Print Page Options
Previous Prev Day Next DayNext

Beginning

Read the Bible from start to finish, from Genesis to Revelation.
Duration: 365 days
Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)
Version
Matendo 21

Paulo Aenda Yerusalemu

21 Baada ya kuwaaga wazee tulitweka tanga moja kwa moja kwenda kwenye kisiwa cha Kosi. Siku iliyofuata tulikwenda kisiwa cha Rhode na kutoka pale tulikwenda Patara. Tulipata meli hapo iliyokuwa inakwenda maeneo ya Foeniki. Tukapanda meli na tukatweka tanga kuondoka.

Tulitweka tanga na kusafiri karibu na kisiwa cha Kipro. Tuliweza kukiona upande wa kaskazini, lakini hatukusimama. Tulisafiri mpaka katika jimbo la Shamu. Tulisimama Tiro kwa sababu meli ilitakiwa kupakua mizigo yake pale. Tuliwapata wafuasi wa Bwana pale na tukakaa pamoja nao kwa siku saba. Walimuonya Paulo asiende Yerusalemu kwa sababu ya kile walichoambiwa na Roho Mtakatifu. Lakini muda wetu wa kukaa pale ulipokwisha, tulirudi kwenye meli na kuendelea na safari yetu. Wafuasi wote, hata wanawake na watoto walikuja pamoja nasi pwani. Tulipiga magoti ufukweni sote, tukaomba, na tukaagana. Kisha tukaingia melini, na wafuasi wa Bwana wakarudi nyumbani.

Tuliendelea na safari yetu kutoka Tiro na kwenda katika mji wa Ptolemai. Tuliwasalimu waamini pale na kukaa nao kwa siku moja. Siku iliyofuata tuliondoka Ptolemai na kwenda katika mji wa Kaisaria. Tulikwenda nyumbani kwa Filipo na kukaa kwake, alikuwa mhubiri wa Habari Njema. Alikuwa mmoja wa wasaidizi saba.[a] Alikuwa na mabinti wanne mabikira waliokuwa na karama ya kutabiri.

10 Baada ya kuwa pale kwa siku kadhaa, nabii aliyeitwa Agabo alikuja kutoka Uyahudi. 11 Alikuja Kwetu na kuazima mkanda wa Paulo. Aliutumia mkanda huo na akajifunga mikono na miguu yake mwenyewe. Kisha akasema, “Roho Mtakatifu ananiambia, ‘Hivi ndivyo ambavyo Wayahudi walioko Yerusalemu watamfunga mtu anayeuvaa mkanda[b] huu. Kisha watamkabidhi kwa watu wasiomjua Mungu.’”

12 Tuliposikia hili, sisi na wafuasi wengine pale tukamsihi Paulo asiende Yerusalemu. 13 Lakini Paulo alisema, “Kwa nini mnalia na kunihuzunisha? Niko radhi kufungwa Yerusalemu. Niko tayari hata kufa kwa ajili ya jina la Bwana Yesu!”

14 Hatukuweza kumshawishi asiende Yerusalemu. Hivyo tuliacha kumsihi na tukasema, “Tunaomba lile alitakalo Bwana lifanyike.”

15 Baada ya hili, tulijiandaa na kuelekea Yerusalemu. 16 Baadhi ya Wafuasi wa Yesu kutoka Kaisaria walikwenda pamoja nasi. Wafuasi hawa walitupeleka nyumbani kwa Mnasoni, mtu kutoka Kipro, ambaye alikuwa mmoja wa watu wa kwanza kuwa wafuasi wa Yesu. Walitupeleka nyumbani kwake ili tukae pamoja naye.

Paulo Amtembelea Yakobo

17 Ndugu na dada wa Yerusalemu walitukabisha kwa furaha sana walipotuona. 18 Siku iliyofuata Paulo alikwenda pamoja nasi kumtembelea Yakobo. Wazee wote walikuwepo pia. 19 Baada ya kuwasalimu, Paulo aliwaambia hatua kwa hatua yote ambayo Mungu aliyatenda katikati ya watu wasio Wayahudi kupitia huduma yake.

