Revised Common Lectionary (Complementary)
Mungu Hajawakataa Watu wake
11 Hivyo ninauliza, “Je, Mungu aliwakataa watu wake?” Hapana! Mimi mwenyewe ni Mwisraeli, wa ukoo wa Ibrahimu, katika kabila la Benjamini. 2 Mungu aliwachagua Waisraeli wawe watu wake kabla hawajazaliwa. Na hajawakataa. Hakika mnajua Maandiko yanavyosema kuhusu Eliya anapomwomba Mungu dhidi ya watu wa Israeli. Anasema, 3 “Bwana, wamewaua manabii wako na kuharibu madhabahu zako. Mimi ndiye nabii pekee niliyebaki hai, na sasa wanajaribu kuniua mimi pia.”(A) 4 Lakini ni jibu gani Mungu alilompa Eliya? Mungu alisema, “Nimejihifadhia watu elfu saba wasiomwabudu Baali.”(B)
5 Ndivyo ilivyo sasa. Mungu amewachagua watu wachache kwa neema yake. 6 Na kama aliwachagua kwa neema yake, hivyo si kwa sababu ya matendo yao yaliyowafanya wawe watu wake. Kama wangefanywa kuwa watu wake kutokana na matendo yao, zawadi yake ya neema isingekuwa zawadi halisi.
7 Hivyo hivi ndivyo ilivyotokea: Watu wa Israeli wanazitaka sana baraka za Mungu, lakini si wote waliozipata. Watu aliowachagua walipata baraka zake, lakini wengine wakawa wagumu na wakakataa kumsikiliza. 8 Kama Maandiko yanavyosema,
“Mungu aliwafanya watu walale usingizi.”(C)
“Mungu aliyafumba macho yao ili wasione,
na aliyaziba masikio yao ili wasisikie.
Hili linaendelea hata sasa.”(D)
9 Na Daudi anasema,
“Watu hawa na wakamatwe na kunaswa
katika tafrija wanazofurahia.
Nyakati hizo nzuri ziwasababishe waanguke
ili wapate adhabu wanayoistahili.
10 Yapofushe macho yao ili wasiweze kuona.
Ipindishe migongo yao kwa mzigo wa matatizo.”(E)
© 2017 Bible League International