Print Page Options
Previous Prev Day Next DayNext

Beginning

Read the Bible from start to finish, from Genesis to Revelation.
Duration: 365 days
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)
Version
Yohana 7-8

Yesu na Ndugu Zake

Baada ya hayo, Yesu alitembea kuizunguka miji ya Galilaya. Hakutaka kutembelea Uyahudi, kwa sababu viongozi wa Kiyahudi kule walitaka kumuua. Huu ulikuwa ni wakati wa sherehe za sikukuu ya Wayahudi ya Vibanda. Hivyo ndugu zake wakamwambia, “Unapaswa kuondoka hapa na kwenda kwenye sikukuu Uyahudi. Kisha wafuasi wako kule wataweza kuona ishara unazofanya. Ikiwa unataka kujulikana, basi usiyafiche mambo unayoyafanya. Ikiwa unaweza kufanya mambo ya ajabu hivi, acha ulimwengu wote uone.” Ndugu zake Yesu walisema hivi kwa kuwa hata wao hawakumwamini.

Yesu akawaambia, “Wakati unaonifaa kufanya hivyo haujafika, lakini kwenu ninyi kila wakati unafaa. Ulimwengu hauwezi kuwachukia ninyi. Bali ulimwengu unanichukia mimi kwa sababu nawaambia watu ulimwenguni ya kwamba wanafanya maovu. Hivyo ninyi nendeni kwenye sikukuu. Mimi sitaenda sasa, kwa sababu wakati unaonifaa haujafika.” Baada ya Yesu kusema hayo, akabaki Galilaya.

10 Ndugu zake nao wakaondoka kwenda kwenye sikukuu ya Wayahudi ya Vibanda. Baada ya kuondoka kwao Yesu naye akaenda huko, ingawa hakutaka watu wamwone. 11 Baada ya sikukuu ile kupita viongozi wa Kiyahudi wakawa wanamtafuta Yesu. Wakasema, “Yuko wapi huyo Yesu?”

12 Lilikuwepo kundi la watu wengi mahali pale. Wengi kati yao walikuwa wakizungumza kwa siri kuhusu Yesu. Wengine wakasema, “Huyu ni mtu mzuri.” Lakini wengine wakakataa na kusema, “Hapana, mtu huyo huwadanganya watu.” 13 Pamoja na hayo hakuwepo mtu aliyekuwa na busara zaidi kati yao kusema na Yesu kwa uwazi. Kwani waliwaogopa viongozi wa Wayahudi.

Yesu Afundisha Yerusalemu

14 Sherehe ile ilipokaribia kuisha, Yesu akaenda katika maeneo ya Hekalu na kuanza kufundisha. 15 Viongozi wa Kiyahudi waliomsikiliza walishangazwa na kusema, “Mtu huyu amejifunza wapi mambo haya yote? Yeye hakuwahi kupata mafundisho kama yale tuliyonayo.”

16 Yesu akajibu, “Ninayofundisha siyo yangu. Mafundisho yangu yanatoka kwake Yeye aliyenituma. 17 Watu wanaotaka kufanya kwa uhakika kama anavyotaka Mungu watafahamu kuwa mafundisho yangu yanatoka kwa Mungu. Watafahamu kwamba mafundisho haya siyo yangu. 18 Kama ningeyafundisha mawazo yangu, ningekuwa najitafutia heshima yangu mwenyewe. Lakini kama najaribu kumletea heshima Yeye aliyenituma, basi naweza kuaminiwa. Yeyote anayefanya kama hivyo hawezi kusema uongo. 19 Musa aliwapa sheria, sivyo? Lakini hamuitii hiyo sheria. Kama mnaitii, kwa nini basi mnataka kuniua?”

20 Watu wakamjibu Yesu, “Pepo amekuchanganya akili! Sisi hatuna mipango ya kukuua!”

21 Yesu akawambia, “Nilitenda ishara moja siku ya Sabato, na wote mkashangaa. 22 Lakini mnatii sheria aliyowapa Musa kuhusu kutahiriwa; nanyi mnatahiri hata siku ya Sabato! (Lakini hakika, Musa siye aliyewatahiri. Tohara Ilitoka kwa baba zenu walioishi kabla ya Musa.) Ndiyo, siku zote mnatahiri wana wenu hata siku ya Sabato. 23 Hii inaonesha kuwa mtu anaweza kutahiriwa siku ya Sabato ili kuitimiza sheria ya Musa. Sasa kwa nini mnanikasirikia mimi kwa kuuponya mwili wote wa mtu siku ya Sabato? 24 Acheni kuhukumu mambo ya watu kwa jinsi mnavyoyaona. Muwe makini kutoa kuhukumu kwa njia ya haki kabisa.”

