Revised Common Lectionary (Semicontinuous)
1 Salamu toka kwa Paulo, Sila, na Timotheo.
Kwa kanisa lililoko Thesalonike lililo milki ya Mungu baba na Bwana Yesu Kristo.
Neema na amani ziwe zenu.
Maisha na Imani ya Wathesalonike
2 Kila mara tunamshukuru Mungu kwa ajili yenu nyote na kuwataja katika maombi yetu. 3 Kila tunapomwomba Mungu baba yetu, tunawakumbuka kwa yote mliyofanya kwa sababu ya imani yenu. Na tunawakumbuka kwa kazi mliyofanya kwa sababu ya upendo wenu. Na tunakumbuka jinsi mlivyo imara kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo.
4 Ndugu zetu, Mungu anawapenda. Nasi twajua yakuwa amewachagua muwe watu wake. 5 Tulipowaletea Habari Njema kwenu, tulikuja na yaliyo zaidi ya maneno. Tuliwaletea ile Habari Njema yenye uweza, pamoja na Roho Mtakatifu, na tulikuwa na uhakika kamili hiyo ilikuwa ni Kweli halisi. Pia mnafahamu tulivyo enenda tulipo kuwa pamoja nanyi. Tuliishi hivyo ili kuwasaidia ninyi. 6 Nanyi mkauiga mfano wetu na mfano wa Bwana. Mliteseka sana, lakini bado mliyakubali mafundisho na furaha inayotokana na Roho Mtakatifu.
7 Mlifanyika mfano wa kuigwa na waaminio wote wa Makedonia na Akaya. 8 Mafundisho ya Bwana yameenea toka Makedonia mpaka Akaya na nje ya mipaka yake. Kwa kweli, imani yenu katika Mungu imejulikana kila mahali, hivyo hatuna haja ya kumwambia mtu yeyote kwa habari hii. 9 Watu kila mahali wanasimulia habari ya namna mlivyotupokea vizuri tulipo kuwa pamoja nanyi. Wanasimulia namna mlivyoacha kuiabudu miungu ya uongo na kubadilika na kuanza kumwabudu Mungu aliye hai na wa kweli. 10 Na mkaanza kumngoja mwana wa Mungu aje kutoka mbinguni, Mwana ambaye Baba alimfufua kutoka kwa wafu. Yeye ni Yesu, anayetuokoa kutoka katika hukumu yenye hasira ya Mungu inayokuja.
Yesu Ajibu Swali Lenye Mtego
(Mk 12:13-17; Lk 20:20-26)
15 Kisha Mafarisayo wakaondoka mahali ambapo Yesu alikuwa anafundisha. Wakapanga mpango wa kumfanya aseme kitu ambacho wangekitumia dhidi yake. 16 Wakawatuma kwake baadhi ya wafuasi wao na baadhi ya watu kutoka katika kundi la Maherode. Watu hawa walipofika kwa Yesu wakasema, “Mwalimu, tunajua kuwa wewe ni mtu mwema na kwamba daima unafundisha ukweli kuhusu njia ya Mungu, bila kujali ni nani anakusikiliza. Huna wasiwasi namna ambavyo wengine wanaweza wakasema. 17 Sasa tuambie, unadhani ni sahihi kulipa kodi kwa Kaisari au la?”
18 Lakini Yesu alijua kuwa watu hawa walikuwa wanamtega. Hivyo akasema, “Enyi wanafiki! Kwa nini mnajaribu kunitega ili niseme jambo lililo kinyume? 19 Nionesheni sarafu inayotumika kulipa kodi.” Wakamwonesha Yesu sarafu iliyotengenezwa kwa fedha. 20 Kisha Yesu akauliza, “Picha iliyo kwenye sarafu hii ni ya nani? Na jina lililo kwenye sarafu hii ni la nani?”
21 Wakajibu, “Ni picha ya Kaisari na ni jina la Kaisari.”
Ndipo Yesu akawajibu, “Mpeni Kaisari vilivyo vyake na mpeni Mungu vilivyo vyake.”
22 Waliposikia yale Yesu aliyosema, wakashangaa na kuondoka.
© 2017 Bible League International