20 Viongozi waliposikia hili, wakamsifu Mungu. Kisha wakamwambia Paulo, “Ndugu yetu, unaweza kuona maelfu ya Wayahudi wamekuwa waamini, lakini wanadhani ni muhimu kutii Sheria ya Musa. 21 Wameambiwa kuwa unawafundisha Wayahudi wanaoishi katika majimbo yasiyo ya Kiyahudi kuacha kufuata Sheria ya Musa. Wamesikia kuwa unawaambia wasiwatahiri watoto wao na wasifuate desturi zetu.

22 Tufanye nini? Wafuasi wayahudi hapa watajua kuwa umekuja. 23 Hivyo tutakwambia nini cha kufanya: Watu wanne miongoni mwa watu wetu wameweka nadhiri[c] kwa Mungu. 24 Wachukue watu hawa walio pamoja nawe na ushiriki katika ibada ya utakaso.[d] Lipia gharama zao ili wanyoe nywele za vichwa vyao. Hili litathibitisha kwa kila mmoja kuwa mambo waliyosikia kuhusu wewe si sahihi. Watajua kuwa wewe mwenyewe unaitii Sheria ya Musa katika maisha yako.

25 Tumekwisha watumia barua waamini wasio Wayahudi kuwaambia ambayo hawapaswi kufanya:

‘Wasile chakula kilichotolewa kwa sanamu.

Wasile nyama inayotokana na wanyama walionyongwa au nyama zilizo na damu ndani yake.

Wasijihusishe na uzinzi.’”

Paulo Akamatwa

26 Hivyo Paulo akawachukua wale watu wanne aliokuwa pamoja nao. Siku iliyofuata alishiriki kwenye ibada ya kuwatakasa. Kisha akaenda eneo la Hekalu na kutangaza siku ya mwisho ambapo kipindi cha utakaso kitakwisha na kwamba sadaka ingetolewa kwa ajili ya kila mmoja wa watu hao siku hiyo.

27 Siku saba zilipokuwa zinakaribia kumalizika, baadhi ya Wayahudi kutoka Asia walimwona Paulo katika eneo la Hekalu. Wakamshawishi kila mtu, kisha wakakusanyika kama kundi wakiwa na hasira, kisha wakamkamata Paulo 28 na wakapiga kelele wakisema, “Watu wa Israeli, tusaidieni! Huyu ndiye mtu anayefundisha mambo yaliyo kinyume na Sheria ya Musa, kinyume na watu wetu, na kinyume na Hekalu letu. Hivi ndivyo anavyowafundisha watu kila mahali. Na sasa amewaleta baadhi ya Wayunani katika eneo la Hekalu na amepanajisi mahali hapa patakatifu!” 29 (Wayahudi walisema hili kwa kuwa walimwona Trofimo akiwa na Paulo Yerusalemu. Trofimo alikuwa mwenyeji wa Efeso, Wayahudi walidhani kuwa Paulo alikuwa amempeleka eneo takatifu la Hekalu.)

30 Watu katika mji wote wakajaa hasira, na kila mtu akaja akikimbilia kwenye Hekalu. Wakamkamata Paulo na kumtoa nje ya eneo takatifu, malango ya Hekalu yakafungwa saa hiyo hiyo. 31 Walipokuwa wanajaribu kumwua Paulo, Kamanda wa jeshi la Rumi katika mji wa Yerusalemu akapata taarifa kuwa ghasia zilikuwa zimeenea mji wote. 32 Mara hiyo hiyo kamanda alikimbilia mahali ambako umati wa watu ulikuwa umekusanyika, aliwachukua baadhi ya maofisa wa jeshi na askari. Watu walipomwona kamanda na askari wake waliacha kumpiga Paulo.