Watu Wajiuliza Ikiwa Yesu Ni Masihi

25 Kisha baadhi ya watu waliokuwepo Yerusalemu wakasema, “Huyo ndiye mtu wanayetaka kumuua. 26 Lakini anafundisha mahali ambapo kila mtu anaweza kumwona na kumsikia. Wala hakuna anayejaribu kumzuia kufundisha. Inawezekana viongozi wamekubali kuwa kweli yeye ni Masihi. 27 Lakini Masihi halisi atakapokuja, hakuna atakayejua anakotoka. Nasi tunajua nyumbani kwake mtu huyu ni wapi.”

28 Yesu alikuwa bado anafundisha katika eneo la Hekalu aliposema kwa sauti, “Ni kweli mnanijua mimi na kule ninakotoka? Niko hapa, lakini siyo kwa matakwa yangu. Nilitumwa na Yeye aliye wa kweli. Lakini ninyi hamumjui. 29 Mimi namfahamu kwa sababu ninatoka kwake. Naye Ndiye aliyenituma.”

30 Yesu aliposema hivi, watu wakajaribu kumkamata. Lakini hakuna aliyethubutu hata kumgusa, kwa sababu wakati unaofaa kufanya hivyo ulikuwa bado haujafika. 31 Hata hivyo watu wengi wakamwamini Yesu. Wakasema, “Je, tunafikiri kuna haja ya kuendelea kumngojea Masihi mwingine aje atakayetenda ishara nyingine zaidi ya zile alizotenda mtu huyu?”

Viongozi wa Kiyahudi Wajaribu Kumkamata Yesu

32 Mafarisayo wakasikia yale ambayo watu walikuwa wakiyasema juu ya Yesu. Kwa sababu hiyo viongozi wa makuhani na Mafarisayo wakawatuma walinzi wa Hekalu kwenda kumkamata. 33 Kisha Yesu akasema, “Nitakuwa nanyi kwa muda mfupi. Kisha nitarudi kwake Yeye aliyenituma. 34 Ninyi mtanitafuta, lakini hamtaniona. Nanyi hamwezi kuja kule nitakapokuwa.”

35 Hawa Wayahudi wakaambiana wao kwa wao, “Huyu mtu atakwenda wapi sisi tusikoweza kufika? Je, anaweza kwenda kwenye miji ya Wayunani wanamoishi watu wetu? Je, atawafundisha Wayunani katika miji hiyo? 36 Anasema, ‘Mtanitafuta, lakini hamtaniona.’ Vile vile anasema, ‘Hamwezi kuja kule nitakapokwenda.’ Maana yake ni nini?”

Yesu Azungumza Juu ya Roho Mtakatifu

37 Siku ya mwisho ya kusherehekea sikukuu ikafika. Nayo Ilikuwa siku muhimu zaidi. Katika siku hiyo Yesu alisimama na kusema kwa sauti kubwa, “Yeyote aliye na kiu aje kwangu anywe. 38 Kama mtu ataniamini, mito ya maji yenye uzima itatiririka kutoka ndani ya moyo wake. Ndivyo Maandiko yanavyosema.” 39 Yesu alikuwa anazungumza juu ya Roho Mtakatifu ambaye alikuwa hajatolewa kwa watu bado, kwa sababu Yesu naye alikuwa bado hajatukuzwa. Ingawa baadaye, wale waliomwamini Yesu wangempokea huyo Roho.

Watu Wanabishana Juu ya Yesu

40 Watu waliposikia maneno aliyosema Yesu, baadhi yao wakasema, “Hakika mtu huyu ni nabii.”[a]

41 Wengine wakasema, “Huyu ni Masihi.”

Na wengine wakasema, “Masihi hawezi kutoka Galilaya. 42 Maandiko yanasema kwamba Masihi atatoka katika ukoo wa Daudi. Na wanasema kwamba atatoka Bethlehemu, mji alimoishi Daudi.” 43 Kwa jinsi hiyo watu hawakukubaliana wao kwa wao kuhusu Yesu. 44 Baadhi yao wakataka kumkamata. Lakini hakuna aliyejaribu kufanya hivyo.

