Book of Common Prayer
Yesu Kuhani Wetu Mkuu
8 Hii ndiyo hoja tunayosema: Tunaye kuhani mkuu wa jinsi hiyo, anayeketi upande wa kuume[a] wa kiti cha enzi cha Mungu Mkuu mbinguni. 2 Kuhani wetu mkuu anahudumia katika Patakatifu pa Patakatifu.[b] Anahudumia katika mahali pa hakika kwa ibada[c] palipotengenezwa na Bwana, siyo na mtu yeyote duniani.
3 Kila kuhani mkuu anayo kazi ya kutoa sadaka na sadaka kwa Mungu. Hivyo kuhani wetu mkuu pia anahitajika kutoa kitu kwa Mungu. 4 Kama kuhani wetu mkuu angekuwa anaishi duniani, asingekuwa kuhani. Nasema hivi kwa sababu tayari hapa wapo makuhani ambao wanafuata sheria kwa kutoa sadaka kwa Mungu. 5 Kazi ambayo makuhani hawa wanafanya hakika ni nakala tu na kivuli cha yaliyoko mbinguni. Ndiyo sababu Mungu alimwonya Musa alipokuwa amejiandaa kujenga Hema Takatifu: “Uwe na uhakika kufanya kila kitu sawasawa na kielelezo nilichokuonesha kule mlimani.”(A) 6 Lakini kazi ambayo tayari imetolewa kwa Yesu ni kuu zaidi ya kazi iliyotolewa na makuhani hao. Kwa jinsi hiyo hiyo, agano jipya ambalo Yesu alilileta kutoka kwa Mungu kuja kwa watu wake ni kuu zaidi kuliko lile la zamani. Na agano jipya limeelemea katika ahadi bora zaidi.
7 Kama kusingekuwa na makosa katika agano la kwanza, kisha kusingekuwa na haja ya agano la pili. 8 Lakini Mungu aligundua kitu kilichokuwa na kasoro kwa watu, akasema:
“Wakati unakuja, asema Bwana,
nitakapofanya agano jipya na watu wa Israeli na watu wa Yuda.
9 Halitakuwa sawa na agano lililotengenezwa na baba zao.
Hilo ni agano nililowapa nilipowachukua kwa mkono na kuwatoa Misri.
Hawakuendelea kufuata agano nililowekeana nao,
na nikageuka mbali nao, asema Bwana.
10 Hili ni agano jipya nitakalofanya
na watu wa Israeli siku zijazo, asema Bwana:
Nitaziweka sheria zangu katika fahamu zao,
na nitaandika sheria zangu katika mioyo yao.
Nitakuwa Mungu wao,
nao watakuwa watu wangu.
11 Hakuna tena atakayemfundisha jirani yake au familia yake kumjua Bwana.
Watu wote, wakuu zaidi na wasio na umuhimu kabisa, watanijua.
12 Na nitawasamehe makosa waliyotenda,
na sitazikumbuka dhambi zao.”(B)
13 Mungu aliliita hili ni agano jipya, hivyo amelifanya agano la kwanza kuwa la zamani. Na chochote kilicho cha zamani na kisichokuwa na matumizi kiko tayari kutoweka.
Maria na Martha
38 Yesu na wafuasi wake walipokuwa wanasafiri, walifika katika kijiji kimoja. Mwanamke aitwaye Martha alimkaribisha nyumbani kwake. 39 Alikuwa na mdogo wake aliyeitwa Mariamu. Mariamu alikuwa amekaa karibu na Yesu akimsikiliza anavyofundisha. 40 Lakini Martha dada yake Mariamu alikuwa anashughulisha na shughuli mbalimbali zilizotakiwa kufanywa. Martha aliingia ndani na akasema, “Bwana, hujali kuona mdogo wangu ameniacha nifanye kazi zote peke yangu? Mwambie aje kunisaidia.”
41 Lakini Bwana akamjibu, “Martha, Martha, unasumbuka na kuhangaika kwa shughuli nyingi. 42 Lakini kitu kimoja tu ndicho cha lazima. Mariamu amefanya uchaguzi sahihi na kamwe hautachukuliwa kutoka kwake.”
© 2017 Bible League International