamani kabla sijazaliwa.’”
16 Alikuwa amejaa neema na kweli ya Mungu,
tulipokea kutoka baraka moja
baada ya nyingine[a] kutoka kwake.
17 Hiyo ni kusema kuwa,
sheria ililetwa kwetu kupitia Musa.
Lakini neema na kweli imekuja
kupitia Yesu Kristo.
18 Hakuna aliyewahi kumwona Mungu
isipokuwa Mwana peke yake,
ambaye yeye mwenyewe ni Mungu,
ametuonesha jinsi Mungu alivyo.
Yuko karibu sana na Baba
kiasi kwamba tunapomwona,
tumemwona Mungu.
© 2017 Bible League International