Print Page Options
Previous Prev Day Next DayNext

Beginning

Read the Bible from start to finish, from Genesis to Revelation.
Duration: 365 days
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)
Version
Ufunuo 17-19

Mwanamke Juu ya Mnyama Mwekundu

17 Mmoja wa malaika saba waliokuwa na bakuli sa akaja kuzungumza nami. Akasema, “Njoo, nami nitakuonesha adhabu itakayotolewa kwa kahaba maarufu. Ndiye yule aketiye juu ya maji mengi. Watawala wa dunia walizini pamoja naye. Watu wa dunia walilewa kutokana na mvinyo wa dhambi yake ya uzinzi.”

Kisha malaika akanichukua mbali kwa Roho Mtakatifu mpaka jangwani. Huko nikamwona mwanamke amekaa juu ya mnyama mwekundu. Mnyama alikuwa ameandikwa majina ya kumkufuru Mungu katika mwili wake wote. Alikuwa na vichwa saba na pembe kumi. Mwanamke aliyekuwa juu yake alikuwa amevaa nguo za zambarau na nyekundu. Alikuwa anang'aa kutokana na dhahabu, vito na lulu alizokuwa amevaa. Mkononi mwake alikuwa ameshika kikombe cha dhahabu. Kikombe hiki kilijaa maovu na machukizo ya dhambi yake ya uzinzi. Alikuwa na jina kwenye kipaji cha uso wake. Jina hili lina maana iliyofichwa. Hiki ndicho kilichoandikwa:

babeli mkuu

mama wa makahaba

na machukizo ya dunia.

Nikatambua kuwa mwanamke alikuwa amelewa. Alikuwa amelewa kwa damu ya watakatifu wa Mungu. Alikuwa amelewa kwa damu ya wale walioshuhudia imani yao katika Yesu Kristo.

Nilipomwona mwanamke, nilishangaa sana. Kisha malaika akaniambia, “Kwa nini unashangaa? Nitakuambia maana iliyofichwa kuhusu mwanamke huyu na mnyama mwenye vichwa saba na pembe kumi anayeendeshwa na mwanamke huyu. Mnyama unayemwona alikuwa hai kwanza, lakini sasa si hai. Hata hivyo, atapanda kutoka kuzimu na kwenda kuangamizwa. Watu wanaoishi duniani watashangaa watakapomwona mnyama, kwa sababu aliwahi kuwa hai, hayuko hai, lakini atakuwa hai tena. Hawa ni watu ambao majina yao hayajawahi kuandikwa katika kitabu cha uzima tangu mwanzo wa ulimwengu.

Unahitaji hekima kulielewa hili. Vichwa saba juu ya mnyama ni milima saba ambako mwanamke amekaa. Pia ni watawala saba. 10 Watawala watano wamekwisha kufa tayari. Mmoja wa watawala anaishi sasa, na mtawala wa mwisho anakuja. Atakapokuja, atakaa kwa muda mfupi tu. 11 Mnyama ambaye hapo kwanza alikuwa hai, lakini haishi tena ni mtawala wa nane. Naye ni mmoja wa watawala saba wa kwanza. Naye ataangamizwa.

12 Pembe kumi ulizoziona ni watawala kumi. Watawala hawa kumi hawajapata falme zao, lakini watapata nguvu ya kutawala pamoja na mnyama kwa saa moja. 13 Lengo la watawala hawa wote kumi linafanana. Nao watampa mnyama nguvu na mamlaka yao. 14 Watafanya vita kinyume na Mwanakondoo. Lakini Mwanakondoo atawashinda, kwa sababu ni Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme. Pamoja naye watakuwepo wateule wake na wafuasi waaminifu, watu aliowaita kuwa wake.”

15 Kisha malaika akaniambia, “Uliyaona maji ambako kahaba amekaa. Maji haya ni watu wengi, wa asili, mataifa, na lugha tofauti ulimwenguni. 16 Mnyama na pembe kumi ulizoziona watamchukia kahaba. Watachukua kila kitu alichonacho na kumwacha akiwa uchi. Watakula nyama yake na kumteketeza kwa moto. 17 Mungu aliweka wazo katika akili zao kutenda yale yatakayotimiza kusudi lake. Walikubaliana kumpa mnyama nguvu zao kutawala mpaka yale aliyosema Mungu yamekamilika. 18 Mwanamke uliyemwona ni mji mkuu ambao unatawala juu ya wafalme wa dunia.”

Babeli Inaangamizwa

18 Kisha nikaona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni. Malaika huyu alikuwa na nguvu kuu. Utukufu wa malaika ukaing'arisha dunia. Malaika akapaza sauti akasema:

“Ameteketezwa!
    Mji mkuu Babeli umeteketezwa!
Umekuwa nyumba ya mapepo.
    Mji ule umekuwa najisi.
Mji uliojaa kila aina ya ndege najisi.
    Ni mahali ambapo kila mnyama najisi
    na anayechukiwa anaishi.
Watu wote wa dunia wamekunywa mvinyo
    wa uzinzi wake na ghadhabu ya Mungu.
Watawala wa dunia walizini pamoja naye,
    na wafanya biashara wa ulimwengu walitajirika
    kutokana na utajiri wa anasa zake.”

Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni ikisema:

“Enyi watu wangu, tokeni katika mji huo,
    ili msishiriki katika dhambi zake.
    Ili msiteseke kwa adhabu yoyote kuu atakayoipata.
Dhambi za mji huo zimerundikana na kufika mbinguni.
    Mungu hajasahau makosa aliyotenda.
Upeni mji huo sawasawa na ulivyowapa wengine.
    Mlipeni mara mbili kadiri ya alivyotenda.
Mwandalieni mvinyo ulio na nguvu mara mbili
    ya mvinyo aliowaandalia wengine.
Alijipa utukufu mwingi na kuishi kitajiri.
    Mpeni mateso mengi na huzuni nyingi.
    Kama vile utukufu na starehe aliyoifurahia.
Hujisemea mwenyewe, ‘Mimi ni malkia nikaaye kwenye kiti changu cha enzi.
    Mimi si mjane;
    Sitakuwa na huzuni.’
Hivyo katika siku moja atateseka
    kwa njaa kuu, maombolezo na kifo.
Atateketezwa kwa moto,
    kwa sababu Bwana Mungu anayemhukumu ni mwenye nguvu.”

Watawala wa dunia waliozini pamoja naye na kushiriki utajiri wake watakapoona moshi wa kuungua kwake, watalia na kuhuzunika kwa sababu ya kifo chake. 10 Wataogopa mateso yake na kukaa mbali sana. Watasema:

“Inatisha! Inatisha sana, Ee mji mkuu,
    ee Babeli, mji wenye nguvu!
Adhabu yako imekuja katika saa moja!”

11 Na wafanya biashara wa dunia watalia na kuhuzunika kwa ajili yake. Watahuzunika kwa sababu hakutakuwa hata mmoja wa kununua vitu wanavyouza; 12 dhahabu, fedha, vito, lulu, nguo za kitani safi, nguo za zambarau, hariri na nguo nyekundu, aina zote za mti wa udi, na aina zote za vitu vilivyotengenezwa kutokana na pembe za wanyama, miti ya thamani, shaba, chuma, na marimari. 13 Na mdalasini, viungo, uvumba, marhamu, ubani, mvinyo, mafuta ya mzeituni, unga safi, ngano, ng'ombe, kondoo, farasi, magari na watumwa, ndiyo hata maisha ya watu. Wafanya biashara watalia na kusema:

14 “Ee Babeli, mambo mazuri uliyoyataka yamekuacha.
Utajiri wako wote na vitu vya fahari vimetoweka.
    Hautakuwa navyo tena.”

15 Wafanya biashara wataogopa mateso yake na watakaa mbali naye. Hawa ni wale waliotajirika kwa kumwuzia vitu hivyo. Watalia na kuhuzunika. 16 Watasema:

“Inatisha! Inatisha kwa mji mkuu!
    Alivalishwa kitani safi;
    alivaa zambarau na nguo nyekundu.
    Alikuwa anang'aa kwa sababu ya dhahabu, vito na lulu!
17 Utajiri wote huu umeteketezwa kwa saa moja!”

Kila nahodha, wote ambao husafiri katika meli, mabaharia na wote ambao hupata pesa kutokana na bahari walisimama mbali na Babeli. 18 Waliuona moshi wa kuungua kwake. Walilia kwa sauti, “Hakukuwa na mji kama mji huu mkuu!” 19 Walirusha mavumbi juu ya vichwa vyao na kulia kwa sauti kuu kuonesha huzuni kuu waliyokuwa nayo. Walisema:

“Inatisha! Inatisha sana kwa mji mkuu!
    Wote waliokuwa na meli baharini walitajirika kwa sababu ya utajiri wake!
    Lakini umeteketezwa katika saa moja!
20 Ufurahi kwa sababu ya hili, Ee mbingu!
    Furahini, watakatifu wa Mungu, mitume na manabii!
Mungu amemhukumu kwa sababu ya kile alichowatendea ninyi.”

21 Kisha malaika mwenye nguvu akainua jiwe kubwa. Jiwe hili lilikuwa kubwa kama jiwe kubwa la kusagia. Malaika akalitupia jiwe baharini na kusema:

“Hivyo ndivyo mji mkuu Babeli utakavyotupwa chini.
    Hautaonekana tena.
22 Ee Babeli, muziki wa wapigao vinanda na ala zingine waimbaji na tarumbeta,
    hautasikika tena ndani yako.
Hakuna mfanyakazi afanyaye kazi atakayeonekana ndani yako tena.
    Sauti ya jiwe la kusagia haitasikika ndani yako tena.
23 Mwanga wa taa hautang'aa ndani yako tena.
    Sauti za maarusi hazitasikika ndani yako tena.
Wafanyabiashara wako walikuwa watu wakuu wa ulimwengu.
    Mataifa yote yalidanganyika kwa uchawi wako.
24 Una hatia ya vifo vya manabii, na watakatifu wa Mungu,
    na vya wote waliouawa duniani.”