33 Kamanda alikwenda mahali alipokuwa Paulo na akamkamata. Akawaambia askari wake wamfunge kwa minyororo miwili. Kisha akauliza, “Mtu huyu ni nani? Amefanya nini kibaya?” 34 Baadhi ya watu pale walipiga kelele wakisema kitu hiki na wengine walisema kingine. Kwa sababu ya kuchanganyikiwa huku na kelele kamanda hakujua ukweli kuhusu kilichotokea. Hivyo akawaambia askari wamchukue Paulo mpaka kwenye jengo la jeshi. 35-36 Umati wote ulikuwa unawafuata. Askari walipofika kwenye ngazi ilibidi wambebe Paulo. Walifanya hivi ili kumlinda, kwa sababu watu walikuwa tayari kumwumiza. Watu walikuwa wanapiga kelele wakisema, “Auawe!”

37 Askari walipokuwa tayari kumwingiza Paulo kwenye jengo la jeshi, Paulo alimwuliza kamanda akasema, “Je, ninaweza kukwambia kitu?”

Kamanda akasema, “Kumbe, unaongea Kiyunani? 38 Kwa hiyo wewe si mtu niliyemdhania. Nilidhani wewe ni Mmisri aliyeanzisha vurugu dhidi ya serikali siku si nyingi na akawaongoza magaidi elfu nne kwenda jangwani.”

39 Paulo akasema, “Hapana, Mimi ni Myahudi kutoka Tarso katika jimbo la Kilikia. Ni raia wa mji ule muhimu. Tafadhali niruhusu niseme na watu.”

40 Kamanda akamwambia Paulo unaweza kusema. Hivyo Paulo akasimama kwenye ngazi na kupunga mkono wake ili watu wanyamaze. Watu walinyamaza na Paulo akaanza kusema nao kwa Kiaramu.

Paulo Azungumza Mbele za Watu

22 Paulo akasema, “Baba zangu na kaka zangu, nisikilizeni! Nitajitetea kwenu.”

Wayahudi walipomsikia Paulo anazungumza kwa Kiaramu wakanyamaza. Kisha Paulo akasema,

“Mimi ni Myahudi, nilizaliwa katika mji wa Tarso katika jimbo la Kilikia. Nilikulia hapa katika mji huu. Nilikuwa mwanafunzi wa Gamalieli[e] ambaye kwa umakini alinifundisha kila kitu kuhusu sheria ya baba zetu. Daima nimekuwa na shauku ya kumheshimu Mungu, sawa na ninyi nyote hapa leo. Niliwatesa watu walioifuata Njia. Baadhi yao hapa waliuawa kwa sababu yangu. Niliwakamata wanaume na wanawake na kuwaweka gerezani.

Kuhani mkuu na baraza lote la wazee wa Wayahudi wanaweza kuwathibitishia hili. Wakati mmoja viongozi hawa walinipa barua. Barua hizo waliandikiwa ndugu zetu Wayahudi katika mji wa Dameski. Nilikuwa naenda huko kuwakamata wafuasi wa Yesu na kuwaleta Yerusalemu ili waadhibiwe.

Paulo Aeleza Kuhusu Kuokolewa Kwake

Lakini kitu fulani kilinitokea nikiwa njiani kwenda Dameski. Ilipokuwa inakaribia mchana na nilikuwa karibu na mji wa Dameski. Ghafla mwanga kutoka mbinguni ulining'aria kunizunguka. Nilianguka chini na nikasikia sauti ikiniambia, ‘Sauli, Sauli kwa nini unanitesa?’

Niliuliza, ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Sauti ikasema, ‘Mimi ni Yesu kutoka Nazareti, unayemtesa.’ Watu waliokuwa pamoja nami hawakuisikia sauti lakini waliona mwanga.

