Book of Common Prayer
37 Askari walipokuwa tayari kumwingiza Paulo kwenye jengo la jeshi, Paulo alimwuliza kamanda akasema, “Je, ninaweza kukwambia kitu?”
Kamanda akasema, “Kumbe, unaongea Kiyunani? 38 Kwa hiyo wewe si mtu niliyemdhania. Nilidhani wewe ni Mmisri aliyeanzisha vurugu dhidi ya serikali siku si nyingi na akawaongoza magaidi elfu nne kwenda jangwani.”
39 Paulo akasema, “Hapana, Mimi ni Myahudi kutoka Tarso katika jimbo la Kilikia. Ni raia wa mji ule muhimu. Tafadhali niruhusu niseme na watu.”
40 Kamanda akamwambia Paulo unaweza kusema. Hivyo Paulo akasimama kwenye ngazi na kupunga mkono wake ili watu wanyamaze. Watu walinyamaza na Paulo akaanza kusema nao kwa Kiaramu.
Paulo Azungumza Mbele za Watu
22 Paulo akasema, “Baba zangu na kaka zangu, nisikilizeni! Nitajitetea kwenu.”
2 Wayahudi walipomsikia Paulo anazungumza kwa Kiaramu wakanyamaza. Kisha Paulo akasema,
3 “Mimi ni Myahudi, nilizaliwa katika mji wa Tarso katika jimbo la Kilikia. Nilikulia hapa katika mji huu. Nilikuwa mwanafunzi wa Gamalieli[a] ambaye kwa umakini alinifundisha kila kitu kuhusu sheria ya baba zetu. Daima nimekuwa na shauku ya kumheshimu Mungu, sawa na ninyi nyote hapa leo. 4 Niliwatesa watu walioifuata Njia. Baadhi yao hapa waliuawa kwa sababu yangu. Niliwakamata wanaume na wanawake na kuwaweka gerezani.
5 Kuhani mkuu na baraza lote la wazee wa Wayahudi wanaweza kuwathibitishia hili. Wakati mmoja viongozi hawa walinipa barua. Barua hizo waliandikiwa ndugu zetu Wayahudi katika mji wa Dameski. Nilikuwa naenda huko kuwakamata wafuasi wa Yesu na kuwaleta Yerusalemu ili waadhibiwe.
Paulo Aeleza Kuhusu Kuokolewa Kwake
6 Lakini kitu fulani kilinitokea nikiwa njiani kwenda Dameski. Ilipokuwa inakaribia mchana na nilikuwa karibu na mji wa Dameski. Ghafla mwanga kutoka mbinguni ulining'aria kunizunguka. 7 Nilianguka chini na nikasikia sauti ikiniambia, ‘Sauli, Sauli kwa nini unanitesa?’
8 Niliuliza, ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Sauti ikasema, ‘Mimi ni Yesu kutoka Nazareti, unayemtesa.’ 9 Watu waliokuwa pamoja nami hawakuisikia sauti lakini waliona mwanga.
10 Nilisema, ‘Nifanye nini Bwana?’ Bwana alinijibu, ‘Simama na uingie Dameski. Humo utawaambia yote niliyopanga uyafanye.’ 11 Sikuweza kuona kwa sababu mwanga ule angavu ulinilemaza macho. Hivyo wale watu waliokuwa pamoja nami waliniongoza kuingia mjini Dameski.
12 Alikuwepo mtu mmoja katika mji wa Dameski aliyeitwa Anania.[b] Mtu huyu alikuwa mcha Mungu na aliitii Sheria ya Musa na Wayahudi wote walioishi kule walimheshimu. 13 Alikuja kwangu na kuniambia, ‘Sauli, ndugu yangu, tazama juu na uone tena!’ Ghafla niliweza kumwona.
14 Anania aliniambia, ‘Mungu yule yule aliyeabudiwa na baba zetu alikuchagua wewe tangu zamani kuujua mpango wake. Amekuchagua wewe kumwona Mwenye Haki wake na kusikia maneno kutoka kwake. 15 Utakuwa shahidi wake kwa watu wote. Utawaambia ulichoona na kusikia. 16 Sasa usisubiri zaidi. Simama, ubatizwe na usafishwe dhambi zako, mwamini Yesu ili akuokoe.’[c]
Yesu Achagua Wanafunzi Wake Kumi na Wawili
(Mt 10:1-4; Mk 3:13-19)
12 Siku chache baadaye, Yesu alikwenda mlimani kuomba. Alikaa huko usiku kucha akimwomba Mungu. 13 Asubuhi iliyofuata aliwaita wafuasi wake, akachagua kumi na wawili miongoni mwao na kuwaita Mitume. Nao ni:
14 Simoni (ambaye Yesu alimwita Petro),
Andrea aliyekuwa kaka yake Petro,
Yakobo,
Yohana,
Filipo,
Bartholomayo,
15 Mathayo na
Tomaso,
Yakobo mwana wa Alfayo,
Simoni aliyeitwa Mzelote,
16 Yuda mwana wa Yakobo,
na Yuda Iskariote (yule ambaye baadaye alimsaliti Yesu).
Yesu Afundisha na Kuponya Watu
(Mt 4:23-25; 5:1-12)
17 Yesu na mitume wakatelemka kutoka mlimani. Yesu akasimama mahali tambarare. Kundi kubwa la wafuasi wake lilikuwa pale. Walikuwepo pia watu wengi waliotoka sehemu zote za Uyahudi, Yerusalemu, na maeneo ya pwani karibu na Tiro na Sidoni. 18 Wote walikuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao. Aliwaponya watu waliokuwa wanasumbuliwa na mapepo. 19 Kila mtu alijaribu kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa unamtoka. Yesu aliwaponya wote.
20 Yesu akawatazama wafuasi wake na kusema,
“Heri ninyi mlio maskini.
Maana Ufalme wa Mungu ni wenu.
21 Heri ninyi mlio na njaa sasa.
Maana mtashibishwa.
Heri ninyi mnaolia sasa.
Maana mtafurahi na kucheka.
22 Watu watawachukia kwa sababu ninyi ni wa milki ya Mwana wa Adamu. Watawabagua na watawatukana. Watajisikia vibaya hata kutamka majina yenu. Mambo haya yatakapotukia, mjue kuwa baraka kuu ni zenu. 23 Ndipo mfurahi na kurukaruka kwa furaha, kwa sababu mna thawabu kuu mbinguni. Baba zao waliwafanyia manabii vivyo hivyo.
24 Lakini ole wenu ninyi matajiri,
kwa kuwa mmekwishapata maisha yenye raha.
25 Ole wenu ninyi mlioshiba sasa,
kwa kuwa mtasikia njaa.
Ole wenu ninyi mnaocheka sasa,
kwa kuwa mtalia na kuhuzunika.
26 Ole wenu watu wote wanapowasifu ninyi. Maana mababu zao waliwasifu manabii wa uongo vivyo hivyo daima.
© 2017 Bible League International