Book of Common Prayer
Babeli Inaangamizwa
18 Kisha nikaona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni. Malaika huyu alikuwa na nguvu kuu. Utukufu wa malaika ukaing'arisha dunia. 2 Malaika akapaza sauti akasema:
“Ameteketezwa!
Mji mkuu Babeli umeteketezwa!
Umekuwa nyumba ya mapepo.
Mji ule umekuwa najisi.
Mji uliojaa kila aina ya ndege najisi.
Ni mahali ambapo kila mnyama najisi
na anayechukiwa anaishi.
3 Watu wote wa dunia wamekunywa mvinyo
wa uzinzi wake na ghadhabu ya Mungu.
Watawala wa dunia walizini pamoja naye,
na wafanya biashara wa ulimwengu walitajirika
kutokana na utajiri wa anasa zake.”
4 Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni ikisema:
“Enyi watu wangu, tokeni katika mji huo,
ili msishiriki katika dhambi zake.
Ili msiteseke kwa adhabu yoyote kuu atakayoipata.
5 Dhambi za mji huo zimerundikana na kufika mbinguni.
Mungu hajasahau makosa aliyotenda.
6 Upeni mji huo sawasawa na ulivyowapa wengine.
Mlipeni mara mbili kadiri ya alivyotenda.
Mwandalieni mvinyo ulio na nguvu mara mbili
ya mvinyo aliowaandalia wengine.
7 Alijipa utukufu mwingi na kuishi kitajiri.
Mpeni mateso mengi na huzuni nyingi.
Kama vile utukufu na starehe aliyoifurahia.
Hujisemea mwenyewe, ‘Mimi ni malkia nikaaye kwenye kiti changu cha enzi.
Mimi si mjane;
Sitakuwa na huzuni.’
8 Hivyo katika siku moja atateseka
kwa njaa kuu, maombolezo na kifo.
Atateketezwa kwa moto,
kwa sababu Bwana Mungu anayemhukumu ni mwenye nguvu.”
9 Watawala wa dunia waliozini pamoja naye na kushiriki utajiri wake watakapoona moshi wa kuungua kwake, watalia na kuhuzunika kwa sababu ya kifo chake. 10 Wataogopa mateso yake na kukaa mbali sana. Watasema:
“Inatisha! Inatisha sana, Ee mji mkuu,
ee Babeli, mji wenye nguvu!
Adhabu yako imekuja katika saa moja!”
11 Na wafanya biashara wa dunia watalia na kuhuzunika kwa ajili yake. Watahuzunika kwa sababu hakutakuwa hata mmoja wa kununua vitu wanavyouza; 12 dhahabu, fedha, vito, lulu, nguo za kitani safi, nguo za zambarau, hariri na nguo nyekundu, aina zote za mti wa udi, na aina zote za vitu vilivyotengenezwa kutokana na pembe za wanyama, miti ya thamani, shaba, chuma, na marimari. 13 Na mdalasini, viungo, uvumba, marhamu, ubani, mvinyo, mafuta ya mzeituni, unga safi, ngano, ng'ombe, kondoo, farasi, magari na watumwa, ndiyo hata maisha ya watu. Wafanya biashara watalia na kusema:
14 “Ee Babeli, mambo mazuri uliyoyataka yamekuacha.
Utajiri wako wote na vitu vya fahari vimetoweka.
Hautakuwa navyo tena.”
Je, ni Sahihi Kuponya Siku ya Sabato?
14 Siku moja ya Sabato Yesu alikwenda nyumbani kwa miongoni mwa viongozi wa Mafarisayo kula chakula pamoja naye. Watu wote mahali pale walikuwa wanamwangalia kwa makini kuona atafanya nini. 2 Mbele yake kulikuwa na mtu aliyekuwa na ugonjwa mbaya.[a] 3 Yesu akawauliza wanasheria na Mafarisayo, “Je, ni halali au kosa kuponya siku ya Sabato?” 4 Lakini walishindwa kujibu swali lake. Hivyo akamshika yule mgonjwa, na kumponya, akamruhusu aende zake. 5 Kisha akawaambia Mafarisayo na wanasheria, “Ikiwa mwanao au mnyama wako atatumbukia kisimani siku ya Sabato, mnatambua kuwa mtamtoa haraka.” 6 Mafarisayo na wanasheria hawakuweza kujibu kinyume na alivyosema.
Usijifanye Mtu wa Muhimu
7 Ndipo Yesu akagundua kuwa baadhi ya wageni walikuwa wanachagua sehemu za heshima za kukaa mezani. Ndipo akawaambia, 8 “Ukialikwa na mtu katika sherehe ya harusi, usikae katika sehemu za heshima. Wanaweza kuwa wamemwalika mtu muhimu kuliko wewe. 9 Na kama umekaa katika kiti muhimu zaidi, watakuja kwako na kukuambia ‘toka ulipokaa umpishe huyu!’ Ndipo itakulazimu kuhamia sehemu zisizo za heshima na utaaibika.
10 Hivyo ukialikwa, nenda ukae mahali pasipo pa heshima, ili yule aliyekualika akija, akuambie, ‘Rafiki, njoo huku mbele zaidi mahali pazuri.’ Ndipo utaheshimiwa mbele ya wageni wote walio mezani pamoja nawe. 11 Kila ajikwezaye atashushwa. Lakini ajishushaye atakwezwa.”
© 2017 Bible League International