Tito 2
Neno: Bibilia Takatifu
Mafundisho Sahihi
2 Lakini wewe, mafundisho yako ni lazima yawe sahihi. 2 Wafundishe wazee kuwa na kiasi, watulivu, wenye busara na tha biti katika imani, upendo na subira. 3 Hali kadhalika akina mama wazee wawe na mwenendo wa unyenyekevu. Wasiwe wachonganishi, wala wasiwe watumwa wa pombe; bali waonyeshe mfano mwema. 4 Hivyo wawafundishe akina mama vijana kuwapenda waume zao na watoto wao 5 na kuwa wenye kiasi na safi, wakitumia wakati wao kushughulika nyumbani mwao. Wawe wema na watii kwa waume zao, ili neno la Mungu lisije likadharauliwa kwa ajili yao. 6 Vile vile uwahimize vijana kuwa na kiasi. 7 Katika mambo yote wewe mwenyewe uwe kielelezo cha matendo mema. Uonyeshe usa hihi na uthabiti katika mafundisho yako. 8 Maneno yako yawe na kina na mantiki safi, mtu asiweze kuyatoa kasoro na hata yule anayepinga aaibike kwa kukosa lo lote baya la kusema juu yetu.
9 Wahimize watumwa kuwatii mabwana wao na kuwapendeza katika mambo yote; wasijibishane nao 10 wala kuwaibia, bali watumwa waonyeshe kuwa wanaweza kuaminika kabisa ili katika kila hali mafundisho ya Mungu Mwokozi wetu yapate sifa njema.
11 Kwa maana neema ya Mungu iletayo wokovu imedhihirishwa kwa watu wote. 12 Neema hiyo inatufundisha kukataa uovu na tamaa za dhambi, tupate kuishi maisha ya kiasi, ya haki na ya kumcha Mungu, katika ulimwengu huu. Wakati huo huo 13 tukingojea tumaini letu lenye baraka - kuja kwa utukufu wa Mungu wetu Mkuu na Mwokozi wetu, Yesu Kristo. 14 Yeye alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe katika uasi wote, na kutufanya tuwe safi kwa ajili yake; na tuwe watu wake kabisa, ambao wana juhudi katika kutenda mema.
15 Fundisha mambo haya; himiza na kemea kwa mamlaka yote. Mtu ye yote asikudharau.
Yohana 1:35-42
Neno: Bibilia Takatifu
Wanafunzi Wa Kwanza Wa Yesu
35 Kesho yake, Yohana alikuwapo pale pamoja na wanafunzi wake wawili. 36 Alipomwona Yesu akipita, alisema, “Tazameni! Mwana-Kondoo wa Mungu!” 37 Wale wanafunzi wawili walipomsikia Yohana akisema haya, walimfuata Yesu. 38 Yesu akageuka akawaona wakimfuata akawauliza, “Mnataka nini?” Wakamwambia, “Rabi’ 39 Yesu akawajibu, “Njooni mkapaone!” Ilikuwa yapata saa kumi jioni. Basi wakaenda wakaona alipokuwa anaishi, wakashinda naye siku hiyo.
40 Mmojawapo wa hao wanafunzi wawili waliomfuata Yesu baada ya kusikia maneno ya Yohana, alikuwa ni Andrea, ndugu yake Simoni Petro. 41 Mara baada ya haya Andrea alikwenda kumtafuta ndugu yake akamwambia, “Tumemwona Masihi,” yaani Kristo. 42 Andrea akampeleka Simoni kwa Yesu. Yesu akamtazama, akasema, “Wewe ni Simoni mwana wa Yohana; sasa utaitwa Kefa.” Tafsiri ya Kefa kwa Kigiriki ni Petro, maana yake ‘Mwamba’.
Read full chapterCopyright © 1989 by Biblica