Revised Common Lectionary (Semicontinuous)
3 Neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana wetu Yesu Kristo iwe pamoja nanyi.
Paulo Amshukuru Mungu
4 Ninamshukuru Mungu daima kwa sababu ya neema aliyowapa katika Kristo Yesu. 5 Ambaye kwa njia yake Mungu amewabariki sana kwa namna mbalimbali hata miongoni mwenu wapo watu wenye vipawa vya kuzungumza na wengine wana vipawa vya maarifa! 6 Hii ni kwa sababu yale tuliyowaambia kuhusu Kristo yamedhihirika kuwa kweli katikati yenu. 7 Na sasa mna karama zote mnapomsubiri Mungu audhihirishie ulimwengu jinsi Bwana wetu Yesu Kristo alivyo wa ajabu. 8 Ataendelea kuwatia nguvu na hakuna atakayeweza kuwashtaki mpaka siku ya mwisho Bwana wetu Yesu atakaporudi. 9 Mungu ni mwaminifu. Na ndiye aliyewachagua ninyi ili mshiriki uzima pamoja na Mwanaye, Yesu Kristo Bwana wetu.
Yesu Atakaporudi Tena
(Mt 24:29-51; Lk 21:25-36; 19:12-13,40)
24 Lakini katika siku hizo, baada ya kipindi cha dhiki,
‘Jua litatiwa giza,
mwezi hautatoa mwanga,
25 nyota zitaanguka kutoka angani,
na mbingu yote itatikisika.’[a]
26 Ndipo watu watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni pamoja na nguvu kubwa na utukufu. 27 Baada ya hapo Mwana wa Adamu atawatuma malaika, na atawakusanya wateule wake kutoka kila upande wa dunia.
28 Jifunzeni somo hili kutoka katika mti wa mtini: Matawi yake yanaponyauka na kubeba majani, unajua kwamba kiangazi kimekaribia. 29 Vivyo hivyo, unapoona mambo haya yanaanza kutokea unajua kwamba muda umekaribia na umeshafika mlangoni. 30 Ninawaambieni ukweli: Kizazi hiki hakitapita kabla ya mambo haya yote hayajatokea. 31 Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe.
32 Hakuna anayejua wakiwemo malaika wa mbinguni ama Mwana bali baba peke yake lini siku au saa ile itakapowadia. 33 Mjihadhari; Kesheni! Kwani hamjui lini muda huo utafika.
34 Ni kama mtu anayeenda safarini na kabla ya kuondoka huiacha nyumba yake mikononi mwa watumishi wake. Kabla ya kuiacha nyumba yake anawaweka watumishi wake kusimamia kila mmoja akiwa na kazi yake maalumu. Kisha atamwamuru mlinzi mlangoni awe macho. 35 Vivyo hivyo ni lazima mjihadhari, kwa sababu hamjui ni muda gani mkuu wa nyumba atakuja; hamjui kama atakuja jioni, usiku wa manane, wakati jogoo anawika, au alfajiri. 36 Ikiwa atakuja ghafula, basi asiwakute mmelala. 37 Ninachowaambia, namwambia kila mmoja: ‘muwe tayari.’”
© 2017 Bible League International