Book of Common Prayer
Siri ya Maisha Yetu
14 Ninatarajia kuja kwenu hivi karibuni. Lakini ninakuandikia maneno haya sasa, 15 ili kwamba, hata kama sitakuja mapema, utafahamu jinsi ambavyo watu wanapaswa kuishi katika familia[a] ya Mungu. Familia hiyo ni kanisa la Mungu aliye hai. Na Kanisa la Mungu ni msaada na msingi wa ukweli. 16 Ndiyo, Mungu ametuonesha siri ya maisha yanayompa heshima na kumpendeza Yeye. Siri hii ya ajabu ni ukweli ambao wote tunakubaliana nao:
Kristo[b] alijulikana kwetu katika umbile la kibinadamu;
alioneshwa na Roho[c] kuwa kama alivyojitambulisha;
alionwa na malaika.
Ujumbe kuhusu Yeye ulitangazwa kwa mataifa;
watu ulimwenguni walimwamini;
alichukuliwa juu mbinguni katika utukufu.
Maonyo juu ya Walimu wa uongo
4 Roho anasema wazi wazi kwamba katika siku za mwisho wengine watajitenga na imani. Watazitii roho zinazodanganya, na kufuata mafundisho ya mashetani. 2 Mafundisho hayo yanafundishwa na watu wanaodanganya na kuwafanyia hila wengine. Watu hawa waovu hawapambanui kati ya mema na maovu. Ni kana kwamba dhamiri zao zimeharibiwa kwa chuma cha moto. 3 Wanasema ni vibaya kuoa. Na wanasema kwamba kuna baadhi ya vyakula ambavyo watu lazima wasile. Lakini Mungu aliumba vyakula hivi, na wale wanaoamini na kuelewa ukweli wanaweza kuvila kwa shukrani. 4 Kila kitu alichokiumba Mungu ni chema, hakuna chakula kitakachokataliwa kama kikikubaliwa kwa shukrani. 5 Kila kitu alichokiumba kiliumbwa kitakatifu kwa namna alivyosema na kwa maombi.
Simulizi Kuhusu Ngano na Magugu
24 Kisha Yesu akatumia simulizi nyingine kuwafundisha. Yesu akasema, “Ufalme wa Mungu unafanana na mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. 25 Usiku ule, kila mtu alipokuwa amelala, adui wa yule mtu akaja na kupanda magugu katikati ya ngano kisha akaondoka. 26 Baadaye, ngano ikakua na vichwa vya nafaka vikaota juu ya mimea. Kisha mtumishi akayaona magugu. 27 Watumwa wa mwenye shamba wakaja na akasema, ‘Bwana ulipanda mimea mizuri kwenye shamba lako. Magugu yametoka wapi?’
28 Yule mtu akajibu, ‘Adui alipanda magugu.’
Wale watumwa wakauliza, ‘Je, unataka twende na kung'oa magugu?’
29 Akajibu, ‘Hapana, kwa sababu mtakapokuwa mnang'oa magugu, mtaweza pia kung'oa ngano. 30 Yaacheni magugu na ngano vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati wa mavuno nitawaambia wafanyakazi hivi: Kwanza, yakusanyeni magugu na kuyafunga pamoja ili myachome. Kisha kusanyeni ngano na kuileta ghalani mwangu.’”
Simulizi Nyingine ya Ufalme
(Mk 4:30-34; Lk 13:18-21)
31 Kisha Yesu akawaambia watu simulizi nyingine: “Ufalme wa Mungu unafanana na mbegu ya mharadali ambayo mtu alipanda katika shamba lake. 32 Ni mbegu ndogo sana kuliko mbegu zote. Lakini unapokua, ni kubwa kuliko mimea yote ya bustanini. Unakuwa mti mkubwa unaotosha ndege kuja na kutengeneza viota kwenye matawi yake.”
33 Kisha Yesu akawaambia simulizi nyingine: “Ufalme wa Mungu unafanana na chachu ambayo mwanamke huichanganya katika bakuli kubwa la unga ili atengeneze mkate. Chachu hufanya kinyunya chote kiumuke.”
34 Yesu alitumia simulizi akasema mambo yote haya kwa watu. Daima alitumia simulizi kuwafundisha.
© 2017 Bible League International