Book of Common Prayer
Umoja wa Mwili wa Kristo
4 Hivyo, mimi niliye mfungwa kwa ajili ya Bwana nawasihi mwishi kwa jinsi inavyowapasa watu wa Mungu, kwa sababu aliwachagua muwe wake. 2 Iweni wanyenyekevu na wapole siku zote. Mvumiliane na kuchukuliana ninyi kwa ninyi katika upendo. 3 Mmeunganishwa pamoja kwa amani na Roho. Jitahidini mwezavyo kudumu kuutunza umoja huo, mkiunganishwa pamoja kwa amani. 4 Kuna mwili mmoja na Roho moja, na Mungu aliwachagua ili muwe na tumaini moja. 5 Kuna Bwana mmoja, imani moja, na ubatizo mmoja. 6 Mungu ni mmoja na ni Baba wetu sote, anayetawala juu ya kila mtu. Hutenda kazi kupitia kwetu sote na ndani yetu sote.
7 Kristo alimpa kila mmoja wetu karama. Kila mmoja alipokea kwa jinsi alivyopenda yeye kuwapa. 8 Ndiyo maana Maandiko yanasema,
“Alipaa kwenda mahali pa juu sana;
aliwachukua wafungwa pamoja naye,
na akawapa watu vipawa.”(A)
9 Inaposema, “Alipaa juu,” inamaanisha nini? Inamaanisha kuwa kwanza alikuja chini duniani. 10 Hivyo Kristo alishuka chini, na ndiye aliyekwenda juu. Alikwenda juu ya mbingu za juu zaidi ili avijaze vitu vyote pamoja naye. 11 Na Kristo huyo huyo aliwapa watu hawa vipawa: aliwafanya wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kwenda na kuhubiri Habari Njema, na wengine kuwa wachungaji[a] ili wawafundishe watu wa Mungu. 12 Mungu aliwapa hao ili kuwaandaa watakatifu wa Mungu kwa ajili ya kazi ya huduma, kuufanya imara mwili wa Kristo. 13 Kazi hii inabidi iendelee hadi wote tutakapounganishwa pamoja katika lile tunaloliamini na tunalolijua kuhusu Mwana wa Mungu. Lengo letu ni kufanana na mtu mzima aliyekomaa na kuwa kama Kristo tukiufikia ukamilifu wake wote.
14 Ndipo tutakapokuwa si kama watoto wachanga. Hatutakuwa watu ambao nyakati zote hubadilika kama meli inayochukuliwa na mawimbi huku na kule. Hatutaweza kuathiriwa na fundisho lolote jipya tutakalosikia kutoka kwa watu wanaojaribu kutudanganya. Hao ni wale wanaoweka mipango ya ujanja na kutumia kila aina ya mbinu kuwadanganya wengine waifuate njia iliyopotoka. 15 Hapana, tunapaswa kusema ukweli kwa upendo. Tutakua na kuwa kama Kristo katika kila njia. Yeye ni kichwa, 16 na mwili wote unamtegemea yeye. Viungo vyote vya mwili vimeunganishwa na kushikanishwa pamoja, huku kila kiungo kikitenda kazi yake. Hili huufanya mwili wote ukue na kujengeka katika upendo.
Yesu Afukuza Mashetani Kutoka Kwa Watu Wawili
(Mk 5:1-20; Lk 8:26-39)
28 Yesu alifika ng'ambo ya ziwa katika nchi walimoishi Wagadarini.[a] Hapo wanaume wawili waliokuwa na mashetani ndani yao na kuishi makaburini walimwijia Yesu. Watu hao walikuwa hatari sana na watu hawakuitumia njia iliyopita karibu na makaburi yale. 29 Wakapaza sauti na akasema, “Unataka nini kwetu, Mwana wa Mungu? Umekuja kutuadhibu kabla ya wakati uliopangwa?”
30 Mbali kidogo na mahali hapo lilikuwepo kundi la nguruwe waliokuwa wanapata malisho yao. 31 Mashetani yakamsihi Yesu yakasema, “Ikiwa utatufukuza kutoka ndani ya watu hawa, tafadhali tuache tuwaingie wale nguruwe.”
32 Ndipo akawaamuru na akasema, “Nendeni!” Wale mashetani wakatoka ndani ya wale watu na kuwaingia nguruwe. Kisha kundi lote la nguruwe likaporomoka ziwani na nguruwe wote wakazama na kufa. 33 Wachungaji waliokuwa wakiwachunga wale nguruwe wakakimbia. Wakaenda mjini na kuwaambia watu kila kitu kilichotukia, hasa juu ya wanaume wale wawili waliokuwa na mashetani. 34 Kisha watu wote mjini walikwenda kumwona Yesu. Walipomwona, walimsihi aondoke katika eneo lao.
© 2017 Bible League International