Print Page Options
Previous Prev Day Next DayNext

Beginning

Read the Bible from start to finish, from Genesis to Revelation.
Duration: 365 days
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)
Version
1 Wakorintho 15-16

Habari Njema Kuhusu Yesu Kristo

15 Sasa ndugu zangu, ninataka mkumbuke Habari Njema niliyowahubiri. Mliupokea ujumbe huo na endeleeni kuishi kwa kuufuata. Habari Njema hiyo, ujumbe mliousikia kutoka kwangu, ni njia ya Mungu kuwaokoa. Ni lazima mwendelee kuuamini. Ikiwa mtaacha, kuamini kwenu ni bure.

Niliwapa ujumbe nilioupokea. Niliwaambia ukweli muhimu zaidi ya kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama Maandiko yanavyosema; kuwa alizikwa na alifufuliwa siku ya tatu, kama Maandiko yanavyosema na kwamba alimtokea Petro kisha mitume kumi na wawili. Baada ya hilo, aliwatokea waamini wengine zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja. Wengi wao bado wanaishi sasa, lakini wengine wamekwisha kufa. Kisha alimtokea Yakobo na baadaye aliwatokea mitume wote. Mwisho wa yote kabisa alinitokea mimi. Nilikuwa tofauti, kama mtoto anayezaliwa wakati usiostahili.

Mitume wengine wote ni wakuu kuliko mimi. Ninasema hivi kwa sababu nililitesa kanisa la Mungu. Ndiyo sababu sistahili hata kuitwa mtume. 10 Lakini, kwa sababu ya neema ya Mungu, ndivyo hivi nilivyo. Na neema aliyonipa haikupotea bure bila manufaa. Nilifanya kazi kwa bidii kuliko mitume wengine wote. (Lakini, kwa hakika si mimi niliyekuwa nafanya kazi. Ni neema ya Mungu iliyo ndani yangu.) 11 Hivyo basi, si muhimu ikiwa ni mimi au mitume wengine ndiyo waliowahubiri, sisi sote tunawahubiri watu ujumbe huo huo, na hiki ndicho mlichoamini.

Tutafufuliwa Kutoka kwa Wafu

12 Tunamwambia kila mtu kuwa Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu. Hivyo kwa nini baadhi yenu mnasema watu hawatafufuliwa kutoka kwa wafu? 13 Ikiwa hakuna atakayefufuliwa kutoka kwa wafu, basi Kristo hakufufuliwa kutoka kwa wafu. 14 Na ikiwa Kristo hakufufuliwa, ujumbe tunaowahubiri ni bure. Na imani yenu ni bure. 15 Nasi tutakuwa na hatia ya kutoa ushuhuda wa uongo kuhusu Mungu, kwa sababu tumewahubiri watu kuhusu Yeye, kwa kusema kuwa alimfufua Kristo kutoka kwa wafu. Na ikiwa hakuna anayefufuliwa kutoka kwa wafu, basi Mungu hakumfufua Kristo. 16 Ikiwa wale waliokufa hawatafufuliwa, basi Kristo hakufufuliwa pia. 17 Na ikiwa Kristo hakufufuliwa kutoka kwa wafu, basi imani yenu ni bure; bado mngali watumwa wa dhambi zenu. 18 Na watu wa Kristo waliokwisha kufa wamepotea. 19 Ikiwa tumaini letu katika Kristo ni kwa ajili tu ya maisha haya hapa duniani, basi watu watuhurumie sisi kuliko mtu mwingine yeyote.

20 Lakini hakika Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu; ndiye wa kwanza miongoni mwa wafu wote watakaofufuliwa. 21 Kifo huja kwa watu kwa sababu ya tendo la mtu mmoja. Lakini sasa kuna ufufuo kutoka kwa wafu kwa sababu ya mtu mwingine. 22 Ndiyo, kwa sababu sisi sote ni wa Adamu, sisi sote tunakufa. Kwa njia hiyo hiyo, sisi sote tulio wa Kristo, tutakuwa hai tena. 23 Lakini kila mmoja atafufuliwa kwa mpango sahihi. Kristo alikuwa wa kwanza kufufuliwa. Kisha atakaporudi, wale walio wake watafufuliwa. 24 Ndipo mwisho utakuja. Kristo atamwangamiza kila mtawala na kila mamlaka na nguvu. Kisha atampa Mungu Baba ufalme.

25 Kristo lazima atawale mpaka Mungu atakapowaweka adui zake wote chini ya udhibiti wake.[a] 26 Adui wa mwisho kuangamizwa ni kifo. 27 Kama Maandiko yanavyosema, “Mungu ameweka kila kitu chini ya udhibiti wake.”(A) Inaposema “kila kitu” kimewekwa chini yake, hii ni wazi Mungu peke yake ndiye ambaye hayuko chini yake. Mungu ndiye anayeweka kila kitu chini ya udhibiti wa Kristo. 28 Baada ya kuweka kila kitu chini ya Kristo, ndipo yeye mwenyewe, kama Mwana, atawekwa chini ya Mungu. Katika namna hii Mungu atakuwa mtawala mkuu juu ya kila kitu.

