Print Page Options
Previous Prev Day Next DayNext

Beginning

Read the Bible from start to finish, from Genesis to Revelation.
Duration: 365 days
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)
Version
Warumi 14-16

Msiwakosoe Wengine

14 Iweni tayari kuwakubali wenye mashaka kuhusu yale ambayo waamini wanaweza kufanya. Tena msibishane nao kuhusu mawazo yao tofauti. Baadhi ya watu wanaamini kuwa wanaweza kula aina yoyote ya chakula,[a] lakini wale walio na mashaka wanakula mboga za majani tu. Wale wanaojua kuwa wanaweza kula chakula cha aina yoyote hawapaswi kujisikia kuwa ni bora kuliko wale wanaokula mboga za majani tu. Na wale wanaokula mboga za majani tu hawapaswi kuamua kuwa wale wanaokula vyakula vyote wanakosea. Mungu amewakubali. Huwezi kuwahukumu watumishi wa mtu mwingine. Hilo linamhusu bwana wao mwenyewe ikiwa watafaulu au watashindwa. Na watakubaliwa, kwa sababu Bwana yuko tayari kuwafanya wafaulu.

Watu wengine wanaweza kuamini kuwa siku moja ni ya muhimu zaidi kuliko nyingine. Na wengine wanaweza kuwa na uhakika kuwa siku zote ziko sawa. Kila mtu anapaswa kujihakikisha juu ya imani yake katika akili zake wenyewe. Wale wanaofikiri kuwa siku moja ni ya muhimu kuliko siku zingine wanafanya hivyo kwa ajili ya Bwana. Na wale wanaokula vyakula vya aina zote wanafanya hivyo kwa ajili ya Bwana. Ndiyo, wanamshukuru Mungu kwa ajili ya chakula. Na wale wanaokataa kula vyakula fulani wanafanya hivyo kwa ajili ya Bwana. Nao pia wanamshukuru Mungu.

Hatuishi au kufa kwa ajili yetu sisi wenyewe tu. Kama tukiishi, tunaishi kwa ajili ya Bwana. Na kama tukifa, tunakufa kwa ajili ya Bwana. Hivyo kuishi au kufa, sisi ni mali ya Bwana. Ndiyo sababu Kristo alikufa na kuishi tena ili awe Bwana juu ya wote waliokufa na wanaoishi.

10 Hivyo kwa nini unamhukumu kaka au dada yako katika familia ya Mungu? Au kwa nini unafikiri kuwa wewe ni bora kuliko wao? Sote tutasimama mbele za Mungu, naye atatuhukumu sisi sote. 11 Ndiyo, Maandiko yanasema,

“‘Hakika kama niishivyo’, asema Bwana,
    ‘kila mtu atapiga magoti mbele zangu,
    na kila mtu atasema kuwa mimi ni Mungu.’”(A)

12 Hivyo kila mmoja wetu ataeleza kuhusu matendo yake mbele za Mungu.

Msisababishe Wengine Wakatenda Dhambi

13 Hivyo tuache kuhukumiana sisi kwa sisi. Tuamue kutokufanya kitu ambacho kitasababisha matatizo kwa kaka au dada au kuathiri imani zao. 14 Najua kuwa hakuna chakula ambacho kwa namna yake chenyewe hakifai kuliwa. Bwana Yesu ndiye aliyenithibitisha juu ya jambo hilo. Lakini ikiwa mtu ataamini kuwa si sahihi kula chakula fulani, basi kwake yeye huyo hiyo haitakuwa sahihi akila chakula hicho.

15 Ikiwa utamuumiza kaka au dada yako kwa sababu ya chakula unachokula, hutakuwa unaifuata njia ya upendo. Kristo alikufa kwa ajili yao. Hivyo usiwaharibu kwa kula kitu wanachofikiri kuwa si sahihi kula. 16 Usiruhusu kile ambacho ni chema kwako kiwe kitu watakachosema ni kiovu. 17 Maisha katika ufalme wa Mungu siyo juu ya kile tunachokula na kunywa. Ufalme wa Mungu ni juu ya njia sahihi ya kuishi, amani na furaha. Vyote hii vinatoka kwa Roho Mtakatifu. 18 Yeyote anayemtumikia Kristo kwa kuishi namna hii anampendeza Mungu na ataheshimiwa na wengine.