10 Nilisema, ‘Nifanye nini Bwana?’ Bwana alinijibu, ‘Simama na uingie Dameski. Humo utawaambia yote niliyopanga uyafanye.’ 11 Sikuweza kuona kwa sababu mwanga ule angavu ulinilemaza macho. Hivyo wale watu waliokuwa pamoja nami waliniongoza kuingia mjini Dameski.

12 Alikuwepo mtu mmoja katika mji wa Dameski aliyeitwa Anania.[f] Mtu huyu alikuwa mcha Mungu na aliitii Sheria ya Musa na Wayahudi wote walioishi kule walimheshimu. 13 Alikuja kwangu na kuniambia, ‘Sauli, ndugu yangu, tazama juu na uone tena!’ Ghafla niliweza kumwona.

14 Anania aliniambia, ‘Mungu yule yule aliyeabudiwa na baba zetu alikuchagua wewe tangu zamani kuujua mpango wake. Amekuchagua wewe kumwona Mwenye Haki wake na kusikia maneno kutoka kwake. 15 Utakuwa shahidi wake kwa watu wote. Utawaambia ulichoona na kusikia. 16 Sasa usisubiri zaidi. Simama, ubatizwe na usafishwe dhambi zako, mwamini Yesu ili akuokoe.’[g]

17 Baadaye, nilirudi Yerusalemu. Nilipokuwa naomba katika eneo la hekalu, nikaona maono. 18 Nilimwona Yesu, naye akaniambia, ‘Haraka, ondoka Yerusalemu sasa hivi! Watu hapa hawataukubali ukweli unaowaambia kuhusu mimi.’

19 Nilisema, ‘Lakini, Bwana, Wayahudi wanajua kuwa mimi ndiye niliyewafunga gerezani na kuwapiga wale wanaokuamini wewe. Nilikwenda kwenye masinagogi yote kuwatafuta na kuwakamata Wayahudi wanaokuamini wewe. 20 Watu wanajua pia kuwa nilikuwepo wakati Stefano shahidi wako, alipouawa. Nilisimama pale na kukubaliana nao kuwa wamwue. Nilishikilia hata mavazi ya watu waliokuwa wanamwua!’

21 Lakini Yesu akaniambia, ‘Ondoka sasa. Nitakutuma mbali sana kwa watu wasio Wayahudi.’”

22 Watu waliacha kusikiliza Paulo aliposema jambo hili la mwisho. Walipasa sauti wote, wakisema, “Mwondosheni mtu huyu! Hastahili kuishi katika dunia hii tena.” 23 Waliendelea kupiga kelele, wakichana nguo zao na kurusha mavumbi juu.[h] 24 Ndipo kamanda akawaambia askari wamwingize Paulo kwenye jengo la jeshi na wampige. Alitaka kumlazimisha Paulo aeleze ni kwa nini watu walikuwa wanampigia kelele namna ile. 25 Askari walipokuwa wanamfunga Paulo, wakijiandaa kumpiga alimwuliza ofisa wa jeshi, “Je, mna haki ya kumpiga raia wa Rumi[i] ambaye hajathibitika kuwa na hatia?”

26 Ofisa aliposikia hili, alikwenda kwa kamanda na kumwambia. Ofisa alisema, “Unafahamu unalolifanya? Mtu huyu ni raia wa Rumi!”

27 Kamanda akaenda kwa Paulo na kusema, “Niambie kwa hakika, ‘Je, wewe ni raia wa Rumi?’”

Paulo akajibu, “Ndiyo.”

28 Kamanda akasema, “Nililipa pesa nyingi kuwa raia wa Rumi.”

Lakini Paulo akasema, “Nilizaliwa raia wa Rumi.”

29 Ghafla watu waliokuwa wanajiandaa kumwuliza maswali Paulo waliondoka. Kamanda aliogopa kwa sababu alikuwa ameshamfunga Paulo kwa minyororo na ni raia wa Rumi.