29 Ikiwa hakuna atakayefufuliwa kutoka kwa wafu, sasa watu wanafikiri wanafanya nini kwa kubatizwa kwa ajili ya wale waliokufa? Ikiwa wafu hawafufuliwi kamwe, kwa nini watu wanabatizwa kwa ajili yao?

30 Na vipi kuhusu sisi? Kwa nini tunajiweka katika hatari wakati wote? 31 Ninakumbana na kifo kila siku. Ni kweli, ndugu zangu kwamba ninajivuna kwa sababu ninyi ni wa Kristo Yesu Bwana wetu. 32 Niliwapiga wanyama wa porini kule Efeso. Ikiwa nilifanya hivyo kwa sababu za kibinadamu tu, sijapata kitu. Ikiwa hatufufuliwi kutoka kwa wafu, “basi tule na tunywe, kwa sababu tutakufa kesho.”(B)

33 Msidanganywe: “Marafiki wabaya huharibu tabia njema.” 34 Rudieni kuwaza kwenu kwa usahihi na acheni kutenda dhambi. Baadhi yenu hamumjui Mungu. Ninasema hivi ili niwafedheheshe.

Tutakuwa na Mwili wa Namna Gani?

35 Lakini mtu mmoja anaweza kuuliza, “Waliokufa wanafufuliwaje? Watakuwa na mwili wa namna gani?” 36 Haya ni maswali ya kijinga. Unapopanda kitu fulani, ni lazima kife udongoni kabla hakijawa hai na kuota. 37 Na unapopanda kitu fulani, unachopanda hakina “mwili” sawa na ule kitakachokuwa nao baadaye. Unapanda mbegu, pengine ngano au kitu kingine. 38 Na yeye Mungu hutoa mwili kwa kila aina ya mbegu. 39 Vitu vyote vilivyoumbwa kwa mwili haviko sawa: Wanadamu wana aina moja ya mwili, wanyama wana aina nyingine, ndege wana nyingine na samaki nao wana aina yao. 40 Pia kuna miili ya kimbingu na miili ya kidunia. Lakini uzuri wa miili ya kimbingu ni wa aina yake na uzuri wa miili ya kidunia ni kitu kingine. 41 Jua lina uzuri wa aina yake, mwezi una aina yake na nyota zina aina nyingine ya uzuri. Na kila nyota iko tofauti kwa uzuri wake.

42 Ndivyo itakavyokuwa waliokufa watakapofufuliwa na kuwa hai. Mwili “uliopandwa” kaburini utaharibika na kuoza, lakini utafufuliwa katika uhai usioharibika. 43 Mwili hauna heshima “unapopandwa”. Lakini utakapofufuliwa, utakuwa na utukufu. Mwili unakuwa dhaifu “unapopandwa”. Lakini unapofufuliwa, unakuwa na nguvu nyingi. 44 Mwili unaopandwa ni mwili wa kawaida, wa asili. Utakapofufuliwa utakuwa mwili wa ajabu uliopewa uwezo na Roho.

Kuna mwili wa asili unaoonekana kwa macho. Na hivyo kuna mwili wa Kiroho wa ajabu. 45 Kama Maandiko yanavyosema, “Mtu[b] wa kwanza, Adamu, alikuwa kiumbe asili kilichokuwa hai.”(C) Lakini Adamu[c] wa mwisho akafanyika roho. 46 Mtu wa kiroho hakuja kwanza. Mtu wa asili anayeonekana kwa macho ndiye alikuja kwanza; kisha akaja wa kiroho. 47 Mtu wa kwanza alitokana na mavumbi ya dunia. Mtu wa pili alitoka mbinguni. 48 Watu wote ni wa dunia. Wako sawa na yule mtu wa kwanza wa dunia. Lakini wale walio wa mbinguni wako kama mtu wa mbinguni. 49 Tumeivaa sura ya mtu aliyetoka mavumbini, pia tutaivaa sura ya mtu aliyetoka mbinguni.

50 Ninawaambia hili ndugu zangu: Miili yetu na nyama na damu haiwezi kuwa na nafasi katika ufalme wa Mungu. Kitu kitakachoharibika hakiwezi kuwa na sehemu katika kitu kisichoharibika kamwe. 51 Lakini sikilizeni, ninawaambia siri hii: Sote hatutakufa, lakini sote tutabadilishwa. 52 Itachukuwa sekunde moja. Tutabadilishwa kufumba na kufumbua. Hili litatokea parapanda ya mwisho itakapopulizwa. Parapanda itakapolia wale waliokufa watafufuliwa ili waishi milele. Na tutabadilishwa sote. 53 Mungu ataibadilisha miili yetu ili isiharibike kamwe. Mwili huu unaokufa utabadilishwa na kuwa mwili usiokufa. 54 Hivyo mwili huu unaokufa utajivika kutokufa. Hili litakapotokea, ndipo Maandiko yatatimilizwa:

“Mauti imemezwa katika ushindi.(D)
55 Ewe kifo, ushindi wako uko wapi?
    Nguvu yako ya kudhuru iko wapi?”(E)

56 Dhambi ni nguvu ya mauti inayodhuru, na nguvu ya dhambi ni sheria. 57 Lakini tunamshukuru Mungu anayetupa ushindi kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!