19 Hivyo tujitahidi kwa kadri tuwezavyo kufanya kile kinacholeta amani. Tufanye kile kitakachomsaidia kila mtu kujengeka kiimani. 20 Msiruhusu kula vyakula kuiharibu kazi ya Mungu. Vyakula vyote ni sahihi kula, lakini ni makosa kwa yeyote kula kitu kinachomletea shida kaka au dada katika familia ya Mungu. 21 Ni heri kutokula nyama au kunywa divai au kufanya kitu chochote kinachoumiza imani ya kaka au dada yako.

22 Ilindeni imani yenu kuhusu mambo haya kama siri kati yenu na Mungu. Ni baraka kufanya kile unachofikiri ni sahihi bila kujihukumu mwenyewe. 23 Lakini ikiwa unakula kitu bila kuwa na uhakika kuwa ni sahihi, unakosea. Hii ni kwa sababu hukuamini kuwa ni sahihi. Na ukifanya chochote unachoamini kuwa si sahihi, hiyo ni dhambi.

15 Baadhi yetu hatuna matatizo na mambo haya. Hivyo tunapaswa kuwa wastahimilivu kwa wale wasio imara na wenye mashaka. Hatupaswi kufanya yanayotupendeza sisi bali tufanye yale yanayowapendeza wao na kwa faida yao. Tufanye chochote kinachoweza kumsaidia kila mtu kujengeka katika imani. Hata Kristo hakuishi ili kijaribu kujifurahisha yeye mwenyewe. Kama Maandiko yanavyosema, “Matusi ambayo watu waliyatoa dhidi yako pia yalinifanya niteseke.”(B) Chochote kilichoandikwa zamani kiliandikwa ili kitufundishe sisi. Maandiko haya yaliandikwa ili yatupe matumaini yanayokuja kwa njia ya subira na kutia moyo kunakoletwa nayo. Subira na kuhimiza kote hutoka kwa Mungu. Na ninawaombea ili Mungu awasaidie muwe na nia ile ile ninyi kwa ninyi, kama ilivyo nia ya Kristo Yesu. Kisha ninyi nyote, kwa sauti moja, mtamtukuza Mungu na Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo. Kristo aliwakaribisha ninyi, hivyo nanyi mkaribishane ninyi kwa ninyi. Hili litaleta heshima[b] kwa Mungu. Ndiyo, haya ndiyo maneno yangu kwenu kwamba Kristo alifanyika mtumishi wa Wayahudi ili kuonesha kuwa Mungu amefanya yale aliyowaahidi baba zao wakuu. Na pia alifanya hivi ili wale wasio Wayahudi waweze kumsifu Mungu kwa rehema anazowapa. Maandiko yanasema,

“Hivyo nitakushukuru wewe katikati ya watu wa mataifa mengine;
    Nitaliimbia sifa jina lako.”(C)

10 Na Maandiko yanasema,

“Ninyi watu wa mataifa mengine furahini pamoja na watu wa Mungu.”(D)

11 Pia Maandiko yanasema,

“Msifuni Bwana ninyi watu wote wa mataifa mengine;
    watu wote na wamsifu Bwana.”(E)

12 Na Isaya anasema,

“Mtu mmoja atakuja kutoka katika ukoo wa Yese.[c]
    Atainuka na kutawala juu ya mataifa,
na wataweka matumaini yao kwake.”(F)

13 Naomba kwamba Mungu aletaye matumaini awajaze furaha na amani kadri mnavyomwamini yeye. Na hii isababishe tumaini lenu liongezeke hadi lifurike kabisa ndani yenu kwa nguvu za Roho Mtakatifu.

Paulo Azungumzia Kazi Yake

14 Kaka na dada zangu, najua pasipo mashaka kuwa mmejaa wema na mnayo maarifa yote mnayohitaji. Hivyo kwa hakika mnaweza kushauriana ninyi kwa ninyi. 15 Lakini nimewaandikia ninyi kwa ujasiri wote kuhusu mambo fulani niliyotaka mkumbuke. Nilifanya hivi kwa sababu Mungu alinipa karama hii maalumu: 16 kuwa mtumishi wa Kristo Yesu kwa ajili ya wasio Wayahudi. Natumika kama kuhani ambaye kazi yake ni kuhubiri Habari Njema kutoka kwa Mungu. Alinipa mimi jukumu hili ili ninyi msio Wayahudi mweze kuwa sadaka atakayoikubali, sadaka iliyotakaswa na Roho Mtakatifu.

