Matayo 17:1-9
Neno: Bibilia Takatifu
Yesu Abadilika Sura Mlimani
17 Baada ya siku sita, Yesu akawachukua Petro, Yakobo na Yohana ndugu yake Yakobo, wakaenda peke yao juu ya mlima mrefu. 2 Na wakiwa huko, Yesu akabadilika sura mbele yao, uso wake ukang’aa kama jua na nguo zake zikawa nyeupe kama mwanga. 3 Na mara Musa na Eliya wakawatokea, wakawa wakizungumza na Yesu. 4 Kisha Petro akamwambia Yesu, “Bwana, ni vizuri kwamba sisi tuko hapa. Ukiniruhusu, nitatengeneza vibanda vitatu hapa: kimoja chako, kingine cha Musa na kingine cha Eliya.”
5 Petro alipokuwa bado akizungumza, ghafla, wingu linalong’aa likatanda juu yao na sauti ikatoka kwenye wingu hilo ikasema, “Huyu ni mwanangu mpendwa, ambaye nimependezwa naye; msikilizeni yeye.” 6 Wanafunzi waliposikia haya walianguka chini kifudifudi wakajawa na hofu. 7 Lakini Yesu akaja, akawagusa, akawaambia, “Inukeni. Msiogope.” 8 Walipoinua macho yao hawakumwona mtu mwingine isipokuwa Yesu peke yake.
9 Walipokuwa wakishuka mlimani, Yesu akawaambia, “Msimwambie mtu ye yote maono haya mpaka mimi Mwana wa Adamu nitakapofufuliwa kutoka kwa wafu.”
Read full chapterCopyright © 1989 by Biblica