Wimbo Wa Musa Na Mwana-Kondoo

15 Ndipo nikaona ishara nyingine mbinguni, ishara kubwa na ya ajabu: malaika saba wenye maafa saba ya mwisho, kwa maana, maafa hayo yanakamilisha ghadhabu ya Mungu.

Na nikaona kitu kama bahari ya kioo imechanganyika na moto. Na kando ya hiyo bahari, walikuwa wamesimama wale watu waliom shinda yule mnyama na sanamu yake pamoja na namba ya jina lake. Walikuwa wameshika vinubi walivyopewa na Mungu. Nao waliimba wimbo wa Musa, mtumishi wa Mungu na wimbo wa Mwana-Kondoo wakisema, ‘ ‘Matendo yako Bwana Mungu Mwenyezi, ni makuu na ya ajabu! Njia zako wewe Mfalme wa Mataifa ni za haki na za kweli! Ni nani asiyekucha wewe Bwana na kulitukuza jina lako? Kwa kuwa wewe peke yako ni mtakatifu. Mataifa yote yatakuja na kukuabudu kwa kuwa matendo yako ya haki yamekwisha dhihirishwa.”

Baada ya hapo nikatazama, nikaona mbinguni Hekalu, yaani hema ya ushuhuda, imefunguliwa. Basi wale malaika saba wenye maafa saba wakatoka humo Hekaluni wakiwa wamevaa nguo za kitani safi zing’aazo na vifuani mwao walivaa mikanda ya dhahabu. Kisha mmoja wa wale viumbe wanne wenye uhai, akawapa wale mal aika saba mabakuli saba ya dhahabu yalizojaa ghadhabu ya Mungu aishiye milele na milele. Na Hekalu ilijaa moshi uliotokana na utukufu na uweza wake, wala hakuna mtu aliyeweza kuingia Hekaluni mpaka yale maafa saba ya wale malaika saba yakamilike.

Malaika Wenye Mapigo ya Mwisho

15 Ndipo nikaona ajabu nyingine mbinguni, ilikuwa kubwa na ya kushangaza. Walikuwepo malaika saba wenye mapigo saba. Haya ni mapigo ya mwisho kwa sababu baada ya haya, ghadhabu ya Mungu itakuwa imekwisha.

Niliona kama bahari ya kioo iliyochanganyikana na moto. Wale wote waliomshinda mnyama na sanamu yake na namba ya jina lake walikuwa wamesimama kando ya bahari. Watu hawa walikuwa na vinubi walivyopewa na Mungu. Waliuimba wimbo wa Musa, mtumishi wa Mungu na wimbo wa Mwanakondoo:

“Mambo unayotenda ni makuu na ya kushangaza,
    Bwana Mungu Mwenye Nguvu.
Njia zako ni sahihi na za kweli,
    mtawala wa mataifa.
Watu wote watakucha wewe, Ee Bwana.
    Watu wote watalisifu jina lako.
    Mtakatifu ni wewe peke yako.
Watu wote watakuja na kusujudu mbele yako,
    kwa sababu ni dhahiri kuwa wewe hutenda yaliyo haki.”

Baada ya hili nikaona hekalu, mahali patakatifu pa Mungu[a] mbinguni. Likiwa wazi; kisha malaika saba wenye mapigo saba wakatoka nje ya hekalu. Walikuwa wamevaa kitani safi inayong'aa. Wamevaa mikanda mipana ya dhahabu vifuani mwao. Kisha mmoja wa viumbe wenye uhai wanne akawapa malaika bakuli saba za dhahabu. Bakuli zilikuwa zimejaa ghadhabu ya Mungu, aishiye milele na milele. Hekalu lilikuwa limejaa moshi uliotoka katika utukufu na nguvu ya Mungu. Hakuna ambaye angeweza kuingia hekaluni mpaka mapigo saba ya malaika saba yamemalizika.

Footnotes

  1. 15:5 mahali patakatifu pa Mungu Kwa maana ya kawaida, “Hema ya Ushuhuda”. Tazama Hema Takatifu katika Orodha ya Maneno. Soma Kut 25:8-22.