17 Na hii ndiyo sababu najisikia vizuri kuhusu yale yote yaliyofanyika kwa ajili ya Mungu kwa kuwa mimi ni mali ya Kristo Yesu. 18 Sitazungumzia chochote nilichofanya mwenyewe. Nitazungumza tu kuhusu yale Kristo aliyofanya akinitumia mimi katika kuwaongoza wale wasiokuwa Wayahudi katika kutii. Ni yeye aliyetenda kazi katika yale niliyosema na kufanya. 19 Alitenda kazi kwa ishara za miujiza kwa nguvu ya Roho wa Mungu. Matokeo yake ni kuwa nimewahubiri watu Habari Njema kuhusu Kristo kuanzia Yerusalemu na kuzunguka kote mpaka Iliriko. Na hivyo nimemaliza sehemu hiyo ya wajibu wangu. 20 Imekuwa shabaha yangu daima kuzihubiri Habari Njema katika sehemu ambako watu hawajawahi kusikia juu ya Kristo. Nafanya hivi kwa sababu sitaki kujenga katika kazi ambayo tayari mtu mwingine amekwisha kuianza. 21 Kama Maandiko yanavyosema,

“Wale ambao hawakuambiwa kuhusu yeye wataona,
    na wale ambao hawajasikia juu yake wataelewa.”(G)

Mpango wa Paulo Kwenda Rumi

22 Kazi hiyo imenifanya niwe na shughuli nyingi sana na mara nyingi imenizuia kuja kuwaona.

23 Kwa miaka mingi nimetamani kuwatembelea, na sasa nimekamilisha kazi yangu katika maeneo haya. 24 Hivyo nitawatembelea nitakapoenda Hispania. Ndiyo, napanga kusafiri kwenda Hispania na natumaini kuwatembelea nikiwa njiani. Nitakaa kwa muda na kufurahi pamoja nanyi. Kisha natumaini mtanisaidia kuendelea na safari yangu.

25 Sasa ninakwenda Yerusalemu kuwasaidia watu wa Mungu huko. 26 Baadhi yao ni maskini, na waamini kule Makedonia na Akaya walitaka kuwasaidia. Hivyo walikusanya kiasi cha fedha ili wawatumie. 27 Walifurahia kufanya hivi. Na ilikuwa kama kulipa kitu fulani walichokuwa wakidaiwa, kwa sababu kama watu wasiokuwa Wayahudi walikuwa wamebarikiwa kiroho na Wayahudi. Hivyo nao wanapaswa kutumia baraka za vitu walivyonavyo kwa ajili ya kuwasaidia Wayahudi. 28 Naelekea Yerusalemu kuhakikisha kuwa maskini wanapokea fedha hizi zilizotolewa kwa ajili yao.

Nitakapokuwa nimekamilisha hilo, nitaondoka kuelekea Hispania na nikiwa njiani nitasimama ili niwaone. 29 Na ninajua kwamba nitakapowatembelea, nitakuja na baraka zote anazotoa Kristo.

30 Kaka na dada zangu, nawaomba mnisaidie katika kazi hii kwa kuniombea kwa Mungu. Fanyeni hivi kwa sababu ya Bwana wetu Yesu Kristo na pendo ambalo Roho anatupa. 31 Niombeeni ili niokolewe kutokana na wale walioko Yudea wanaokataa kuupokea ujumbe wetu. Pia ombeni kwamba msaada huu ninaoupeleka Yerusalemu utakubalika kwa watu wa Mungu huko. 32 Kisha, nitakuwa na furaha wakati nitakapokuja kuwaona, Mungu akipenda. Na ndipo tutaweza kufurahia muda wa kujengana sisi kwa sisi. 33 Mungu anayetoa amani awe pamoja nanyi nyote. Amina.

Paulo Anayo Mambo ya Mwisho ya Kusema

16 Napenda mjue kuwa mnaweza kumwamini dada yetu Foebe. Ni mtumishi maalum wa kanisa la kule Kenkrea. Nawaomba mmkaribishe kama yule aliye wa Bwana. Mkaribisheni kwa jinsi ambayo watu wa Mungu wanapaswa. Msaidieni kwa chochote atakachohitaji kutoka kwenu. Yeye amekuwa kiongozi anayeheshimika ambaye amewasaidia watu wengine wengi, pamoja na mimi.

Mpeni salamu Priska na Akila, ambao wametumika pamoja nami kwa ajili ya Kristo Yesu. Waliyahatarisha maisha yao wenyewe ili wayaokoe maisha yangu. Nawashukuru hao, na makanisa yote ya wasio Wayahudi yanawashukuru wao.