Paulo Aongea na Viongozi wa Kiyahudi

30 Siku iliyofuata kamanda alitaka kujua ni kwa nini Wayahudi wanamshitaki Paulo. Hivyo aliamuru viongozi wa makuhani na baraza kuu lote kukutana pamoja. Alimfungua Paulo minyororo na kumleta mbele ya baraza.

23 Paulo aliwatazama wajumbe wa baraza na kusema, “Ndugu zangu, Nimeishi maisha yangu katika njia nzuri mbele za Mungu. Daima nimefanya yale niliyodhani ni haki.” Anania,[j] kuhani mkuu alikuwa pale. Aliposikia hili, aliwaambia watu waliokuwa wamesisima karibu na Paulo wampige kwenye mdomo. Paulo akamwambia Anania, “Mungu atakupiga wewe pia! Wewe ni kama ukuta mchafu uliopakwa rangi nyeupe. Umeketi hapa na kunihukumu, ukitumia Sheria ya Musa. Lakini unawaambia wanipige wakati ni kinyume cha sheria.”

Watu waliokuwa wamesimama karibu na Paulo wakamwambia, “Una uhakika unataka kumtukana kuhani mkuu wa Mungu namna hiyo?”

Paulo akasema, “Ndugu zangu, sikufahamu kuwa mtu huyu ni kuhani mkuu. Maandiko yanasema, ‘Usiseme mambo mabaya kuhusu kiongozi wa watu wako.’”(A)

Paulo alijua kuwa baadhi ya watu kwenye baraza lile ni Masadukayo na baadhi yao ni Mafarisayo. Hivyo akapaza sauti akasema, “Ndugu zangu, Mimi ni Farisayo na baba yangu ni Farisayo! Nimeshitakiwa hapa kwa sababu ninaamini kuwa watu watafufuka kutoka kwa wafu.”

Paulo alipolisema hili, mabishano makubwa yakaanza kati ya Mafarisayo na Masadukayo. Baraza likagawanyika. (Masadukayo hawaamini katika ufufuo, malaika au roho. Lakini Mafarisayo wanaamini vyote.) Wayahudi hawa wote wakaanza kubishana kwa kupaza sauti. Baadhi ya walimu wa sheria, waliokuwa Mafarisayo wakasimama na kusema, “Hatuoni kosa lolote kwa mtu huyu. Inawezekana kwa hakika malaika au roho alizungumza naye.”

10 Mabishano yaligeuka kuwa mapigano na kamanda aliogopa kwamba Wayahudi wangempasua Paulo vipande vipande. Hivyo akawaambia askari wateremke, wamwondoe Paulo na kumweka mbali na Wayahudi hao katika jengo la jeshi.

11 Usiku uliofuata Bwana Yesu akaja na kusimama pembeni mwa Paulo. Akamwambia, “Uwe jasiri! Umewaambia watu kuhusu mimi humu Yerusalemu. Ni lazima ufanye vivyo hivyo Rumi.”

Baadhi ya Wayahudi Wapanga Kumwua Paulo

12 Asubuhi iliyofuata baadhi ya Wayahudi walifanya mpango wa kumwua Paulo. Walijiapiza kuwa hawatakula wala kunywa kitu chochote mpaka watakapomwua Paulo. 13 Walikuwa watu zaidi ya 40 waliofanya mpango huu. 14 Walikwenda wakaongea na viongozi wa makuhani na viongozi wa wazee wa Wayahudi. Walisema, “Tumejiwekea nadhiri kwamba hatutakula wala kunywa mpaka tumemwua Paulo. 15 Tunataka mfanye hivi: Mtumieni kamanda ujumbe kutoka kwenu na baraza kuu. Mwambieni mnamtaka amlete Paulo kwenu. Semeni kwamba mnataka kumwuliza maswali zaidi, tutamwua akiwa njiani kuja hapa.”