Watu Wamsifu Mungu Mbinguni

19 Baada ya hili nikasikia kitu kilichosikika kama kundi kubwa la watu mbinguni. Walikuwa wakisema:

“Haleluya![a]
Ushindi, utukufu na nguvu ni vyake Mungu wetu.
    Hukumu zake ni za kweli na za haki.
Mungu wetu amemwadhibu kahaba.
    Ndiye aliyeiharibu dunia kwa uzinzi wake.
Mungu amemwadhibu kahaba kulipa kisasi cha vifo vya watumishi wake.”

Pia, watu hawa walisema:

“Haleluya!
    Anaungua na moshi wake utasimama milele na milele.”

Ndipo wazee ishirini na nne na viumbe wenye uhai wanne wakaanguka chini kusujudu wakamwabudu Mungu, akaaye kwenye kiti cha enzi. Wakasema:

“Amina! Haleluya!”

Sauti ikatoka kwenye kiti cha enzi na kusema:

“Msifuni Mungu wetu,
    ninyi nyote mnaomtumikia!
Msifuni Mungu wetu,
    ninyi nyote mlio wadogo na wakubwa mnaomheshimu!”

Kisha nikasikia kitu kilichosikika kama kundi kubwa la watu. Kilikuwa na kelele kama mawimbi ya bahari au radi. Watu walikuwa wakisema:

“Haleluya!
    Bwana Mungu wetu anatawala.
    Ndiye Mwenye Nguvu, Mungu Mwenyezi.
Tushangilie na kufurahi na
    kumpa Mungu utukufu!
Mpeni Mungu utukufu, kwa sababu arusi ya Mwanakondoo imewadia.
    Na bibi arusi wa Mwanakondoo amekwisha jiandaa.
Nguo ya kitani safi ilitolewa kwa bibi arusi ili avae.
    Kitani ilikuwa safi na angavu.”

(Kitani safi inamaanisha mambo mazuri ambayo watakatifu wa Mungu waliyatenda.)

Kisha malaika akaniambia, “Andika hili: Heri ni kwa wale walioalikwa kwenye karamu ya arusi ya Mwanakondoo!” Kisha malaika akasema, “Haya ni maneno ya Mungu mwenyewe.”

10 Kisha nikaanguka chini mbele miguuni pa malaika ili nimwabudu. Lakini malaika akaniambia, “Usiniabudu! Mimi ni mtumishi kama wewe na ndugu zako na dada zako walio na ushuhuda kuhusu Yesu Kristo. Hivyo mwabudu Mungu! Kwa sababu ushuhuda kuhusu Yesu ndiyo roho ya unabii.”

Mpanda Farasi Juu ya Farasi Mweupe

11 Kisha nikaona mbingu zimefunguka, na nikamwona farasi mweupe. Mpanda farasi aliitwa Mwaminifu na Kweli, kwa sababu ni wa haki katika maamuzi yake na kufanya vita. 12 Macho yake yalikuwa kama mwali wa moto. Alikuwa na taji nyingi kichwani mwake. Jina lilikuwa limeandikwa juu yake, lakini yeye peke yake ndiye aliyejua maana ya jina hilo. 13 Alivaa vazi lililochovywa katika damu, na aliitwa Neno la Mungu. 14 Majeshi ya mbinguni yalikuwa yanamfuata mpanda farasi mweupe. Walikuwa wanaendesha farasi weupe pia. Walikuwa wamevaa kitani nzuri, nyeupe na safi. 15 Upanga mkali ulikuwa unatoka kwenye kinywa chake, upanga ambao angeutumia kuyashinda mataifa. Na atayatawala mataifa kwa fimbo ya chuma. Atazikanyaga zabibu katika shinikizo la ghadhabu ya Mungu Mwenye Nguvu. 16 Kwenye vazi lake na kwenye mguu wake alikuwa ameandikwa jina lake:

mfalme wa wafalme na bwana wa mabwana.

17 Kisha nikaona malaika amesimama katika jua. Kwa sauti kuu malaika akawaambia ndege wote wanaoruka angani, “Kusanyikeni kwa ajili ya karamu kuu ya Mungu. 18 Kusanyikeni mle miili ya watawala, majemadari na watu maarufu. Njooni mle miili ya farasi na wanaowapanda na miili ya watu wote, walio huru na watumwa, wadogo na wakubwa.”

19 Kisha nikamwona mnyama na watawala wa dunia. Majeshi yao yalikusanyika pamoja ili kufanya vita kupigana na mpanda farasi mweupe na jeshi lake. 20 Lakini mnyama na nabii wa uongo walikamatwa. Nabii wa uongo ndiye aliyefanya miujiza[b] kwa ajili ya mnyama. Alitumia miujiza hii kuwahadaa wale waliokuwa na alama ya mnyama na walioabudu sanamu yake. Nabii wa uongo na mnyama walitupwa kwenye ziwa la moto linalowaka kwa baruti. 21 Majeshi yao yaliuawa kwa upanga uliotoka kwenye kinywa cha mpanda farasi. Ndege wote walikula miili hii mpaka wakashiba.

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)

© 2017 Bible League International