Vilevile, fikisheni salamu katika kanisa linalokusanyikia nyumbani mwao.

Msalimuni rafiki yangu mpendwa Epaineto. Alikuwa mtu wa kwanza kumfuata Kristo kule Asia. Pia msalimieni Mariamu ambaye alifanya kazi kwa juhudi kubwa kwa ajili yenu. Pia msalimieni Androniko na Yunia. Hao ni jamaa zangu, na walikuwa gerezani pamoja nami. Walikuwa wafuasi wa Kristo kabla yangu. Nao ni miongoni mwa wale walio muhimu sana waliotumwa na Kristo kuifanya kazi yake.[d]

Msalimuni Ampliato, rafiki yangu mpendwa miongoni mwa watu wa Bwana, na kwa Urbano. Aliyefanya kazi pamoja nasi kwa ajili ya Kristo. Pia fikisheni salamu kwa rafiki yangu mpendwa Stakisi

10 na Apele, aliyejithibitisha kuwa yeye ni mfuasi wa kweli wa Kristo.

Nisalimieni watu wote katika nyumba ya Aristobulo 11 na Herodioni, jamaa yangu.

Wasalimieni nyumba nzima ya Narkiso aliye wake Bwana 12 na Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa juhudi kubwa kwa ajili ya Bwana. Nisalimieni rafiki yangu mpendwa Persisi. Dada huyu amefanya kazi kwa juhudi kubwa kwa ajili ya Bwana.

13 Pia msalimieni Rufo, mmoja wa wateule wa Bwana, na mama yake, ambaye amefanyika mama yangu pia.

14 Fikisheni salamu kwa Asinkrito, Flegoni, Hermesi, Patroba, Herma na waamini wote walio pamoja nao.

15 Msalimieni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, Olimpa na watu wote wa Mungu walio pamoja nao.

16 Mpeni kila mmoja ile salamu maalum ya watu wa Mungu.[e]

Makanisa yote yaliyo ya Kristo yanatuma salamu zao kwenu.

17 Kaka na dada zangu, ninataka muwe macho na wale wanaosababisha mabishano na kuumiza imani za watu kwa kufundisha mambo ambayo ni kinyume cha yale mliyojifunza. Mjitenge nao. 18 Watu wa namna hiyo hawamtumikii Kristo Bwana wetu. Wanajifurahisha wenyewe tu. Wanatumia mazungumzo matamu na kusema mambo yanayopendeza ili kuwadanganya wale wasiojua kuhusu uovu. 19 Kila mtu amesikia juu ya utii wenu kwa Bwana, nami nafurahi sana juu ya hilo. Lakini ninataka muwe werevu kuhusu yaliyo mema na kutokujua lolote kuhusu yaliyo maovu.

20 Mungu mwenye kuleta amani atamwangamiza Shetani mapema na kuwapa nguvu juu yake.

Neema ya Bwana wetu Yesu iwe pamoja nanyi.

21 Timotheo, mtumishi pamoja nami, anawatumieni salamu. Pia Lukio, Yasoni na Sosipatro (hawa ni jamaa zangu) wanawatumieni salamu.

22 Mimi Tertio, ninayeandika barua hii kwa ajili ya Paulo. Ninawasalimu kama mmoja aliye wa Bwana.

23 Gayo ameniruhusu na kanisa lote hapa kuitumia nyumba yake. Anawatumia salamu zake. Erasto na kaka yetu Kwarto pia wanatuma salamu. Erasto ndiye mtunza hazina wa mji hapa. 24 [f]

25 Atukuzwe Mungu! Yeye ndiye anayeweza kuzitumia Habari Njema ninazozifundisha kuwaimarisha katika imani. Ni ujumbe ninaowaambia watu kuhusu Yesu Kristo. Ujumbe huo ni siri ya ukweli iliyofichwa kwa karne nyingi sana lakini sasa imefunuliwa. 26 Na kweli hiyo sasa imeonyeshwa kwetu. Ilijulishwa kwa yale ambayo manabii waliandika katika Maandiko, kama Mungu wa milele alivyoagiza. Na sasa imejulikana kwa mataifa yote ili waweze kuamini na kumtii yeye. 27 Utukufu wa milele ni kwa Mungu mwenye hekima pekee kwa njia ya Yesu Kristo. Amina.

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)

© 2017 Bible League International