16 Lakini mpwaye Paulo aliusikia mpango huu. Alikwenda kwenye jengo la jeshi na kumwambia Paulo. 17 Kisha Paulo akamwita mmoja wa maofisa wa jeshi na kumwambia, “Mchukue huyu kijana kwa kamanda. Ana ujumbe kwa ajili yake.” 18 Hivyo ofisa wa jeshi akampeleka mpwaye Paulo kwa kamanda. Ofisa wa jeshi akasema, “Mfungwa Paulo ameniomba nimlete kijana huyu kwako. Ana kitu cha kukueleza.”

19 Kamanda akamchukua kijana na kwenda naye mahali ambapo wangekuwa peke yao. Kamanda akamwuliza, “Unataka kuniambia nini?”

20 Kijana akasema, “Baadhi ya Wayahudi wameamua kukuomba umpeleke Paulo kwenye mkutano wa baraza lao kesho. Wanataka wewe udhani kuwa wamepanga kumwuliza Paulo maswali zaidi. 21 Lakini usiwaamini! Zaidi ya watu 40 miongoni mwao wamejificha na wanasubiri kumwua. Wote wameweka nadhiri kuwa hawatakula wala kunywa mpaka wamemwua Paulo. Sasa hivi wanasubiri wewe ukubali.”

22 Kamanda akamtoa kijana, akamwambia, “Usimwambie yeyote kuwa umeniambia kuhusu mpango wao.”

Paulo Apelekwa Kaisaria

23 Ndipo Kamanda akawaita maofisa wawili wa jeshi. Akawaambia, “Ninataka baadhi ya watu kwenda Kaisaria. Andaeni askari mia mbili. Pia andaeni askari sabini waendao kwa farasi na mia mbili wa kubeba mikuki. Iweni tayari kuondoka saa tatu usiku. 24 Andaeni baadhi ya farasi kwa ajili ya Paulo kuendesha ili aweze kupelekwa kwa Gavana Feliki salama.” 25 Kamanda aliandika barua kuhusu Paulo. Hivi ndivyo alivyosema:

26 Kutoka kwa Klaudio Lisiasi.

Kwenda kwa Mheshimiwa Gavana Feliki.

Salamu:

27 Baadhi ya Wayahudi walimkamata mtu huyu na walikuwa karibu ya kumwua. Lakini nilipogundua kuwa ni raia wa Rumi, nilikwenda pamoja na askari wangu tukamwokoa. 28 Nilitaka kufahamu kwa nini walikuwa wanamshitaki. Hivyo nikampeleka kwenye mkutano wa baraza lao. 29 Hivi ndivyo nilivyoona: Wayahudi walisema mtu huyu alifanya mambo mabaya. Lakini mashitaka haya yalihusu sheria zao za Kiyahudi, na hakukuwa kosa lolote linaloweza kusababisha kufungwa au kifo. 30 Nimeambiwa kuwa baadhi ya Wayahudi walikuwa wanafanya mpango wa kumwua. Hivyo nimeamua kumleta kwako. Pia nimewaambia Wayahudi hao wakwambie walichonacho dhidi yake.

31 Askari walifanya kile walichoambiwa. Walimchukua Paulo na kumpeleka kwenye mji wa Antipatri usiku ule. 32 Siku iliyofuata askari wa farasi walikwenda na Paulo mpaka Kaisaria, lakini askari wengine na wale wa mikuki walirudi kwenye jengo la jeshi mjini Yerusalemu. 33 Askari wa farasi waliingia Kaisaria, wakampa barua Gavana Feliki, kisha wakamkabidhi Paulo kwake.

34 Gavana akaisoma barua na kumwuliza Paulo, “Unatoka jimbo gani?” Gavana alitambua kuwa Paulo alikuwa anatoka Kilikia. 35 Gavana akasema, “Nitakusikiliza Wayahudi wanaokushitaki watakapokuja hapa pia.” Kisha gavana akaamuru Paulo awekwe kwenye jumba la kifalme. (Jengo hili lilijengwa na Herode.)

Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi (TKU)

© 2017 Bible League International