Readings for Lent and Easter
Yesu Aingia Yerusalemu Kama Mfalme
(Mk 11:1-11; Lk 19:28-38; Yh 12:12-19)
21 Yesu na wafuasi wake walipokaribia Yerusalemu, walisimama Bethfage kwenye kilima kinachoitwa Mlima wa Mizeituni. Wakiwa hapo Yesu aliwatuma wafuasi wake wawili mjini. 2 Aliwaambia, “Nendeni kwenye mji mtakaoweza kuuona huko. Mtakapoingia katika mji huo, mtamwona punda na mwanapunda wake.[a] Wafungueni wote wawili, kisha waleteni kwangu. 3 Mtu yeyote akiwauliza kwa nini mnawachukua punda, mwambieni, ‘Bwana anawahitaji. Atawarudisha mapema.’”
4 Hili lilitimiza maneno yaliyosemwa na nabii:
5 “Waambie watu wa Sayuni,[b]
‘Mfalme wako anakuja sasa.
Ni mnyenyekevu na amempanda punda.
Na amempanda mwana punda dume tena safi.’”(A)
6 Wafuasi walikwenda na kufanya yale walioambiwa na Yesu. 7 Waliwaleta kwake punda jike na mwanapunda. Waliwafunika punda kwa nguo zao na Yesu akaketi juu yao. 8 Akiwa njiani kuelekea Yerusalemu, watu wengi walitandaza mavazi yao barabarani kwa ajili Yake. Wengine walikata matawi ya miti na kuyatandaza barabarani ili kumkaribisha. 9 Wengine walimtangulia Yesu, na wengine walikuwa nyuma yake. Wote walipaza sauti wakisema:
“Msifuni[c] Mwana wa Daudi!
‘Karibu! Mungu ambariki yeye
ajaye katika jina la Bwana!’(B)
Msifuni Mungu wa mbinguni!”
10 Kisha Yesu aliingia Yerusalemu. Watu wote mjini wakataharuki. Wakauliza, “Mtu huyu ni nani?”
11 Kundi la watu waliomfuata Yesu wakajibu, “Huyu ni Yesu. Ni nabii kutoka katika mji wa Nazareti ulio Galilaya.”
Yesu Asafisha Eneo la Hekalu
(Mk 11:15-19; Lk 19:45-48; Yh 2:13-22)
12 Yesu alipoingia katika eneo la Hekalu, aliwatoa nje wote waliokuwa wanauza na kununua vitu humo. Alizipindua meza za watu waliokuwa wanabadilishana pesa. Na alipindua viti vya watu waliokuwa wanauza njiwa. 13 Yesu aliwaambia, “Maandiko yanasema, ‘Hekalu langu litaitwa nyumba ya sala.’(C) Lakini mmelibadilisha na kuwa ‘maficho ya wezi’.(D)”
14 Baadhi ya watu waliokuwa wasiyeona na walemavu wa miguu walimjia Yesu alipokuwa eneo la Hekalu, naye aliwaponya. 15 Viongozi wa makuhani na walimu wa sheria waliona mambo ya ajabu aliyokuwa anatenda. Na waliona watoto walivyokuwa wanamsifu wakisema, “Sifa kwa Mwana wa Daudi.” Mambo haya yote yaliwakasirisha makuhani na walimu wa sheria.
16 Wakamwuliza Yesu, “Unasikia wanayosema watoto hawa?”
Akajibu, “Ndiyo. Maandiko yanasema,
‘Umewafundisha watoto wadogo na watoto
wanyonyao kusifu.’(E)
Hamjasoma Maandiko haya?”
© 2017 Bible League International