Book of Common Prayer
Ni lazima Tupendane Sisi kwa Sisi
11 Haya ni mafundisho mliyoyasikia toka mwanzo: Ni lazima tupendane sisi kwa sisi. 12 Msiwe kama Kaini. Aliyekuwa upande wa Mwovu. Kaini alimwua ndugu yake. Lakini kwa nini alimwua? Ni kwa sababu alichokifanya Kaini kilikuwa cha kiovu, na alichokifanya nduguye kilikuwa cha haki.
13 Kaka zangu na dada zangu, msishangae watu wa dunia hii wakiwachukia. 14 Tunafahamu ya kuwa tumevuka kutoka mautini na kuingia uzimani. Tunafahamu hili kwa sababu tunapendana sisi kwa sisi kama ndugu wa kike na wa kiume. Yeyote asiyewapenda kaka zake na dada zake angali amekufa. 15 Kila anayemchukia nduguye anayeamini ni muuaji. Nanyi mnajua kuwa hakuna muuaji aliye na uzima wa milele.
16 Hivi ndivyo tunavyojua jinsi upendo wa kweli ulivyo: Yesu aliyatoa maisha yake kwa ajili yetu. Hivyo nasi tunapaswa kuyatoa maisha yetu, kwa ajili ya ndugu wa kike na wa kiume katika familia ya Kristo. 17 Itakuwaje pale muumini tajiri mwenye fedha za kutosha kupata mahitaji yake yote akamwona dada ama kaka yake aliye maskini na asiye na fedha za kutosha kupata mahitaji yake yote. Endapo muumini huyu tajiri hatamsaidia muumini yule maskini, basi ni wazi kwamba upendo wa Mungu haumo ndani ya muumini yule tajiri. 18 Watoto wangu, upendo wetu usiwe wa maneno na kuongea tu. Hapana, upendo wetu unapaswa kuwa halisi. Hatuna budi kuuonyesha upendo wetu kwa mambo yale tunayofanya.
Kifo cha Lazaro
11 Alikuwepo mtu aliyekuwa mgonjwa aliyeitwa Lazaro. Huyo aliishi katika mji wa Bethania, mahali ambapo Mariamu na dada yake Martha waliishi. 2 (Mariamu ni mwanamke yule aliyempaka Bwana manukato na kumpangusa miguu kwa nywele zake.) Ndugu wa Mariamu alikuwa Lazaro, ambaye sasa alikuwa mgonjwa. 3 Kwa hiyo Mariamu na Martha walimtuma mtu kwa Yesu kumwambia, “Bwana, rafiki yako mpendwa Lazaro ni mgonjwa.”
4 Yesu aliposikia hayo alisema, “ugonjwa huu sio wa kifo. Isipokuwa, ugonjwa huu ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Hili limetokea ili kuleta utukufu kwa Mwana wa Mungu.” 5 Yesu aliwapenda Martha, na dada yake na Lazaro. 6 Hivyo aliposikia kwamba Lazaro ni mgonjwa, akabaki alipokuwa kwa siku mbili zaidi, 7 kisha akawaambia wafuasi wake, “Inatupasa kurudi tena Uyahudi.”
8 Wakamjibu, “Lakini Mwalimu, ni muda mfupi tu uliopita viongozi wa Wayahudi pale walijitahidi kukuua kwa mawe. Sasa unataka kwenda huko tena?”
9 Yesu akajibu, “Yako masaa kumi na mawili ya mchana katika siku. Yeyote anayetembea mchana hatajikwaa na kuanguka kwani anamulikiwa na nuru ya ulimwengu huu. 10 Lakini yeyote anayetembea usiku atajikwaa kwa sababu hana nuru[a] inayomwongoza.”
11 Kisha Yesu akasema, “Rafiki yetu Lazaro sasa amelala, lakini nitakwenda ili nimwamshe.”
12 Wafuasi wake wakajibu, “Lakini, Bwana, kama amelala ataweza kupona.” 13 Walifikiri kwamba Yesu alikuwa na maana kwamba Lazaro alikuwa amelala usingizi, lakini Yeye alikuwa na maana kuwa amefariki.
14 Kisha hapo Yesu akasema wazi wazi, “Lazaro amekufa. 15 Na ninafurahi sikuwepo hapo. Ninafurahi kwa ajili yenu kwa sababu sasa mtaniamini mimi. Twendeni kwake sasa.”
16 Ndipo Tomaso, pia aliyeitwa “Pacha”, akawaambia wafuasi wengine, “Nasi pia tutaenda kule kufa pamoja na Yesu.”
© 2017 Bible League International