Baadhi ya Viongozi wa Kiyahudi Wakataa Kuamini

45 Walinzi wa Hekalu wakarudi kwa viongozi wa makuhani na Mafarisayo. Makuhani na Mafarisayo wakawauliza, “Kwa nini hamjamleta Yesu?”

46 Walinzi wa Hekalu wakajibu, “Hatujawahi kumsikia mtu akisema mambo ya ajabu kiasi hicho!”

47 Mafarisayo wakajibu, “Kwa hiyo Yesu amewadanganya hata ninyi? 48 Hamuoni kuwa hakuna kiongozi yeyote wala sisi Mafarisayo anayemwamini? 49 Lakini watu hao walio nje wasiojua sheria wamo katika laana ya Mungu.”

50 Lakini Nikodemu alikuwa katika kundi lile. Naye ndiye yule aliyekwenda kumwona Yesu pale mwanzo.[b] Naye akasema, 51 “Sheria yetu haitaturuhusu kumhukumu mtu na kumtia hatiani kabla ya kumsikiliza kwanza na kuyaona aliyotenda?”

52 Viongozi wa Kiyahudi wakajibu, “Wewe nawe utakuwa umetoka Galilaya. Jifunze Maandiko. Hutapata lolote kuhusu nabii[c] anayetoka Galilaya.”

Mwanamke Afumaniwa Akizini

53 Kisha wote wakaondoka na kwenda nyumbani.

Usiku ule Yesu akaenda katika mlima wa Mizeituni. Mapema asubuhi akarudi katika eneo la Hekalu. Watu wengi wakaja kwake, naye akakaa pamoja nao na kuwafundisha.

Walimu wa sheria na Mafarisayo wakamleta kwake mwanamke waliyemfumania akizini. Wakamlazimisha asimame mbele ya watu. Wakamwambia Yesu, “Mwalimu, mwanamke huyu amekamatwa akifanya zinaa. Sheria ya Musa inatuagiza kumponda kwa mawe mpaka afe mwanamke wa jinsi hiyo. Je, Unasema tufanye nini?”

Watu hao waliyasema haya ili kumtega Yesu. Walitaka kumkamata akisema mambo tofauti ili wapate mashtaka ya kumshitaki. Lakini Yesu akainama chini na kuanza kuandika kwenye udongo kwa kidole chake. Viongozi wa Kiyahudi waliendelea kumuuliza swali lao hilo. Naye akainuka na kusema, “Yeyote hapa ambaye hajawahi kutenda dhambi awe wa kwanza kumponda jiwe mwanamke huyu.” Kisha Yesu akainama chini tena na kuendelea kuandika katika udongo.

Waliposikia hayo, wale watu walianza kuondoka mmoja baada ya mwingine. Wanaume wazee wakitangulia kwanza, na kisha wengine wakifuata. Wakamwacha Yesu peke yake na yule mwanamke akiwa amesimama mbele yake. 10 Kisha Yesu akainua uso wake tena na kumwambia, “Wameenda wapi hao wote? Je, hakuna aliyekuhukumu kuwa una hatia?” 11 Mwanamke akajibu, “Hakuna hata mmoja aliyenihukumu, Bwana.”[d]

Kisha Yesu akasema, “Hata mimi sikuhukumu. Unaweza kwenda sasa, lakini usifanye dhambi tena.”

Yesu ni Nuru ya Ulimwengu

12 Baadaye Yesu akazungumza tena na watu. Akasema, “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu. Yeyote atakayenifuata mimi hataishi gizani kamwe. Atakuwa na nuru inayoleta uzima.”

13 Lakini Mafarisayo wakamwambia Yesu, “Unapojishuhudia mwenyewe, unakuwa ni wewe peke yako unayethibitisha kuwa mambo haya ni kweli. Hivyo hatuwezi kuyaamini unayosema.”

