Add parallel Print Page Options

Baadhi ya Watu Wawa na Mashaka na Mamlaka ya Yesu

(Mk 8:11-12; Lk 11:29-32)

38 Kisha baadhi ya Mafarisayo na walimu wa sheria wakamjibu Yesu. Wakasema, “Mwalimu, tunataka kukuona ukifanya miujiza kama ishara kuwa unatoka kwa Mungu.”

39 Yesu akajibu, “Watu wenye dhambi na wasio na imani hutafuta kuona muujiza kama ishara kutoka kwa Mungu. Lakini hakuna muujiza utakaofanyika kudhibitisha chochote kwao. Yona[a] ni ishara pekee itakayotolewa kwenu ninyi mlio wa kizazi kiovu cha leo. 40 Yona alikuwa ndani ya tumbo la samaki mkubwa kwa siku tatu, mchana na usiku. Vivyo hivyo, Mwana wa Adamu atakuwa kaburini kwa siku tatu, mchana na usiku. 41 Siku ya hukumu, ninyi watu mnaoishi leo mtalinganishwa na watu wa Ninawi, nao watakuwa mashahidi watakaoonyesha namna mlivyokosea. Kwa nini ninasema hivi? Kwa sababu Yona alipowahubiri watu hao, walibadili maisha yao. Na aliye mkuu kuliko Yona, yupo hapa lakini mnakataa kubadilika!

42 Pia, siku ya hukumu, Malkia wa Kusini[b] atasimama pamoja na wale wanaoishi sasa, atasababisha mhukumiwe kuwa na makosa. Ninasema hivi kwa sababu alisafiri kutoka mbali, mbali sana kuja kusikiliza mafundisho yenye hekima ya Sulemani. Nami Ninawaambia aliye mkuu zaidi ya Sulemani yuko hapa, lakini hamnisikii!

Read full chapter

Footnotes

  1. 12:39 Yona Au “Nabii Yona”, nabii katika Agano la Kale. Baada ya kukaa katika tumbo la samaki mkubwa kwa siku tatu alitoka akiwa mzima, kisha akaenda kwenye mji uliojaa uovu wa Ninawi kuwaonya watu huko kama alivyotumwa na Mungu. Kwa njia hiyo hiyo, Yesu angetoka kaburini siku ya tatu, ishara ya kuthibitisha ukweli wa ujumbe wake kutoka kwa Mungu.
  2. 12:42 Malkia wa Kusini Au “Malkia wa Sheba.” Alisafiri kama maili 1,000 (kilomita 1,600) ili kujifunza hekima ya Mungu kutoka kwa Sulemani. Tazama 1 Fal 10:1-13.