58 Hivyo, kaka na dada zangu, simameni imara. Msiruhusu kitu chohote kiwabadilishe. Jitoeni nafsi zenu kikamilifu kwa kazi yenu katika Bwana. Mnajua ya kuwa chochote mnachofanya kwa ajili ya Bwana hakitapotea bure bila manufaa.

Makusanyo kwa Ajili ya Waamini Katika Uyahudi

16 Sasa, kuhusu mchango wa pesa kwa ajili ya watu wa Mungu: Fanyeni kama nilivyoyaambia makanisa ya Galatia kufanya. Siku ya kwanza ya kila wiki, kila mmoja wenu achukue kiasi cha pesa kutoka kwenye pesa zake na azitenge. Akusanye kiasi anachoweza kutokana na anavyobarikiwa. Na hivyo hamtahitaji kukusanya nitakapokuja. Nitakapofika, nitatuma baadhi ya watu wapeleke sadaka yenu Yerusalemu. Hawa watakuwa wale ambao ninyi mtakubali kuwa waende. Nitawatuma na barua ya utambulisho. Ikiwa itakuwa vizuri kwangu kwenda pia, basi tutasafiri pamoja.

Mipango ya Paulo

Nimepanga kupitia Makedonia, hivyo nitakuja kwenu baada ya hapo. Pengine nitakaa kwenu kwa muda. Pengine nitakaa kwenu majira yote ya baridi. Hivyo mtaweza kunisaidia katika safari yangu, kila ninapokwenda. Sitaki kuja kuwaona sasa, kwa sababu nitaweza tu kukaa nanyi kwa muda mfupi, kabla haijanilazimu kwenda mahali pengine. Ninategemea kukaa pamoja nanyi kwa muda mrefu, ikiwa Bwana ataruhusu. Lakini nitakaa Efeso mpaka wakati wa Pentekoste. Nitakaa hapa, kwa sababu sasa nimepewa fursa nzuri kwa kazi kubwa na inayokua. Na kuna watu wengi wanaopinga.

10 Timotheo atakapokuja kwenu, mjitahidi akae kwa raha na amani akiwa kwenu. Anafanya kazi kwa ajili ya Bwana kama mimi. 11 Hivyo yeyote miongoni mwenu asikatae kumpokea Timotheo. Msaidieni aendelee katika safari yake kwa amani ili aweze kurudi kwangu. Ninategemea atakuja kwangu pamoja na ndugu wengine.

12 Na sasa kuhusu Apolo: Ninamsihi sana aje na ndugu wengine kuwatembelea ninyi huko Korintho. Hajataka kuja sasa, lakini atakuja kwenu atakapopata nafasi.

Paulo Amalizia Barua Yake

13 Iweni waangalifu. Simameni imara katika imani yenu. Mwe jasiri na wenye nguvu. 14 Fanyeni kila kitu katika upendo.

15 Mnajua kuwa Stefana na familia yake walikuwa waamini wa kwanza katika Akaya. Wamejitia katika kazi ya kuwahudumia watu wa Mungu. Ndugu zangu, ninawaomba, 16 mjiweke chini ya uongozi wa watu kama hawa na wengine wanaofanya kazi kwa bidii na kutumika pamoja nao.

17 Ninafurahi kwa sababu Stefana, Fortunato na Akaiko wamekuja. Hamko hapa pamoja nami lakini wamejaza nafasi yenu. 18 Wamekuwa faraja kuu kwangu na kwenu pia. Basi, mnapaswa kuitambua thamani ya watu kama hawa.

19 Makanisa ya Asia yanawasalimu. Akila na Priska wanawasalimu katika Bwana. Na kanisa linalokutana nyumbani mwao linawasalimu pia. 20 Ndugu wote walioko hapa wanawasalimu. Salimianeni kila mmoja wenu kwa salamu maalum ya watu wa Mungu.[d]

21 Hii ni salamu yangu kwa mkono wangu mwenyewe: Paulo.

22 Ikiwa mtu yeyote hampendi Bwana, mwacheni mtu huyo abaki chini ya laana ya Mungu.

Njoo, Ewe Bwana![e]

23 Neema ya Bwana Yesu iwe pamoja nanyi.

24 Upendo wangu uwe nanyi nyote katika Kristo Yesu.

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)

© 2017 Bible League International