14 Yesu akajibu, “Ndiyo, nasema mambo haya juu yangu mwenyewe. Lakini watu wanaweza kuamini ninayosema, kwa sababu mimi najua nilikotoka. Pia najua ninakoenda. Lakini ninyi hamjui mimi ninakotoka wala ninakoenda. 15 Mnanihukumu kama watu wanavyowahukumu wengine. Mimi simhukumu mtu yeyote. 16 Lakini ikiwa ninahukumu, basi hukumu yangu ni ya kweli, kwa sababu ninapohukumu sifanyi hivyo peke yangu. Baba aliyenituma yuko pamoja nami. 17 Sheria yenu inasema kwamba mashahidi wawili wakilisema jambo hilo hilo, basi mnapaswa kukubali wanayosema. 18 Mimi shahidi ninayeshuhudia mambo yangu mwenyewe. Na Baba yangu aliyenituma ndiye shahidi wangu mwingine.”

19 Watu wakamwuliza, “Baba yako yuko wapi?”

Yesu akajibu, “Hamnijui mimi wala Baba yangu hamumjui. Lakini mngenijua mimi, mngemjua Baba pia.”

20 Yesu alisema maneno haya alipokuwa anafundisha katika eneo la Hekalu, karibu na chumba ambamo sadaka za Hekaluni zilitunzwa. Hata hivyo hakuna hata mmoja aliyemkamata, kwa sababu wakati sahihi wa kufanya hivyo ulikuwa bado haujafika.

Baadhi ya Wayahudi Hawamwelewi Yesu

21 Kwa mara nyingine, Yesu akawaambia watu, “Mimi nitawaacha. Nanyi mtanitafuta, lakini pamoja na hayo mtakufa katika dhambi zenu. Kwani hamuwezi kuja kule niendako.”

22 Hivyo viongozi wa Kiyahudi wakaulizana wenyewe, “Je, atajiua mwenyewe? Je, ndiyo maana alisema, ‘Hamuwezi kuja kule niendako’?”

23 Lakini Yesu akawaambia, “Ninyi watu ni wa hapa chini, lakini mimi ni wa kule juu. Ninyi ni wa ulimwengu huu, lakini mimi si wa ulimwengu huu. 24 Niliwaambia kwamba mnaweza kufa katika dhambi zenu. Ndiyo, kama hamtaamini kuwa MIMI NDIYE,[e] mtakufa katika dhambi zenu.”

25 Wakamwuliza, “Sasa wewe ni nani?”

Yesu akajibu, “Mimi ni yule niliyekwisha kuwaambia tangu mwanzo kuwa ni nani. 26 Ninayo mengi zaidi ya kusema na ya kuwahukumu. Lakini nawaambia watu yale tu niliyosikia kutoka kwake aliyenituma, naye daima husema kweli.”

27 Wale watu hawakuelewa alikuwa anazungumza habari za nani. Kwani Yeye alikuwa anawaambia habari za Baba. 28 Naye akawaambia, “Mtamwinua juu[f] Mwana wa Adamu. Ndipo mtakapojua kuwa MIMI NDIYE. Mtajua kuwa lo lote nilifanyalo silifanyi kwa mamlaka yangu. Mtajua kuwa nayasema tu yale Baba yangu aliyonifundisha. 29 Yeye aliyenituma yuko pamoja nami. Siku zote nafanya yale yanayompendeza. Naye hajawahi kuniacha peke yangu.” 30 Yesu alipokuwa akisema mambo haya, watu wengi wakamwamini.

Yesu Azungumzia Uhuru kutokana na Dhambi

31 Hivyo Yesu akawaambia Wayahudi waliomwamini, “Kama mtaendelea kuyakubali na kuyatii mafundisho yangu, mtakuwa wafuasi wangu wa kweli. 32 Mtaijua kweli, na kweli hiyo itawafanya muwe huru.”

33 Wakamjibu, “Sisi ni wazaliwa wa Ibrahimu. Na hatujawahi kamwe kuwa watumwa. Sasa kwa nini unasema kuwa tutapata uhuru?”

34 Yesu akasema, “Ukweli ni huu, kila anayefanya dhambi ni mtumwa wa dhambi. 35 Mtumwa hakai na jamaa yake siku zote. Lakini mwana hukaa na jamaa yake siku zote. 36 Hivyo kama Mwana atawapa uhuru, mtakuwa mmepata uhuru wa kweli. 37 Najua kuwa ninyi ni wazaliwa wa Ibrahimu. Lakini mmekusudia kuniua, kwa sababu hamtaki kuyakubali mafundisho yangu. 38 Nawaambia yale ambayo Baba yangu amenionyesha. Lakini ninyi mnayafanya yale mliyoambiwa na baba yenu.”

