Book of Common Prayer
Iweni Kama Mungu Anavyotaka
12 Rafiki zangu wapendwa, daima mnatii yale mliyofundishwa. Kama mlivyotii nilipokuwa pamoja nanyi, ni muhimu zaidi na zaidi kwamba mtii wakati huu ambapo sipo pamoja nanyi. Hivyo ni lazima mwendelee kuishi katika namna inayoleta maana kwa wokovu wenu. Fanyeni hivi kwa wingi wa heshima na utii kwa Mungu. 13 Ndiyo, Mungu ndiye anayetenda kazi ndani na miongoni mwenu. Anawasaidia ninyi kutaka kutenda yanayomfurahisha, naye anawapa nguvu ya kuyatenda.
14 Fanyeni mambo yote pasipo kulalamika wala kubishana. 15 Nanyi mtakuwa watoto wa Mungu wasiolaumiwa na wasio na hatia. Ijapokuwa mnaishi mkiwa mmezungukwa na watu wasio waaminifu wasiojali thamani haki. Katikati ya watu hao mnang'ara kama mianga katika ulimwengu wenye giza, 16 nanyi mnawapa mafundisho yanayotoa uhai. Hivyo nitaona fahari juu yenu wakati Kristo atakapokuja tena. Ninyi ndiyo mtakaothibitisha kuwa kazi niliyoifanya haikukosa matokeo, ya kwamba nilishindana mbio na nikashinda.
17 Imani yenu inayatoa maisha yenu kama sadaka katika kumtumikia Mungu. Hata kama ni kweli kwamba sasa ninajimimina mimi mwenyewe kama sadaka ya kinywaji pamoja na sadaka yenu, ninayo furaha, na nitawashirikisha ninyi nyote furaha yangu. 18 Ninyi pia mnapaswa kufurahi na kunishirikisha furaha yenu.
Habari Kuhusu Timotheo na Epafrodito
19 Kwa baraka za Bwana Yesu, ninategemea kuwa nitamtuma Timotheo kwenu hivi karibuni. Naye atarejesha kwangu taarifa kuhusu ninyi ili nifurahi. 20 Sina mtu mwingine yeyote kama Timotheo, ambaye kwa dhati kabisa anayajali mambo yanayowahusu. 21 Wengine wote wanajishughulisha na maisha yao wenyewe. Hawajali kazi ya Yesu Kristo. 22 Mnafahamu Timotheo amejithibitisha kuwa ni mtu wa aina gani. Ametumika pamoja nami katika kuhubiri Habari Njema kwa njia ambavyo mwana angemtumikia baba yake. 23 Ninategemea kumtuma aje kwenu haraka baada ya kujua yatakayonipata. 24 Bwana hunifanya niwe jasiri ili niweze pia kuja kwenu haraka.
25 Kwa sasa, nadhani ni lazima nimrudishe Epafrodito kwenu. Ni mtumishi na mtenda kazi pamoja nami na askari mwenzangu katika jeshi la Bwana. Nilipotaka msaada, mlimtuma kwangu. Kama mjumbe wenu, alinihudumia mahitaji yangu. 26 Lakini sasa anataka kuwaona ninyi nyote tena. Ana wasiwasi sana kwa sababu mlisikia kuwa alikuwa mgonjwa. 27 Alikuwa mgonjwa karibu ya kufa. Lakini Mungu alimsaidia yeye na mimi ili nisiwe na huzuni zaidi. 28 Hivyo ninataka sana kumtuma kwenu. Ili mtakapomwona, mfurahi. Nami nitaacha kuwa na wasiwasi juu yenu. 29 Mkaribisheni kwa furaha nyingi katika Bwana. Waheshimuni watu kama Epafrodito. 30 Anapaswa kuheshimiwa kwa sababu alikaribia kufa akifanya kazi kwa ajili ya Kristo. Aliyaweka maisha yake katika hatari ili aweze kunisaidia. Ni msaada ambao msingeweza kunisaidia.
Yesu Apelekwa Uhamishoni Misri
13 Baada ya wenye hekima kuondoka, malaika wa Bwana akamjia Yusufu katika ndoto na kumwambia, “Damka! Mchukue mtoto pamoja na mama yake ukimbilie Misri kwa sababu Herode amedhamiria kumwua mtoto na sasa atatuma watu kumtafuta. Na mkae Misri mpaka nitakapowaambia mrudi.”
14 Hivyo Yusufu alidamka na kutoka kwenda Misri akiwa na mtoto na mama yake. Nao waliondoka usiku. 15 Yusufu na familia yake walikaa huko Misri mpaka Herode alipofariki. Hili lilitukia ili maneno yaliyosemwa na nabii yatimie: “Nilimwita mwanangu atoke Misri.”(A)
Herode Aua Watoto wa Kiume Katika Mji wa Bethlehemu
16 Herode alipoona kuwa wenye hekima wamemfanya aonekane mjinga, alikasirika sana. Hivyo akatoa amri ya kuua watoto wote wa kiume wenye umri wa miaka miwili au chini ya miaka hiyo katika mji wa Bethlehemu na vitongoji vyake. Herode alifahamu kutoka kwa wenye hekima kwamba walikuwa wameiona nyota miaka miwili kabla. 17 Hili likatimiza yale yaliyosemwa na Mungu kupitia nabii Yeremia aliposema:
18 “Sauti imesikika Rama,
sauti ya kilio na huzuni kuu.
Raheli akiwalilia watoto wake,
na amekataa kufarijiwa
kwa sababu watoto wake hawapo tena.”(B)
Yusufu na Familia Yake Warudi Kutoka Misri
19 Wakati Yusufu na familia yake wakiwa Misri, Herode alifariki. Malaika wa Bwana akamjia Yusufu katika ndoto 20 na akamwambia, “Damka! Mchukue mtoto na mama yake urudi Israeli, kwani waliojaribu kumwua mtoto wamekwisha kufa.”
21 Hivyo Yusufu alidamka na kumchukua mtoto Yesu na mama yake na kurudi Israeli. 22 Lakini Yusufu aliposikia kuwa Arkelao alikuwa mfalme wa Yuda baada ya baba yake kufa, aliogopa kwenda huko. Lakini baada ya kuonywa na Mungu katika ndoto, Yusufu aliondoka pamoja na familia yake akaenda sehemu za Galilaya. 23 Alikwenda katika mji wa Nazareti na kukaa huko. Hii ilitokea ili kutimiza maneno yale yaliyosemwa na manabii. Mungu alisema Masihi angeitwa Mnazareti.[a]
© 2017 Bible League International