39 Wakasema, “Baba yetu ni Ibrahimu.”

Yesu akasema, “Kama mngekuwa wazaliwa wa Ibrahimu kweli, mngefanya yale aliyofanya Ibrahimu. 40 Mimi ni mtu niliyewaambia ukweli niliousikia kutoka kwa Mungu. Lakini Ibrahimu hakufanya kama hayo mnayotaka kufanya. 41 Mnafanya yale aliyofanya baba yenu.”

Lakini wakasema, “Sisi sio kama watoto ambao hawajawahi kumjua baba yao ni nani. Mungu ni Baba yetu. Ni baba pekee tuliye naye.”

42 Yesu akawaambia, “Kama Mungu angekuwa Baba yenu kweli, mngenipenda. Nilitoka kwa Mungu, na sasa niko hapa. Sikujileta kwa mamlaka yangu mwenyewe. Mungu alinituma. 43 Hamuyaelewi mambo ninayosema, kwa sababu hamuwezi kuyakubali mafundisho yangu. 44 Baba yenu ni ibilisi. Ninyi ni wa kwake. Nanyi mnataka kufanya anayotaka. Yeye alikuwa muuaji tangu mwanzo. Siku zote alikuwa kinyume na ukweli. Hakuna ukweli ndani yake. Yuko kama uongo anaousema. Ndiyo, ibilisi ni mwongo. Na ni baba wa uongo.

45 Nawaambieni ukweli, na ndiyo maana hamniamini. 46 Kuna mtu miongoni mwenu anayeweza kunishuhudia kuwa mimi nina hatia ya dhambi? Kama nawaeleza ukweli, kwa nini hamniamini? 47 Yeyote aliye wa Mungu huyapokea anayosema. Lakini ninyi hamuyapokei anayosema Mungu, kwa sababu ninyi si wa Mungu.”

Yesu Azungumza Juu yake na Ibrahimu

48 Wayahudi wakajibu, “Sisi tunasema kuwa wewe ni Msamaria na pepo anakufanya uwe mwendawazimu! Je, hatuko sahihi kusema hivyo?”

49 Yesu akajibu, “Sina pepo ndani yangu. Nampa heshima Baba yangu, lakini ninyi hamnipi heshima. 50 Sijaribu kujitukuza mimi mwenyewe. Yupo mmoja anayetaka kunitukuza. Ndiye hakimu. 51 Nawaahidi, yeyote anayeendelea kutii mafundisho yangu, hatakufa milele.”

52 Wayahudi wakamwambia Yesu, “Sasa tunatambua kuwa una pepo ndani yako! Hata Ibrahimu na manabii walikufa. Lakini unasema, ‘Yeyote anayetii mafundisho yangu, hatakufa kamwe.’ 53 Wewe si mkuu zaidi ya baba yetu Ibrahimu! Yeye alikufa na manabii nao walikufa. Unadhani wewe ni nani?”

54 Yesu akajibu, “Kama ningejipa heshima mwenyewe, heshima hiyo isingelifaa kwa namna yoyote ile. Yule anayenipa mimi heshima ni Baba yangu. Ninyi mnasema kuwa ndiye Mungu wenu. 55 Lakini kwa hakika hamumjui yeye. Mimi namjua. Kama ningesema simjui, basi ningekuwa mwongo kama ninyi. Lakini namjua, na kuyatii anayosema. 56 Baba yenu Ibrahimu alifurahi sana kwamba angeiona siku nilipokuja duniani. Hakika aliiona na akafurahi sana.”

57 Wayahudi wakamwambia Yesu, “Ati nini? Wawezaje kusema ulimwona Ibrahimu? Wewe bado hujafikisha hata umri wa miaka hamsini!”

58 Yesu akajibu, “Ukweli ni kwamba, kabla Ibrahimu hajazaliwa MIMI NIPO.” 59 Aliposema haya, wakachukua mawe ili wamponde. Lakini Yesu akajificha, na kisha akaondoka katika eneo la Hekalu.

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)

© 2017 Bible League International